Ijumaa, 29 Septemba 2023

TIMU YA MAHAKAMA NETIBOLI ‘YAUA MTU’ SHIMIWI

·Yaikandamiza Ras Kilimanjaro vikapu 49

Na Faustine Kapama-Mahakama, Iringa

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Netiboli imeyaanza vyema mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) leo tarehe 29 Septemba, 2023 baada ya kuiadhibu vikali timu ya Ras Kilimanjaro kwa jumla ya vikapu 49:6.

Katika mchezo huo uliochezwa majira ya alasili, timu ya Mahakama ilienda mapumziko ikiwa imeshatumbukiza vikapu 31kwa 2 na kuifanya kuongeza katika kipindi cha kwanza. 

Baada ya mapumziko, Mahakama Sports waliendelea kulisakama lango la Ras Kilimanjaro na waliwabana pumzi wapinzani wao wasifurutike hadi dakika ya mwisho.

Tupia tupia ya vikapu iliendelea, huku timu ya Mahakama ikiwachachafya wapinzani wao. Hadi mwamuzi anapuliza kipenga cha mwisho, Mahakama Sports ilikuwa imeshatupia vikapu 49 kwa 6 walizoambulia wapinzani wao, Ras Kilimanjaro. 

Akizungumza baada ya mchezo huo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema kipigo hicho kitaendelea na ni onyo kali kwa yule atakayethubutu kuwachezea.

"Nilisema tangu mwanzo, hatutamchekea mtu tusije tukaambulia mabua. Sisi tunachotaka ni makombe. Natoa onyo, wasijaribu kutuchezea, wataumia," Mwenyekiti Dede ameonya.

Naye Mwalimu wa Timu Paul Mathias amewapongeza vijana wake kwa kuonyesha mchezo mzuri na kuzingatia maelekezo aliyowapa. "Kama tutaendelea hivi, kuna mtu atakula mia hapa. Hatuna utani na mtu sisi," amesema. 

Wachezaji walioiwakilisha Mahakama ni Tatu Mawazo, Philomena Haule, Upendo Gustav, Nyangi Kisangenta, Shani Ally, Eunice Chengo na  Sophia Songoro. Waliokuwa kwenye mbao ndefu ni Leah Danda, Agnes Mwanyika, Lulu Nchimbi, Rohiba Makassi, Malkia Nondo, Angela Dismas, Akinzia Kimaro na Lucy Kibona.

Matokeo hayo ni mwendelezo wa ushindi ambao timu za Mahakama zimeupata. Mapema leo asubuhi, Mahakama Sports Kamba Wanaume na Kamba Wanawake walianza vizuri mashindano hayo baada ya kutembeza vipigo kwa wapinzani wao Ras Kigoma na Waziri Mkuu Sera ambao waliamua kuingia mitini.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotangazwa kuhusu mashindano haya, Mahakama Sports inatarajia kuvaana na timu zingine 14 ili kupata nafasi ya kutinga 16 bora.

Katika mpira wa miguu, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itachuana na Viwanda na Biashara, Maji, RAS Kigoma na Kilimo, timu ya netiboli ya Mahakama imepangwa katika kundi G na itapepetana na timu za Ardhi, RAS Kilimanjaro na Elimu.

Kwenye mchezo wa Kamba Wanaume, timu ya Mahakama imepangwa kundi A na itaumana na TAKUKURU, RAS Kigoma, Mawasiliano na Ardhi na Kamba Wanawake imepangwa kundi A pia na itakabiliana vilivyo na timu kutoka Tume ya Utumishi wa Umma, Waziri Mkuu Kazi na Tume ya Uchaguzi (NEC).

Mahakama Sports inashiriki katika michezo mbalimbali mwaka huu, ikiwemo Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha na Baiskeli.

Katika mashindano ya SHIMIWI yaliyofanyika mwaka jana jijini Tanga, timu ya Mahakama ya Tanzania ilizoa makombe saba baada ya kuibuka washindi katika michezo mbalimbali.

Michezo ambayo Mahakama Sports ilipata medali na makombe ni Kamba Wanawake walioibuka mshindi wa kwanza, Riadha Wanawake mita 3,000 mshindi wa kwanza, Tufe Wanawake mshindi wa kwanza, Kamba Wanaume walioshika nafasi ta pili, Mpira wa Miguu Wanaume walioshika nafasi ya pili na Bao Wanaume mshindi wa tatu.


Mashabiki wa Mahakama Sports wakinyanyua mtupiaji kinara wa vikapu,Tatu Mawazo baada ya kumalizika kwa mchezo. Picha chini wakimnyanyua mtupiaji mwingine hatari Philemona Haule.


Hawa hapa vijana wa Professa walioipeperusha vyema bendera ya Mahakama.


Tazama mpira unavyotumbukia kwenye kikapu.
Pasi ya kutafuta kikapu ilianzia hapa.
Ikapokelewa hapa.
Ikatupiwa hapa.

Hatimaye mpira ukajaa kwenye nyavu.

Mpira huooooo unatumbukia.
Ni shangwa kila kona.
Benchi la wachezaji likiongozwa na Katibu Msaidizi Theodosia Mwangoka (wa pili kulia) likowa na furaha tele. Kulia ni Mwalimu Paul Mathias akiendelea kutoa maelekezo kwa vijana wake.
Ilikuwa shangwa kila kona (juu na chini).


Hawa hapa Ras Kilimanjaro waliopokea kichapo.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni