Jumatano, 23 Aprili 2025

MAJENGO YA MAHAKAMA IRINGA KUFANYIWA UKARABATI

Na LUSAKO MWANG’ONDA-Mahakama, Iringa

Mahakama ya Tanzania imeazimia kufanya ukarabati wa majengo yake yaliyopo mkoani Iringa, ikiwemo Mahakama Kuu.

Hayo yamebainishwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Angaza Mwipopo wakati wa makabidhiano ya mradi huo wa ukarabati wa majengo hayo.

Majengo yanayotegemewa kufanyiwa ukarabati huo ni yale yote yaliyo katika eneo la Viwanja vya Haki linalopatikana katika Mtaa wa Gangilonga katika Manispaa ya Iringa.

Majengo hayo ni pamoja na jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa na jengo la Mahakama ya Wilaya Iringa.

Akizungumza wakati wa makabidhiano ya mradi huo yaliyofanyika hivi karibuni na kuzikutanisha pande tatu, yaani Mahakama ya Tanzania, Mshauri wa Mradi ambaye ni TBA na Mkandarasi ambaye ni Kampuni ya Sadtech, Jaji Mwipopo alisema ukarabati huo unakwenda kuondoa adha mbalimbali ambazo watumiaji wa majengo hayo walikuwa wanakumbana nazo ikiwa ni pamoja kuvuja maji wakati wa mvua.

Kwa mujibu wa Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Bw. Noel Shao, mradi wa ukarabati wa majengo hayo utakuwa ni kipindi cha miezi nane, hivyo ukarabati huo unategemewa kukamilika kabla ama ifikapo mwezi Disemba, 2025.

 

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Angaza Mwipopo akiwa kwenye kikao cha makabidhiano ya mradi wa ukarabati wa majengo ya Mahakama. Kikao kilishirikisha pande tatu; Mahakama, TBA (Mshauri) na Sadtech (Mkandarasi).

Kikao cha makabidhiano ya mradi kilichofanyika ndani ya jengo la Mahakama Kuu Kanda ya Iringa kilichofanyika baina ya Mahakama, TBA na Kampuni ya Sadtech. Kikao kiliongozwa na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa Mhe. Angaza Mwipopo (hayupo pichani).

Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Bw. Noel Shao akiwa anawatembeza wataalamu kutoka TBA na wale wa Kampuni ya ujenzi ya Sadtech maeneo mbalimbali ya majengo yanayotakiwa kukarabatiwa.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni