Jumatano, 23 Aprili 2025

MAJAJI WA RUFANI WAFUNDISHWA UMUHIMU WA KULINDA MILIKI BUNIFU

Na MWANAIDI MSEKWA na NAOMI KITONKA-Mahakama, Dar es Salaam

Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania leo tarehe 23 Aprili, 2025 wamekutana jijini Dar es Salaam kushiriki kwenye warsha kwa ajili ya kujadili na kuzungumzia masuala yanayohusu miliki bunifu (Intellectual Property).

Warsha hiyo inayofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Kambarage Nyerere imefunguliwa na Amiri wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija, kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamisi Juma.

Akizungumza kwenye ufunguzi huo, Mhe. Mwarija ameeleza kuwa lengo la warsha hiyo ni kujenga uwezo ndani ya Mahakama na kusisitiza kujitolea kwa pamoja kudumisha utawala wa sheria, haki miliki na kuweka haki miliki kama kichocheo cha nguvu cha uvumbuzi, ubunifu na mabadiliko ya kiuchumi

“Sisi kama Mahakama tunajihusisha na sheria hasa pale panapokuwa na migogoro kuhusiana na haki hizo na mpaka sasa maamuzi yetu yameenda WIPO na maamuzi 45 kutoka Mahakama zetu na wametoa baadhi ya muhtasari wa shughuli zao, mfano watu wa BRELA.”  ameongea Mhe. Mwarija.

Pia amewapongeza BRELA kwa kuendelea kuhusika na usaidizi muhimu katika kukuza mfumo thabiti na bunifu wa Mali Miliki kwa maslahi ya Taifa na Wanachi kwa sababu mashauri mengi yanamalizika kwenye Taasisi hiyo na rufaa chache zinazokuja Mahakama Kuu.

Naye Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, akizungumza katika hafla hiyo ameeleza kuwa kuna umuhimu mkubwa wa Majaji na maafisa wa Mahakama kushiriki mafunzo hayo kwa sababu Mahakama inayo jukumu la kuelewa masuala ya miliki bunifu na kudhihirisha kazi zake katika mzunguko wa utatuzi wa migogoro ya miliki bunifu na kuendana na mageuzi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa alizungumza kwa kusema, “Lengo la kukutana leo ni kubadilishana uzoefu na Majaji wa Mahakama ya Rufani ili kuelewa kitu gani hasa, kama BRELA wanahusika kwenye masuala ya umiliki na pale mashauri yanapofika mezani kwao inakuwa ni rahisi katika kuwasaidia kufanya maamuzi.

‘Matarajio yetu ni kwamba elimu hii itasaidia kutambua na kulinda bunifu za Watanzania wenzetu kushirikiana na WIPO na ARIPO, alisema.

Aliongeza pia kwa kusema mashirika hayo yanajulikana kimataifa na duniani kote ambapo ubunifu wowote unaowasilishwa unapitiwa kimataifa na sheria zote zinazotumika zinasaidia kufanya zoezi hilo kikamilifu.

“Kwenye Mahakama, mashauri ya miliki bunifu yanaonekana ni machache kwa sababu mashauri mengi yanamalizwa na kutolewa maamuzi na mengi yanasababishwa na uelewa wa wahusika na hukumu hutolewa, pale wahusika wakiridhika wengine huamua kunyamaza na ikishindikana shauri hukatiwa rufaa na kuja Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani, alisema.

Akizungumza kwenye ufunguzi huo, Mkurugenzi Msaidizi wa Tume ya Ushindani (FCC) Bi. Zaytun Kikila alisema “Tume yetu imeundwa kwa madhumuni ya kuendeleza na kulinda ushindani thabiti katika biashara na kumlinda mtumiaji dhidi ya mienendo inayohadaa na kutotenda haki katika uchumi wa soko na lengo kuu ni kuongeza ufanisi katika uzalishaji, usambazaji na ugavi wa bidhaa na huduma

..Pia tume imekabidhiwa jukumu la kudhibiti biashara ya bidhaa bandia kwa kutumia Sheria ya Alama za Bidhaa (Rajamu) Na. 20 ya mwaka 1963 na marekebisho yake na inaitambua Mahakama kama chombo muhimu katika utekelezaji wa sheria na kuongeza uaminifu kwa wawekezaji.

Takribani Majaji wote wa Mahakama ya Rufani wamehudhuria washa hiyo pamoja na Majaji kutoka Kenya, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Herbert, Naibu Wasajili na Viongozi wengine wa Mahakama.

Amiri wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija akitoa hotuba ya ufunguzi wa Warsha hiyo.

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akizungumza katika warsha hiyo.

Amiri wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija akiwa katika picha ya pamoja na wageni wa meza Kuu katika ufunguzi wa Warsha hiyo.

Amiri wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija-juu na chini- akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama ya Rufani.


Amiri wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija-juu na chini-akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni