Jumatatu, 27 Novemba 2023

TAWJA WAWANOA MAJAJI, MAHAKIMU NAMNA YA UTATUZI KESI UNYANYASAJI WA KIJINSIA

Na. Mwinga Mpoli – Mahakama, Mbeya

Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA), wametoa mafunzo ya namna ya kushughulikia kesi za ukatili na unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto. Mafunzo hayo yamefanyika hivi karibuni mkoani Mbeya yakihusisha waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu Mbeya, Mahakimu kwa mkoa wa Mbeya na Songwe.

Akifungua mafunzo hayo, Afisa Tawala wa Mkoa wa Mbeya Bw. Lodric Mpogolo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Bw. Juma Homera alisema Uongozi wa Mkoa umefurahishwa sana kwa mafunzo hayo kufanyika mkoani hapo kwani Mbeya ni miongoni mwa mikoa mitano inayoongoza katika vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa Tanzania Bara, na pia Tanzania ikiwa inaelekea kuadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia. Hivyo mafunzo hayo yanaweza kuiwezesha jamii kujua haki na sheria na mtiririko wa hatua za kuchukua mtu anapokuwa na matatizo kama hayo mahakamani.

“Nimefurahi kuona kuwa mafunzo haya yamejumuisha Majaji na Mahakimu wa ngazi zote za Mahakama na wa jinsia zote mbili, kike na kiume. Hivyo nina matumaini kuwa washiriki watapata fursa ya kuchangia kubadilishana Mawazo ya namna bora ya kushughulikia kesi au migogoro inayohusiana na ukatili wa kijinsia”, alisema Bw. Mpogolo

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) Mhe. Barke Sehel alisema kuwa mafunzo hayo ni muhimu na ya kipekee yanayohusiana na namna ya kushughulikia kesi au matatizo ya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto hivyo yanahitaji umakini mkubwa.

Aidha, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya na Makamu Mwenyekiti wa TAWJA Mhe. Victoria Nongwa alimpongeza mgeni rasmi kwa kutumia muda wake kuja kuwaunga mkono Majaji na Mahakimu pamoja na washiriki wote wa mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Tanzania (TAWJA) Mhe. Jaji Barke Sehel akitoa neno wakati wa ufunguzi mafunzo ya namna ya kushughulikia kesi za ukatili na unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto.

Afisa Tawala wa Mkoa wa Mbeya Bw. Lodric Mpogolo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Bw. Juma Homera akitoa salamu za mkoa wa mbeya wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo.

Sehemu ya Washiriki wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa kwa umakini mkubwa katika mafunzo hayo.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya na Makamu mwenyekiti wa TAWJA Mhe.Victoria Nongwa akitoa neno la shukrani kwa washiriki wa mafunzo hayo

Afisa Tawala wa Mkoa wa Mbeya Bw. Lodric Mpogolo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Bw. Juma Homera  (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo, wengine walioketi ni Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu. 

Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni