Jumanne, 8 Aprili 2025

TAWJA YAWASILI CAPE TOWN KUSHIRIKI MKUTANO MKUU WA MAJAJI WANAWAKE DUNIANI

Na MARY GWERA, Mahakama-Cape Town

Jumla ya Majaji na Mahakimu Wanawake 43 ambao ni wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wamewasili katika Mji wa Cape Town nchini Afrika Kusini leo tarehe 08 Aprili, 2025 kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 17 wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Duniani (IAWJ) unaotarajiwa kuanza kesho tarehe 09 Aprili, 2025.

Akizungumza katika mahojiano maalum leo tarehe 08 Aprili, 2025 mjini humo, Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel amesema kuwa, Mkutano huo unatarajiwa kuanza rasmi kesho tarehe 09 hadi 12 Aprili, 2025 na Mgeni Rasmi katika mkutano huo anatarajiwa kuwa, Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Mhe. Matamela Cyril Ramaphosa.

“Mkutano huu ni wa Chama cha Majaji na Mahakimu wanawake Dunianikwa ujumla unawakutanisha wanachama Majaji na Mahakimu wanawake duniani. Kwa upande wa Tanzania tutakaoshiriki katika Mkutano huo ni wanachama 43 idadi hii imejumuisha na wenzetu wa Zanzibar,” amesema Mhe. Sehel.

Kaulimbiu ya Mkutano huo inasema; ‘Wanawake na uongozi katika kushughulikia unyanyasaji wa kijinsia na mauaji ya dhidi ya wanawake.’

Mhe. Sehel amesema kuwa, mada mbalimbali zitawasilishwa katika mkutano huo ni pamoja na Majaji wanawake wanaongoza na kuleta mabadiliko katika Mahakama za Kimataifa, Wanawake katika Uongozi-Mahali pa Kazi Usalama kwa Maafisa wa Mahakama, Ubaguzi na biashara haramu ya binadamu na nyingine.

Kwa mujibu wa ratiba ya Mkutano huo, mmoja wa washiriki watakaotoa mada ya ‘Athari za teknolojia katika masuala ya ukatili wa kijinsia’ ni Mhe. Edith Mwalukasa ambaye ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Mwambao Bagamoyo.

Washiriki wa TAWJA wanaotarajia kuhudhuria mkutano huo ni baadhi ya wanachama ni kutoka kutoka Zanzibar, Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya, Arusha, Tabora na Mikoa mingine ya Tanzania Bara.

Mkutano wa aina hii huwakutanisha pamoja Majaji na Mahakimu Wanawake Duniani kote na hufanyika kila baada ya miaka miwili na huwapa fursa Majaji hao kujadili masuala mbalimbali yanayohusu haki za wanawake, ukatili wa kijinsia, watoto na jamii kwa ujumla.

         

Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel akiwa safarini kuelekea mjini Capetown nchini Afrika Kusini kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 17 wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Duniani (IAWJ).




Sehemu ya picha za Wanachama wa TAWJA wakiwa safari kuelekea Cape Town nchini Afrika Kusini kushiriki katika Mkutano wa 17 wa Chama cha Majaji na Mahakimu Duniani (IAWJ).






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni