Jumanne, 23 Aprili 2024

MAJAJI WA RUFANI KUSIKILIZA JUMLA YA MASHAURI YA RUFANI 26 KIGOMA

Na Aidan Robert, Mahakama-Kigoma

Jopo la Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani wapo mkoani Kigoma katika kikao cha kusikiliza jumla ya mashauri 26 yaliyopangwa katika kikao hicho kilichoanza jana tarehe 22 Aprili, 2024 kwenye jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma. 

 

Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Flora Mtarania alisema jopo la Majaji hao limejipanga imara kusikiliza Jumla ya Mashauri 26, ambapo kati ya mashauri hayo 13 ni rufaa za jinai, sita ni rufaa za Madai, pamoja na maombi ya madai saba.

 

 “Jopo hilo la Majaji litasikiliza mashauri kwa muda wa majuma matatu kwa takribani siku 21 mfululizo,” alisema Mhe. Mtarania.

 

Aidha alisema, jopo hilo la Majaji wa Rufani wanakusudia kusikiliza mashauri matatu kwa siku yaani kuanzia jana tarehe 22 Aprili, 2024 hadi tarehe 10 Mei, 2024, ambapo wanatarajia kuhitimisha kikao hicho. 

 

Ameongeza kuwa, wamepanga kusoma Hukumu au maamuzi ya kikao hicho kwa mujibu wa ratiba hiyo ili kuendana na Mpango Mkakati wa Mahakama.


Majaji wa Mahakama ya Rufani waliopo katika vikao hivyo ni Mhe. Mwanaisha A. Kwariko ambaye ni Mwenyekiti wa jopo hilo wengine ni Mhe. Zephrine Galeba na Mhe. Dkt. Benhaji Masoud.

Mapema kabla ya kuanza kwa kikao hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile aliwaongoza watumishi wa Kanda hiyo kuwapokea Majaji watatu wa Mahakama ya Rufani waliofika kwa ajili ya kuanza vikao vya  Mahakama ya Rufani vilivyopangwa  kufanyika katika Kanda hiyo.

 


Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Mwanaisha Kwariko (Mwenyekiti) akiwa ofisini kwake mara baada ya kuwasili Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, akijiandaa kuanza kikao cha Mahakama ya Rufani jana tarehe 22 Aprili, 2024.


Picha ya pamoja ya Majaji wa Mahakama ya Rufani (katikati) ni Mhe. Mwanaisha Kwariko, Mwenyekiti wa Jopo, kulia kwake ni Jaji wa Rufani, Mhe. Zephrine Galeba akifuatiwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Rwizile, kushoto ni Jaji wa Rufani, Mhe. Dkt. Benhaji Masoud, akifuatiwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Francis Nkwabi.


Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Flora Mtarania akiwa ofisini kwake akijiandaa kuanza kwa kikao cha Mahakama ya Rufani mara baada ya kuwasili Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma.


Picha ya Wakili wa Kujitegemea, Bw. Sadik Aliki akijiandaa kwa ajili ya kikao cha Mahakama ya Rufani kilichoanza jana tarehe 22 Aprili, 2024 katika ukumbi namba moja uliopo katika jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma.


Picha ya pamoja ya Wasaidizi wa Sheria wa Majaji wa Mahakama ya  Rufani (katikati) ni Mhe. Khalfan Khalfan, kulia ni Mhe. Julieth Musiza na kushoto ni Mhe. Dorothy Mateni wakiwa katika maandalizi ya kuanza kikao cha Mahakama ya Rufani kilichoanza katika Kanda hiyo jana tarehe 22 Aprili, 2024.

 (Habari hii imehaririwa na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni