Na Seth Kazimoto – Mahakama Kuu, Arusha
Jumla ya mashauri 87
yanatarajiwa kusikilizwa na kuamuliwa na Mahakama ya Rufani ya Tanzania kwenye
vikao maalum viwili vinavyofanyika katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki jijini
hapa.
Vikao hivi vilianza tarehe
30 Octoba, 2023 na vinatarajiwa kumalizika tarehe 17 Novemba, 2023. Miongoni
mwa mashauri yanayosikilizwa ni rufaa ya jinai namba 231/2022 iliyowasilishwa
na Mkurugenzi wa Mashtaka ambaye anapinga aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai
Lengai Ole Sabaya na wenzake wawili kuachiwa huru na Mahakama Kuu Arusha.
Rufaa hiyo imesikilzwa jana
tarehe 1 Novemba, 2023 na jopo la Majaji watatu linaloongozwa na Mwenyekiti wake,
Mhe. Jacobs Mwambegele. Majaji wengine ni Mhe. Ignas Kitusi na Mhe. Leila
Mgonya.
Shauri hilo lilianza kusikilizwa
kuanzia saa 4.00 asubuhi mpaka saa 10.00 alasiri na kuhudhuriwa na umati mkubwa
wa watu kiasi kwamba ukumbi namba nne uliokuwa umeandaliwa kutumika katika
kusikiliza kesi hiyo ulionekana kuwa mdogo.
Kufuatia hali hiyo, iliamuliwa
na Majaji hao kutumia ukumbi namba tatu ambao ni mkubwa zaidi japokuwa watu
wengi hawakupata nafasi za kukaa ikawabidi kusimama sehemu ya nyuma ya ukumbi.
Jopo hilo la Majaji
limesikiliza sababu tatu za rufaa zilizowasilishwa na upande wa mrufani, ambazo
ni kama Jaji wa Mahakama Kuu alikosea kusema usikilizaji wa awali ulikuwa
kinyume cha sheria.
Sababu zingine ni kama shitaka
la unyang’anyi wa kutumia silaha lilithibitishwa bila kuacha shaka na kama
kushindwa kumuuliza maswali shahidi wa pili wa upande wa mashtaka ilikuwa ni
batili.
Uamuzi unatarajiwa kutolewa
kabla ya Novemba 17, 2023 katika kipindi ambacho Mahakama ya Rufani itakitumia kusikiliza
mashauri mbalimbali ambayo yameletwa mbele yake na kupangiwa kusikilizwa. Jumla
ya mashauri 47 yanatarajiwa kusikilizwa katika kikao hicho.
Uamuzi wa Mahakama Kuu unaolalamikiwa ulitolewa na Jaji Ephery Kisanya ambaye aliwaachia huru wajibu rufaa katika shauri la jinai rufaa namba 129/2021 baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha kuwatia hatiani katika kesi ya jinai namba 105/2021.
Mbali na jopo hilo, kuna
kikao kingine cha Mahakama ya Rufani kinachoendelea hapa Arusha ambacho Mwenyekiti
wake ni Mhe. Stella Mugasha ambaye anaketi pamoja na Mhe. Patricia Fikirini na Mhe.
Lilian Mashaka. Kikao hiki kinatarajia kusikiliza na kuamua mashauri 40 yaliyo
mbele ya jopo hilo.
Bw. Lengai Ole Sabaya (katikati mwenye shati la bluu bahari) akiwa nje ya jengo la Mahakama Kuu Arusha baada ya kesi yake kusikilizwa.
(Habari hii imehaririwa na
FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni