Jumatano, 1 Novemba 2023

NAIBU JAJI MKUU WA CHINA AMTEMBELEA JAJI MKUU WA TANZANIA

· Atoa wito kuimarisha ushirikiano katika haki za kimazingira

Na Faustine Kapama, Innocent Kansha- Mahakama, Dar es Salaam

Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping leo tarehe 1 Novemba, 2023 amemtembelea Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na kufanya naye mazungumzo mafupi yenye lengo la kuimarisha ushirikiano na kujifunza kuhusu masuala ya haki za kimazingira Tanzania.

Mhe. Linping aliwasili katika ofisi ya Jaji Mkuu wa Tanzania iliyopo katika jengo la Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam na kupokelewa na mwenyeji wake majira ya saa 4.00 asubuhi. Baada ya kupata utambulisho wa Viongozi mbalimbali wa Mahakama kutoka pande zote mbili, wageni hao walipitishwa kwenye andiko maalumu linalohusu haki za kimazingira Tanzania ambalo liliwasilishwa na Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri, Mhe. Desdery Kamugisha.

Pamoja na mambo mengine, Mhe. Kamugisha aliueleza ujumbe ulioongozwa na Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China kuhusu muundo wa Mahakama ya Tanzania, Mahakama zenye mamlaka ya kusikiliza mashauri ya haki za kimazingira, sheria zinazotumika na mikataba mbalimbali ya kimataifa ambayo Tanzania imesaini ili kulinda mazingira.

Alieleza pia mamlaka za kiserikali zilizoundwa kusimamia mazingira na alitoa uzoefu wa mashauri mbalimbali ambayo yameshatolewa maamuzi na Mahakama kuhusu utunzaji wa mazingira. Baada ya wasilisho hilo, Kiongozi huyo kutoka Jamhuri ya Watu wa China alitoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya Mahakama ya Tanzania na China kuhusu utawala wa sheria katika haki za kimazingira ili yasiendelee kuharibiwa zaidi.

"Kuna haja ya sisi kuimarisha ushirikiano wetu kuhusu utawala wa sheria katika haki za kimazingira kati ya China na Afrika na kati ya China na Tanzania kwa sababu haki za kimazingira ni za pamoja kwa kila binadamu," alisema.

Mhe. Linping alieleza kuwa China na Tanzania tayari ni washirika wa ushirikiano wa kimkakati, kwani Rais Xi Jinping ana uhusiano wa karibu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk Samia Suluhu Hassan.

“China na Tanzania ni marafiki wazuri na pia Tanzania ilichukua jukumu muhimu sana katika ulinzi wa mazingira duniani. Ninaamini kwamba tunapaswa pia kuimarisha ushirikiano wetu katika haki hasa haki za kimazingira kati ya Mahakama zetu, tunaamini kuna maeneo ambayo nyinyi mmepiga hatua katika haki za kimazingira, hivyo na sisi tungependa kujifunza,” alisema.

Kwa upande wake, Jaji Mkuu wa Tanzania alimueleza mgeni wake kuwa eneo la haki za kimazingira linahusishwa na sheria nyingi na kazi kubwa ya Mahakama ni kutafsiri sheria hizo.

“Kwa mfano, Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2002, Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori, Sheria ya Misitu, Sheria ya Hifadhi za Bahari, Sheria ya Uvuvi, pamoja na nyinginezo. Ukisoma sheria hizi zote, unaweza kutambua jinsi zinavyolinda baadhi ya vipengele vya mazingira,” alisema.

Mhe. Prof.Juma alibainisha baadhi ya maeneo ya ushirikiano kati ya Mahakama ya China na Mahakama ya Tanzania, ikiwemo teknolojia na pia uwepo wa vyama ndani ya Mahakama ambapo watu kwa watu wanaweza kushirikiana.

“Nimebaini kuwa mna Chama cha Majaji Wanawake wa China, pia na sisi tuna Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania. Kwa hiyo, haya ndio maeneo ambayo watu kwa watu wanaweza kushirikiana....

“Katika eneo la teknolojia, China iko mbele sana kuliko Tanzania na katika baadhi ya mageuzi yetu tumechunguza China imefanya nini, katika masuala ya uandishi na tafsiri ili kurahisisha upatikanaji wa haki. Kwa hivyo, hili ni eneo lingine ambalo tuna mengi ya kushirikiana,” Jaji Mkuu aliwaambia wageni wake.

Alimshukuru mgeni wake kwa kufika Tanzania na kutembelea Mahakama ya Tanzania, kwani wameshughulikia maeneo kadhaa ambayo ni muhimu, si tu kwa urafiki wa nchi hizo mbili bali pia ushirikiano kati ya Mahakama.

Viongozi wengine wa Mahakama waliofuatana na Jaji Linping katika ziara yake ni Jaji Mkuu na Rais wa Divisheni ya Mazingira na Rasilimali ya Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Jaji Liu Zhumei na Mkuu wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Bi. Li Wenwen.

Wengine ni Jaji Mwandamizi wa Divisheni ya Mazingira na Rasilimali katika Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Jaji Zhu Jing, Jaji Msaidizi, Divisheni ya Mazingira na Rasilimali katika Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China Qiu Yanjun, Ofisa kutoka Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China Huang Zheya, Meneja Mkuu wa Programu au Mkalimani, ClientEarth Liu Mengxing na Mwanasheria ClientEarth Jiang Boya.

Kwa upande wa Mahakama ya Tanzania, Viongozi waliohudhuria ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho, Mhe. Angelo Rumisha na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Wengine Kaimu Msajili Mkuu na Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Sylvester Kainda, Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri, Mhe. Desdery Kamugisha, Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Bw. Kalege Enock, Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi na Katibu wa Jaji Kiongozi, Mhe. Idan Mwilapwa.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kulia) akimpokea mgeni wake Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping alipowasili ofisini kwake leo tarehe 1 Novemba, 2023.
Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping akisalimiana na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (kulia).
Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping akisani kwenye kitabu cha wageni ofisini kwa Jaji Mkuu wa Tanzania jijini Dar es Salaam.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani akijitambulisha mbele ya ujumbe ulioongozwa na  Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping (haupo kwenye picha.
Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping akisalimiana na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (kulia).
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto) akimkabidhi zawadi Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping.

Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping (kulia) akimkabidhi zawadi Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akiagana na Naibu Jaji Mkuu na Makamu wa Rais wa Mahakama ya Upeo ya Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Yang Linping baada ya kukutana na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo kwenye picha). 

(Picha na Innocent Kansha na Faustine Kapama-Mahakama, Dar es Salaam)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni