Ijumaa, 3 Novemba 2023

UJENZI VITUO JUMUISHI SITA VIPYA WAIVA

·Mtendaji Mkuu, Wakandarasi wasaini mikataba

·Aonya ulipuaji, ataka kazi kukamilika kwa wakati

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama

Mahakama ya Tanzania leo tarehe 3 Novemba, 2023 imesaini mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 49 na makampuni manne kwa ajili ya ujenzi wa Vituo Jumusihi vya Utoaji Haki (IJCs) sita katika Mikoa ya Songea, Katavi, Geita, Njombe, Simiyu na Songwe.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ndiye aliyekuwa mgeni rasmi katika hafla ya utiaji saini mikataba hiyo iliyofanyika katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke. Viongozi mbalimbali wa Mahakama, wakiwemo Mkuu wa Kitengo cha Maboresho (JDU) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha na Mtendaji wa Mahakama ya Rufani, Bw. Victor Kategele wameshuhudia utiaji saini huo.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ametia saini mikataba hiyo sita kwa niaba ya Mahakama, huku maofisa wa kampuni nne za ujenzi, za ndani na nje ya nchi, wakisaini kwa makampuni zao na kushuhudiwa na Wakurugenzi na Wakuu wa Idara wa Mahakama ya Tanzania.

Akizungumza baada ya hafla hiyo, Prof. Ole Gabriel amewataka wakandarasi na washauri elekezi kuzingatia muda wa mkataba na mambo yote waliyokubaliana wakati wanapotekeleza ujenzi wa majengo hayo na kuhakisha kazi inafanyika kwa ubora unaostahili.

 “Muda ambao unaoneshwa katika mkataba ni miezi tisa, hatutapenda izidi hata siku moja. Tusingependa nyongeza ya muda, mabadiliko ya gharama, tungependa msisitize na kusimamia kazi zenu ninyi wakandarasi na washauri elekezi juu ya muda huu.

“Muda huu ndiyo Watanzania wanasubiri katika Mikoa hii sita wapate huduma kwenye majengo haya katika ngazi ya Mahakama Kuu. Naamini Wakandarasi hamtaniangusha na mtafanya kazi yenu vizuri na kuzingatia viwango na ubora unaotakiwa,” amesema.

Amewakumbusha wakandarasi hao kuwa utekelezaji wa mikataba hiyo inafuatiliwa kwa karibu na wadau na Viongozi wengi, akiwemo Mkuu wa Nchi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan na Mahakama, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.

“Hatutasita kumchukulia hatua mkandarasi yoyote au mshauri elekezi yoyote au mtumishi yoyote wa Mahakama atakayekuwa kikwazo katika kufanikisha malengo haya. Benki ya Dunia pia nao wanafuatilia ambao ndio wametoa mkopo nafuu kwa kazi hii,” Prof. Ole Gabriel amesema.

Mtendaji Mkuu amewatahadhalisha kutokuingia kwenye mikataba bila kuwasiliana na mteja, yaani Mahakama ya Tanzania na kuridhia kwa maandishi. Alitumia nafasi hiyo kuwaomba wale watakaotaka kuingia mikataba ya ziada na wakandarasi hao kuwa makini ili kuepuka changamoto ambazo zinaweza kujitokeza.

Ameishukuru Serikali, hususan Wizara ya Fedha chini ya Waziri Mwigulu Nchemba na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, kwa kuanzia na Katibu Mkuu wa zamani Emanuel Tutuba na baadaye Dkt. Natu Mwamba kwa kukubali kuondoa kodi kwenye gharama ya miradi hiyo ambayo imesaidia kuongeza idadi ya majengo.

Amewaomba wakandarasi wote kujitambulisha kwa viongozi wa Mikoa watakayokwenda kufanya kazi ili wasionekane wageni kwani kazi wanayofanya ni kusogeza huduma za utoaji haki kwa wananchi.

Kadhalika, amewasihi wananchi katika maeneo ya miradi hiyo kutoa ushirikiano wa kutosha ili kuwawezesha wakandarasi hao kutekeleza majukumu hayo kikamilifu na kujiepusha na uharibifu wa aina yoyote wakati wa kutekeleza miradi hiyo.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Maboresho, akizungumza katika hafla hiyo, ameeleza kuwa jumla ya Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki 14 vinatakiwa kujengwa katika kipindi hiki, lakini mikataba iliyosainiwa ni ya vituo sita.

Amesema mchakato wa kuwapata wakandarasi ulikuwa wa wazi kwani jumla ya zabuni 142 zilinunuliwa na walibaki wakandarasi wanne baada ya mchucho kufanyika ambao ndio wameitwa kusaini mikataba ya ujenzi wa majengo hayo mapya.

Wakandarasi hao na Mikoa wanayojenga kwenye mabano ni M/S Azhar Construction Company Limited Songea na Katavi), M/S Shandong Hi-Speed Dejian Group Co. Ltd (Geita na Njombe), M/S Riha Company Limited (Simiyu) na M/S Home Africa Investment Company Limited (Songwe).

“Mchakato huu haukuwa mwepesi na ulihitaji umakini ili kujiridhisha ili Mahakama ipate watu wenye uwezo na wanaostahili kwenda na kasi ya Mahakama,” amesema na kumshukuru Mkurugenzi wa Ugavi na Manunuzi na timu yake kwa kazi nzuri waliyoifanya.

Amesema kuwa kutiwa saini kwa mikataba hiyo ni kilele cha kazi ambayo imefanyika kwa kipindi cha zaidi ya miaka miwili iliyopita na kwa kuzingatia muda mchache uliokuwepo watumishi hao walifanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha kazi inafanikiwa.

Ametumia nafasi hiyo kuupongeza Uongozi wa Mahakama chini ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel na wote kwa kuwaunga mkono ili kufanikisha kazi hiyo.

Ujenzi wa Vituo hivyo utafanya Mahakama ya Tanzania kuwa na Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki 12. Kwa sasa kuna vituo sita ambavyo vinafanya kazi katika Mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza, Dodoma, Arusha na Morogoro.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wakandarasi wanne walisaini mikataba ya ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki sita vipya. Wengine katika picha ni Mwanasheria wa Mahakama, Mhe. Hassan Chuka (wa kwanza kulia) na Afisa Ugavi Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Damasia Ndunguru (wa kwanza kushoto).
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Mwanasheria wa Mahakama, Mhe. Hassan Chuka (kulia) wakisaini moja ya mikataba hiyo, huku Wakandarasi wakishuhudia. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza baada ya utiaji saini mikataba hiyo.

Mkuu wa Kitengo cha Maboresho (JDU) na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha akizungumza katika hafla hiyo.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel na Mwanasheria wa Mahakama, Mhe. Hassan Chuka (kulia) wakisaini moja ya mikataba hiyo, huku Wakandarasi wakishuhudia.  Picha chini Mkandarasi na Mwanasheria wa Mahakama wakisaini moja ya mikataba hiyo.

Zoezi la utiaji saini wa mikataba hiyo (juu na chini) likiendelea.

Sehemu nyingine ya zoezi la utiaji wa mikataba hiyo (juu na chini) likiendelea.


Sehemu ya Viongozi wa Mahakama ya Tanzania (juu na chini) ikishuhudia utiaji saini wa mikataba hiyo.
 

 (Picha na Innocent Kansha-Mahakama)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni