Alhamisi, 12 Oktoba 2023

JENGO JIPYA LA MAHAKAMA YA WILAYA LIWALE LAKABIDHIWA RASMI

Na. Hilary Lorry Mahakama, Lindi

  • Afurahishwa na kiwango cha ujenzi uliofanywa na kampuni ya Uandisi ya Kiure.
  • Avutiwa na ubora na mwonekano wa Samani zilizotengenezwa kwa ustadi na ubora wa hali ya juu.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela akabidhiwa jengo jipya la Mahakama ya Wilaya ya Liwale na Kampuni ya Uhandisi ya Kiure mara baada ya kukamilika kwake.

Akizungumza wakati wa zoezi la makabidhiano hayo tarehe 10 Oktoba, 2023 Mtendaji huyo Bi. Mbeyela alisema, kampuni ya Uandisi ya Kiure imefanya kazi iliyopewa kwa weledi na ufanisi mkubwa na kuhakikisha kuwa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Liwale linakamilika katika viwango vilivyokubaliwa kwenye mkataba kwa ubora unaotakiwa.

“Nichukue fursa hii kuwapongeza kwa kazi nzuri mliyoifanya ubunifu unaonekana na juhudi kubwa ya kukamilisha kazi hii kwa kiwango kizuri na kutuwezesha makabidhiano haya kufanyika leo ya jengo la kisasa la kutolea huduma ya haki kwa wananchi likiwa katika hali bora ya kuridhisha na samani bora za kuvutia’’alisema Mtendaji Bi. Mbeyela.

Aidha, Mtendaji Mbeyela alimpongeza Mwakilishi wa Meneja wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Lindi pamoja na wasaidizi wake kwa usimamizi mzuri walioufanya katika kuhakikisha jengo la Mahakama ya wilaya ya Liwale linakamilika katika kiwango na ubora  uliokusudiwa kwa kuzingatia matakwa ya mkataba wa ujenzi huo.

Wakielezea kwa nyakati tofauti Meneja wa kampuni ya Uandisi ya Kiure Mhandisi Bw. Juma Mkwawa na mwakilishi wa Meneja wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Lindi Mhandisi Mshauri Bw. Greyson Kanyaburugo waliupongeza Uongozi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi na viongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara kwa uongozi mzuri na ushirikiano wa karibu waliouonyesha katika kipindi chote cha ujenzi jambo ambalo limerahisisha jukumu zima la kukamilisha ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya ya Liwale katika ubora uliokusudiwa.

Zoezi la Makabidhiano ya Jengo jipya la Mahakama ya Wilaya ya Liwale limefanyika kati ya Kampuni ya Uandisi ya Kiure ambao ni wajenzi wa jengo hilo, Kaimu  Meneja  wakala wa Majengo Tanzania (TBA) ambaye ni Mhandisi mshahuri wa ujenzi na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi.

Katika ziara hiyo ya kukabidhiwa jengo Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Mbeyela aliongozana na Afisa utumishi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bw.Stephano Morey, Afisa Utumishi Mahakama ya Wilaya ya Liwale Bi. Neema Nyakaka. 

Mwonekano wa Jengo jipya la kisasa Mahakama ya Wilaya ya Liwale.

Mhandisi Mshauri wa Wakala wa Majengo Lindi  Bw. Grayson Kanyaburugo (mwenye shati la dark blue) akipokea hati ya makabidhiano ya kukamilika kwa jengo kutoka kwa Mhandisi Juma Mkwawa  (kushoto) kutoka kampuni ya Uandisi ya Kiure huku Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela akishuhudia makabidhiano hayo.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela (katikati mstari wa mbele) akiwa katika picha ya pamoja na wahandisi na sehemu ya watumishi wa Mahakama walioshiriki kupokea jengo hilo.

Afisa Utumishi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bw. Stephano Morey aliyenyoosha mikono akitoa neno la pongezi kwa kazi nzuri waliyofanya kampuni ya Uandisi Kiure pamoja na wakala wa majengo Lindi katika kuhakikisha jengo linakabidhiwa katika ubora unatakiwa.

Afisa Utumishi Mahakama ya Wilaya ya Liwale Bi.Neema Nyakaka aliyeshika karatasi  akipitia nyaraka inayoonesha ni vitu gani amekabidhiwa.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela (kushoto) akikabidhiwa ufunguo wa Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Liwale.



(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni