Jumamosi, 23 Septemba 2023

MWENYEKITI MAHAKAMA SPORTS ATEMA NYONGO TIMU IKIINGIA MAFICHONI

Na Faustine Kapama-Mahakama

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) imeingia kambini rasmi kujiwinda na mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayotarajia kuanza mwishoni wa mwezi huu wa Septemba, 2023 mkoani Iringa.

Akizungumza katika viwanja vya mazoezi vilivyoko Shule ya Sheria maeneo ya Mawasilisho jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewahimiza wanamichezo wote kufanya mazoezi kwa kujituma na kuzingatia programu ya mwalimu ili kumwezesha kuunda kikosi imara kitakachoiwakilisha vyema Mahakama ya Tanzania kwenye mashindano hayo.

"Tumeingia rasmi kambini, wachezaji wote tuliowaita kutoka Mikoa yote wameshawasili na tayari wameshaanza mazoezi katika michezo mbalimbali tunayotarajia kushiriki kwenye mashindano. Niwakumbushe wanamichezo wenzangu kuwa mashindano ya SHIMIWI siyo lelemama," alisema.

Dede amemtaka kila mwanamichezo kuonyesha bidii na umakini kwenye mazoezi ili aweze kuchaguliwa kwenye timu itakayoundwa na kupeperusha bendera ya Mahakama kwenye mashindano hayo kwani anaamini watakuwa na timu imara ambayo itashangaza wengi.

"Mwaka huu tuna vijana wazuri sana kwenye kila mchezo. Kinachotakiwa ni wao kumshawishi mwalimu ili awaingize kwenye kikosi chake. Tunao wataalamu ambao wanamfuatilia kila mmoja namna anavyojitoa kuitumikia Mahakama na kuonyesha nidhamu. Niwaombe wenzagu wakubali kujitoa na kuonyesha uzalendo kwa Mahakama ili tuweze kupata ushindi kwenye michezo yote,” amesema.

Ameonya wapinzani wao kuwa safari hii wataambulia makalayi kwani wamejipanga kuzoa kila kitu kwenye mashindano hayo. "Hatutakuwa na utani na mtu safari hii, waanze kujiandaa kisaikolojia na hatutakubali hujuma ya aina yoyote. Ingawa tutapiga pale pale kwenye mshono, tunawaomba wenzetu wavumilie kitakachowakuta,"alionya.

Michezo ambayo Mahakama Sports inatarajia kushiriki katika mashindano hayo ni Kamba Wanaume, Kamba Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha Wanaume na Wanawake pamoja na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.

Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede akieleza jambo kuhusu timu yake.
Mazoezi ya kuvuta kamba yakiendelea (juu na picha mbili chini).


Mwalimu wa Timu ya Mpira wa Miguu Spear Mbwembwe akizungumza na wachezaji.
Viongozi wengine wa Mahakama Sports wakifuatilia kwa makini kinachoendelea kwenye mazoezi.
Timu ya Netiboli ikiwa kwenye mazoezi makali chini ya Mwalimu wao (juu na chini).

Picha za pamoja (juu na chini) baada ya mazoezi makali.


  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni