Jumatatu, 16 Oktoba 2023

MAHAKAMA YA TANZANIA KUANZA MATUMIZI MFUMO WA KURATIBU MASHAURI KIELEKRONIKI NOVEMBA

Na Faustine Kapama – Mahakama.

MAHAKAMA ya Tanzania itaanza kutumia Mfumo mpya wa Kielektroniki wa Kusimamia Kesi (e-Case Management System) kuanzia Novemba 1, 2023 baada ya kukamilika kwa mashauri mwishoni mwa mwezi huu.

Kaimu Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye pia ni Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Sylvester Kainda ameeleza katika taarifa yake aliyoitoa leo tarehe 16 Octoba, 2023 kuwa kuanza kwa mfumo huo mpya ni sehemu ya maboresho yaliyofanywa na Mahakama katika maeneo mbalimbali.

"Lengo la mfumo huu ni kuboresha upatikanaji wa huduma za haki kwa wakati na kwa gharama nafuu. Moja ya maboresho hayo ni kutumia mifumo mbalimbali ya TEHAMA katika uendashaji wa shughuli zake, ukiwemo Mfumo wa Manejimenti ya Mashauri, yaani JSDS2," ameeleza.

Kaimu Msajili Mkuu ameeleza katika taarifa hiyo kuwa maendeleo hayo yanatokana na Mahakama kukamilisha ujenzi wa Mfumo huo ambao unachukua nafasi ya JSDS2 iliyokuwa inatumika tangu mwaka 2018.

“Ujenzi wa mfumo huu unalenga kuongeza tija katika shughuli za kimahakama, kupunguza gharama za kusikiliza mashauri  kwa upande wa Mahakama na wananchi, kupunguza muda wa kusikiliza mashauri na kusogeza zaidi huduma za kimahakama karibu na wananchi,” ameeleza.

Amesema kuwa matumizi ya Mfumo wa e-CMS pia yanalenga kutatua changamoto mbalimbali za JSDS2, zikiwemo kuongezeka kwa watumiaji na matumizi ya mfumo huo usioendana na muundo wa awali wa mfumo na teknolojia iliyotumika kuujenga na kutoruhusu mienendomya mashauri kuandikwa moja kwa moja kwenye mfumo.

Mhe. Kainda ameeleza kuwa Mfumo huo umekuja na muundo na teknolojia ya kisasa inayoendana na mahitaji ya sasa ya Mahakama na wadau wake na inaweza kusomana na mifumo mingine ya ndani ya Mahakama na ile ya wadau muhimu, wakiwemo Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Wakala wa Usajili, Ufilisi na Dhamana (RITA) na Taasisi nyingine.

Kaimu Msajili Mkuu huyo ameeleza katika taarifa yake kuwa hatua hiyo itarahisisha upatikanaji wa taarifa muhimu kutoka katika taasisi na kuwawezesha wadau kupata taarifa mbalimbali za mashauri kwa urahisi.

Amesema mfumo huo mpya pia utarahisisha usajili wa mashauri kwa njia ya mtandao, upangaji wa mashauri kwa Majaji na Mahakimu na utaruhusu mienendo ya mashauri kuandikwa moja kwa moja kwenye mfumo na kuihifadhi kielektroniki.

“Katika Mfumo huo kuna fomu maalum (template) za nyaraka mbalimbali zinazotumika mahakamani, zikiwemo hati za shauri, hati za mashtaka, hukumu zitakazojazwa na watumiaji ndani ya mfumo. Lengo ni kupunguza upakiaji wa nyaraka nyingi kwenye mfumo unaoweza kuathiri utendaji wake,” Mhe. Kainda amesema.

Amesema Mahakama ya Tanzania itakapoanza matumizi ya e-CMS, madirisha yake ya msaada kwa wananchi (viosk) wasioweza kutumia mfumo huo mpya yanayotumika kuwasaidia wananchi wasioweza kutumia wenyewe JSDS2 yataendelea kutumika pia.

Mahakama ya Tanzania ilianza kupima e-CMS tarehe 2 Oktoba, 2023 katika Mahakama zote nchini na zoezi hilo bado linaendelea. Mahakama inawaalika wananchi na wadau wake kufungua mashauri ya majaribio kwa wingi kwenye mfumo huo unaopatikana kupitia anuani ya https://cmstraining.judiciary.go.tz/.

Kipindi cha majaribio kitaendelea hadi tarehe 31 Octoba, 2023 kwa lengo la kupata changamoto zitakazojitokeza katika matumizi ya mfumo huo ili ziweze kufanyiwa kazi kabla ya kuanza kutumika rasmi kwa mfumo huu hapo tarehe 1 Novemba, 2023.

Kaimu Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye pia ni Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Sylvester Kainda.


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni