Na HUBERT MAANGA, Mahakama-Mtwara
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe. Edwin Elias Kakolaki
amefanya ziara ya ukaguzi wa Mahakama za
Mkoa wa Mtwara wenye lengo la kukagua utendaji kazi katika mahakama za ngazi ya
chini kuhakikisha huduma ya utoaji haki inaenda vizuri.
Katika ziara hiyo iliyofanyika tarehe 23, 24
na 30 Juni, 2025, Jaji Kakolaki aliambatana
na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana,
Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Bw. Yusuph Msawanga, Msaidizi wa
Sheria wa Jaji Mfawidhi, Mhe. Stella Shindika na Afisa TEHAMA, Bw. Hubert D.
Maanga.
Miongoni mwa Mahakama zilizokaguliwa ni Mahakama
ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mahakama ya Wilaya Tandahimba, Newala, Nanyumbu,Masasi,
Mahakama ya Mwanzo Mahuta, Kitangali, Chikundi na Nanyumbu.
Katika
ziara yake, Mhe. Kakolaki alikutana na watumishi ambapo alipokea taarifa za
utendaji kazi, kusikiliza changamoto zinazowakabili na kutoa maelekezo
mbalimbali. Aidha, kila Mahakama ya Wilaya, alizungumza na Mahakimu ambapo
aliwasisitizia utendaji wenye uadilifu.
Aidha,
Jaji Mfawidhi huyo aliwapongeza watumishi kwa utendaji kazi mzuri hasa kumaliza
mashauri kwa wakati, kutokuwa na mlundikano wa mashauri, unadhifu na ubunifu wa
kuhifadhi nakala laini za hukumu na mwenendo wa shauri kwa Mahakama za Mwanzo.
"Kwa mwenendo huu, huduma ya Mahakama
itazidi kuonekana bora na kuzidi kuvutia wateja kwa maana, mteja atakapopata
haki yake na kuridhika na huduma yetu, atawashawishi hata wengine kuiamini Mahakama
katika utoaji haki," alisema Mhe. Kakolaki.
Kadhalika,
aliwapongeza Mahakimu kwa elimu inayotolewa redioni na sehemu nyingine kuhusu matumizi
ya mifumo na manufaa yake, huku akiwasihi Mahakimu hao kuendelea kuwapa elimu
wananchi, kuwaelewesha kuhusu matumizi ya TEHAMA katika usikilizaji mashauri na
jinsi gani inavyosaidia kuondoa gharama, kupunguza muda kuwezesha wateja kuendelea
na shughuli nyingine.
Katika kutekeleza
maagizo ya Jaji Mkuu, Jaji Mfawidhi huyo aliwataka Mahakimu wa Mahakama za
Mwanzo kuendelea kuchapa mashauri yote kwenye mfumo ili kurahisisha upatikanaji
wa nakala laini za mienendo hiyo.
Akizungumzia
hali ya Majengo ya Mahakama na vyombo vya usafiri, Mhe. Kakolaki alielekeza majengo
yatunzwe kwa kutumia fedha za ndani zinazopatikana na magari na pikipiki navyo vifanyiwe
matengenezo mara kwa mara ili viendelee kutumika.
“Aidha, Mahakama
za wilaya zihakikishe maeneo yote ya Mahakama ambayo hayana hati miliki,
yanapatiwa hati ili kurahisisha kuombea miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama,”
alisisitiza.
Katika
ziara yake Jaji Kakolaki alikagua miradi miwili ya ujenzi ya Mahakama ya Mwanzo
Kitangari na Chikundi inayoendelea katika Mkoa wa Mtwara na kuridhika na kasi sambamba
na usimamizi wa ujenzi wa miradi hiyo.
Jaji Mfawidhi huyo alitembelea pia Magereza ya Lilungu, Newala na Masasi ambapo alipokea taarifa na kusikiliza changamoto za wafungwa na mahabusu na kuwashauri kujifunza na kukuza vipaji vya elimu ya ujasiriamali kwa manufaa yao watakaporudi uraiani.
Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Masasi wakimpokea Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki alipowasili katika Mahakama hiyo kwa lengo la ukaguzi.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (wa pili kushoto) akiteta machache na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Nanyumbu alipotembelea Mahakama hiyo hivi karibuni.
Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Tandahimba, Mhe. Joseph Waruku (aliyesimama) akiwasilisha taarifa ya Mahakama ya Wilaya hiyo mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati).
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akipanda mti katika viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Mahuta wilayani Tandahimba wakati alipotembelea Mahakama hiyo hivi karibuni.
Ukaguzi wa ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Kitangari iliyopo Wilaya ya Newala.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kulia) akizungumza na watumishi wa Mahakama ya Wilaya na Mkoa Mtwara.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wadau walipotembelea Gereza la Lilungu.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe. Edwin Kakolaki (wa tano kushoto).
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni