Christopher Msagati – Mahakama, Manyara.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza amewasisitiza
watumishi wa Mahakama, Kanda ya Manyara kutimiza majukumu yao kwa weledi ili
kuendana na kasi ya mabadiliko ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano (TEHAMA) yanayotokea kila wakati Mahakamani.
Akizungumza
katika kikao kilichofanyika kwa njia ya Mahakama Mtandao leo tarehe 2 Novemba,
2023 katika ukumbi wa Mahakama Kuu, Mhe. Kahyoza amesema, mfumo mpya wa
usimamizi na uendeshaji wa mashauri ‘Advanced Case Management’ (e-CMS)
utarahisisha kwa kiwango kikubwa shughuli za utoaji haki kwa wananchi.
“Ninawasihi
watumishi wa Kanda ya Manyara tuwe mfano katika matumizi ya TEHAMA na hususani
katika huu mfumo mpya ambao tunauanza. Halitakuwa jambo la busara kama wenzetu
watayapokea mabadiliko haya na sisi tukabaki nyuma, ni wajibu wangu
kuwakumbusha kujiandaa vema kutumia mfumo huo mpya wa uendeshaji mashauri
utakao anza kutumi hivi karibuni” amesema Mhe. Kahyoza.
Akichangia
wakati wa kikao hicho, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Hanang, Mhe.
Arnold Kileo amemuhakikishi Jaji Mfawidhi Mhe. Kahyoza kuendelea kujitahidi kwa
kadri ya uwezo wao kuutumia mfumo huu mpya na kusema hawatamwangusha kwa sababu
wamejipanga vizuri kwa kujifunza tangu walipopokea maelekezo na kwamba wapo
tayari kutekeleza.
Mahakama Kuu Kanda ya Manyara kama zilivyo Kanda nyingine za Kimahakama Nchini ilipokea Maelekezo kutoka Ofisi ya Msajili Mkuu juu ya matumizi ya Mfumo wa Uendeshaji wa Mashauri ambao ni mbadala wa mfumo uliokuwa unatumika wa JSDS2.
Kikao
hicho amabcho kimefanyika kwa njia ya Mahakama Mtandao maarufu kama ‘Video Conference’
kimehudhuriwa na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya za Mkoa wa Manyara
ambazo ni Babati, Hanang, Mbulu, Kiteto na Simanjiro pamoja na Mtendaji wa
Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, Maafisa Utumishi, Maafisa Tawala wa Mahakama
zote katika kanda hiyo.
Sehemu
ya washiriki wa kikao kutoka Mahakama za Wilaya zilizopo Manyara wakionekana
katika Video wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe.
John Kahyoza (aliyeketi kwenye kiti).
Hakimu
Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Babati Mhe. Victor Kimario (kulia)
akifuatilia kikao kilichoendeshwa kwa njia ya Mahakama Mtandao, kushoto ni
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Babati, Mhe. Juma Mwambago.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Kahyoza akiendesha
kikao kwa njia ya Mahakama Mtandao na watumishi wa Mahakama Kuu, Kanda ya
Manyara, kikao kilichohusu matumizi ya Mfumo Mpya wa Uendeshaji wa Mashauri.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni