Na Lydia Churi- Tume ya Utumishi wa Mahakama- Geita
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Kamishna wa
Tume ya Utumishi wa Mahakama Mhe. Mustapher Siyani ametoa rai kwa jeshi la
Polisi nchini kulinda amani na kuzuia uvunjifu wa amani wakati wa urtekelezaji
wa amri halali za Mahakama.
Akizungumza na Wadau wa Utoaji haki hivi karibuni mkoani
Geita wakati wa ziara ya Tume, Jaji Kiongozi alisema jeshi la Polisi pamoja na
Viongozi wa Serikali wanayo nafasi kubwa katika kazi ya utoaji haki hususan
kwenye mashauri ya madai.
”Polisi baada ya kujiridhisha juu ya uwepo wa amri halali
za Mahakama, wanayo nafasi kubwa ya kusaidia kutunza amani”, alisema Jaji
Kiongozi.
Alisema uzoefu katika maeneo mbalimbali nchini unaonesha
kuwa jeshi la Polisi limeshindwa kusaidia kutoa ulinzi wakati wa utekelezaji wa
amri za Mahakama hali inayoweza kuleta uvunjifu wa amani au amri za Mahakama
kutotekelezwa.
Alisema kuna nyakati nyingine katika baadhi ya maeneo,
Madalali wa Mahakama wamekuwa wakizuiwa na viongozi wa Serikali kutekeleza
wajibu wao au viongozi hao kutoa amri kinzani na kuanzisha mchakato mwingine wa
haki ikiwemo kusuluhisha baada ya amri ya Mahakama kuwa imeshatolewa.
Jaji Kiongozi alisema matarajio ya Tume na Mahakama ni
kuona Viongozi wa Serikali pamoja na Jeshi la Polisi, kama wadau muhimu wa
Mahakama hawatakuwa vikwazo katika utekelezaji wa tuzo na amri za Mahakama.
Aliongeza kuwa ikitokea kutoridhishwa na hukumu viongozi hao waelekeze kutumia
fursa zilizopo kisheria kwa kukata rufaa.
Akizungumzia uanzishwaji wa Magereza, Mhe. Siyani alisema
Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani kama mdau wa Mahakama haina budi kusogeza
huduma hiyo ili kuziwezesha Mahakama za Mwanzo zilizo mbali na Magereza kufanya
kazi kwa ufanisi na kurahishisha uhifadhi wa wafungwa na Mahabusu.
Alisema Serikali inao wajibu wa kuweka mazingira bora ya
Mahabusu na wafungwa kama ambavyo kifungu cha 70 cha Sheria ya Mahakama za
Mahakimu kinavyoitaka Wizara ya Mambo ya
Ndani kuanzisha Mahabusu ya wafungwa
wanaohukumiwa na Mahakama za Mwanzo ili wapate hifadhi kabla ya kufikishwa
mahakamani.
Akizungumzia ushiriki wa viongozi wa Serikali katika
kujenga imani ya wananchi kwa Mhimili wa Mahakama, Jaji Kiongozi alisema mtaji
wa Mahakama ni imani ya wananchi kwa kuwa wananchi wasipokuwa na imani
hawataitumia Mahakama na hivyo
kusababisha uvunjifu wa amani.
Alisema Sheria ya Usimamizi wa Mahakama namba 4 ya mwaka
2011 imewapa wakuu wa Mikoa na Wilaya nafasi ya kusimamia maadili ya Maafisa
Mahakama ili kuongeza imani ya wananchi kwa Mhimili wa Mahakama. Aliwataka Viongozi hao kutumia majukwaa
mbalimbali waliyonayo kuifanya Mahakama iaaminike kwa wananchi.
”Mahakama inayoaminika ni msingi wa utulivu na amani
katika nchi na amani na utulivu ni msingi wa maendeleo ya nchi”, alisema Mhe.
Siyani.
Tume ya Utumishi wa Mahakama imemaliza ziara ya siku nne
ya kikazi katika mikoa ya Kagera na Geita yenye lengo la kujitangaza uwepo wake
na kukutana na Wajumbe wa Kamati za Maadili ya Maafisa Mahakama ngazi ya Mikoa
na wilaya na wadau wa utoaji haki.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni