Na MARY GWERA,
Mahakama-Mwanza
Mahakama Kuu ya
Tanzania Divisheni ya Kazi inakusudia kuimarisha usimamizi wa utekelezaji wa
sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi ya mwaka 2003 pamoja na kanuni ili
kuendelea kuboresha mazingira bora ya kazi na kuleta ustawi kwa wafanyakazi.
Hayo yamebainishwa
na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose
Mlyambina leo tarehe 17 Julai, 2025 katika Hoteli ya Malaika jijini Mwanza
wakati akifunga Mafunzo ya Siku mbili kwa Majaji, Watendaji na Wadau wa
Mahakama yaliyotolewa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA).
“Siku ya jana
tuliweza kushuhudia, wakuu wa Taasisi hizi mbili Mahakama ya Tanzania na OSHA
wakiweka saini katika makubaliano ili OSHA kuweza kuendelea kutoa mafunzo ya
aina hii kwa muda wa miaka miwili. Hili ni tukio moja muhimu na la kihistoria,
hivyo Divisheni ya Kazi itaendelea kuimarisha mazingira ya kazi na usalama wa
wafanyakazi,” amesema Mhe. Dkt. Mlyambina.
Jaji Mfawidhi huyo
ameishukuru OSHA kwa kuendelea kushirikiana na Mahakama hususani Divisheni ya
Kazi na kuahidi kuwa, makubaliano hayo yatatekelezwa kupitia mafunzo endelevu
kwa Majaji, Mahakimu, Watendaji wengine wa Mahakama na wadau mbalimbali wa Haki
Kazi.
“Lengo la
kuendelea kutoa mafunzo hayo ni kuwajengea uelewa juu ya Sheria ya Usalama na
Afya Mahali pa Kazi na kanuni zake na hivyo kuwawezesha kusimamia haki kupitia
jukumu lao la msingi la kutafsiri sheria katika mashauri yanayohusiana na
usalama na afya mahali pa kazi,” ameeleza Jaji Mfawidhi huyo.
Kuhusu mafunzo
hayo yaliyohitimishwa leo, Mhe. Mlyambina amesema yalikuwa na malengo makuu
manne nayo ni pamoja na kujenga uelewa wa masuala ya usalama na afya kwa
washiriki hususani kuwawezesha kutambua vihatarishi vya magonjwa na ajali
katika shughuli za kila siku.
Amesema lengo
lingine ni kujenga uelewa juu ya Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi ya
mwaka 2003 pamoja na kanuni zake na viwango vya kimataifa vya usalama
na afya kazini (OSHA) na jinsi ya kuvitumia katika mazingira ya kazi
ya sasa, hasa kwa kuzingatia mabadiliko ya kidijitali na Akili Unde
(AI) miongoni mwa washiriki ili waweze kuitumia ipasavyo katika
kushughulikia mashauri yanayohusiana na masuala ya usalama na afya mahali pa
kazi.
“Lengo lingine ni kuandaa washiriki kuwa na ujuzi wa kisasa unaoendana na mabadiliko ya dunia ya kazi, ili waweze kuchangia katika mazingira ya kazi yenye amani, usalama, na tija — kwa manufaa ya pande zote na kwa maendeleo ya taifa kwa ujumla kufikia malengo ya Dira ya Taifa ambayo inasainiwa leo tarehe 17 Julai, 2025,” amesema Mhe. Dkt. Mlyambina.
Kadhalika, Jaji
Mfawidhi huyo ameongeza kwamba, mafunzo hayo yalilenga pia kuwawezesha
madereva, walinzi wa viongozi na wadau wa usafirishaji kuelewa na kutumia
teknolojia za kisasa kwa kufuata sheria, kuboresha usalama barabarani, kuongeza
ufanisi wa matumizi ya rasilimali, na kukuza ujuzi wa kidijitali kwa ajili ya
huduma bora na salama za usafirishaji.
Aidha, Mhe. Dkt.
Mlyambina amewakumbusha washiriki wa mafunzo hayo kuhusu mada zilizotolewa na
kuwasihi kuzingatia na kutekeleza kwa vitendo yote waliyofunzwa.
Miongoni mwa mada
zilizotolewa wakati wa mafunzo hayo yaliyofunguliwa tarehe 16 Julai, 2025 na
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani
ni pamoja na Itifaki, Mamlaka ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi
(OSHA), Vihatarishi vya Afya na Usalama Mahali pa Kazi na
kadhalika.
“Kwa kupitia mada
hizo ni wazi kuwa tumepata shule ya kutosha na kama alivyoshauri Jaji Kiongozi
ni matumaini yangu kuwa elimu hiyo itasaidia katika utekelezaji wa majukumu
yetu,” amesema Jaji Mfawidhi huyo.
Mhe. Dkt. Mlyambina amewashukuru washiriki wote wa mafunzo hayo kwa ushirikiano, usikivu na michango ya mawazo mbalimbali waliyoyatoa akiongeza kwa kusema, “ni matumaini yangu kuwa yale tuliyojifunza na kushirikiana hapa yatakuwa chachu ya maendeleo kwa kila mmoja wetu na kwa jamii kwa ujumla. Nawatakia kila kheri katika kutekeleza majukumu yenu ya kila siku na tuendelee kushirikiana kama wana Haki Kazi kwa ajili ya ustawi wa pamoja.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina akifunga Mafunzo ya Siku mbili kwa Majaji, Watendaji na Wadau wa Mahakama yaliyotolewa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) leo tarehe 17 Julai, 2025 katika Hoteli ya Malaika jijini Mwanza.
Sehemu ya Majaji, Watendaji na Wadau wengine wa Mahakama ambao ni washiriki wa Mafunzo hayo wakifuatilia hotuba iliyokuwa ikitolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (hayupo katika picha).
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni