- Wakubali kusuluhishwa kwenye mgogoro wa kikazi kuhusu mapunjo ya mshahara
Na FAUSTINE
KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Mahakama Kuu ya Tanzania,
Divisheni ya Kazi, imefanikisha kusuluhisha mgogoro wa kazi kati ya Mwajiri, Kampuni
la Maendeleo Technologies inayoongozwa na Raia wa Urusi na Mwajiriwa, Bw.
Sergiy Lyeshchynskyy, ambaye ni Raia wa Ukraine, uliokuwa unahusu mapunjo ya
mishahara.
Usuluhishi huo uliongozwa
na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose
Mlyambina, kwenye shauri la kazi lililowakutanisha Kampuni hiyo na Kamishna wa
Kazi Tanzania, aliyemwakilisha Mwajiriwa huyo.
Kufuatia usuluhishi huo,
kampuni hiyo imekubali kulipa kwa awamu mbili Dola za Kimarekani 40,000, ambayo
ni zaidi ya Shilingi za Kitanzania milioni 100 kwa Mwajiriwa huyo, ambaye
alikuwa Fundi Mitambo katika kampuni hiyo inayojihusisha na kukodi mitambo ya
uchimbaji madini.
‘Mwajiri atamlipa
Mwajiriwa Dola za Kimarekani 20,000 siku au kabla ya tarehe 30 Juni, 2025 na
kiwango kitakachobaki cha Dola za Kimarekani 20,000 zitalipwa siku au kabla ya
tarehe 31 Julai 31, 2025 na kufanya jumla ya Dola za Kimarekani 40,000 ya madai
yote,’ inaeleza sehemu ya amri iliyotolewa hivi karibuni.
Katika makubaliano hayo,
Mwajiri pia amekubali kulipa gharama za shauri ambazo ni sawa na asilimia tano
ya Dola za Kimarekani 40,000 (Dola za Kimarekani 2,000) moja kwa moja kwa
Wakili wa Mwajiriwa.
Kadhalika, Mwajiri
amekubali kutoa tiketi ya ndege kwa mwajiriwa ya kurudi nchini kwake siku au
kabla ya tarehe 31 Julai, 2025.
‘Kama Mwajiri atashindwa
kutekeleza malipo hayo kama walivyokubaliana, Mwajiriwa atakuwa na haki ya
kuomba amri ya utekelezaji wa makubaliano hayo dhidi yake,’ inaeleza sehemu ya
amri hiyo.
Kukamilika kwa mgogoro
huu kunatoa somo kuwa usuluhishi una faida nyingi, ikiwemo kama ukisimamiwa
vizuri unawapatia nafasi waajiri na waajiriwa kujielekeza zaidi katika
shughuli za uzalishaji na kukuza uchumi endelevu kwa maslahi yao na kwa Taifa,
kuliko kupoteza muda mwingi pamoja na rasilimali fedha katika kufuatilia
migogoro kwenye hatua ya uamuzi na marejeo.
Usuluhishi pia ni njia
inayoweza kumaliza shauri kwa wakati na kwa urafiki na unaepusha upatikanaji wa
tuzo isiyotekelezeka, mfano: Wakati kesi inaisha mdaiwa wa hukumu ana kuwa hana
kitu cha kumlipa, mmiliki wa tuzo, kwa sababu ya muda mrefu ulitumika
kusikiliza shauri lake na pengine anakuwa amefirisika.
Aidha, usuluhishi
unaondoa uadui baina ya pande mbili zenye mgogoro na ukifanywa vizuri unaponya.


Hakuna maoni:
Chapisha Maoni