- Serikali yasisitiza ushirikiano kuwezesha upatikanaji wa haki kwa wananchi
Na HALIMA MNETE, Mahakama-Dodoma
Rais wa Chama cha
Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi na Naibu Mwanasheria Mkuu
wa Serikali, Mhe. Samweli Maneno wamewahimiza Mawakili wapya 774 kuutumikia
wito wao kwa uadilifu, uzalendo na ushirikiano katika kuboresha mfumo wa utoaji
haki nchini.
Akizungumza leo tarehe 05
Desemba, 2025, kwenye Sherehe za Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili hao wapya,
Wakili Mwabukusi amesema kuwa kazi ya uwakili siyo ajira ya kawaida bali ni
wito wa kuhudumia haki na jamii kwa mujibu wa Katiba na misingi ya utawala
bora.
Akizungumza katika Sherehe
hito, Rais wa TLS amesema kuwa kuwakilisha wateja ni kuhudumia haki, kulinda
misingi ya katiba na kuendeleza utawala wa sheria unaozingatia usawa na haki za
binadamu.
“Wakili ni mtu ambaye
kiwango chake cha uzalendo kwa Taifa, ujasiri katika kusimamia na kulinda
Katiba na sheria, pamoja na utawala bora na haki za binadamu, kinapaswa kuwa
cha juu kuliko kitu kingine chochote,” amesema Wakili Mwabukusi.
Ameongeza kuwa, Mawakili
ni nguzo muhimu katika jamii na wanapaswa kuishi kwa maadili, uadilifu na
ukweli, huku akisisitiza kuwa uaminifu kwa wateja, mahakama na jamii ni mtaji
mkubwa unaojengwa kwa muda mrefu lakini unaweza kupotea kwa kosa moja.
Wakili Mwabukusi pia
amewakumbusha mawakili wapya umuhimu wa elimu endelevu, kujitolea kwa ajili ya
wanyonge, kuheshimu mahakama na kushirikiana kwa karibu na mihimili ya dola kwa
maslahi ya taifa. Aidha amesisitiza kuwa Chama cha Wanasheria Tanganyika si
mpinzani wa Serikali bali ni mshirika katika kusimamia utawala wa sheria, haki
za binadamu na utawala bora.
Kwa upande wake, Naibu
Mwanasheria Mkuu wa Serikali amewapongeza mawakili wote waliokubaliwa pamoja na Taasisi
ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo (Law School of Tanzania) kwa kazi kubwa ya
kuwaandaa wanataaluma hao.
Amesema mafanikio ya Mawakili wapya ni matokeo ya jitihada za muda mrefu za walimu, wazazi, walezi,
Serikali na wadau mbalimbali waliochangia katika safari yao ya kitaaluma.
Bw. Maneno ameishukuru
Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kuipa kipaumbele sekta ya Sheria,
akieleza kuwa ongezeko la mawakili nchini litaongeza kasi ya upatikanaji wa
haki kwa wananchi na kusaidia kupunguza changamoto za kisheria.
Ameeleza kuwa ofisi ya
Mwanasheria Mkuu wa Serikali itaendelea kushirikiana bega kwa bega na mawakili
pamoja na wadau wa haki jinai na madai katika kuboresha mfumo wa utoaji haki
nchini.
“Mawakili ni kiungo
muhimu kati ya wananchi na mahakama. Mna nafasi kubwa sana ya kuhakikisha haki
inapatikana kwa ufanisi na kwa kuzingatia sheria, usawa na haki za binadamu,”
amesema.
Kauli za Viongozi hao
zimekuja wakati ambapo Taifa linaendelea kushuhudia ongezeko la idadi ya
mawakili, hali inayotajwa kuwa chachu ya kuimarisha utawala wa sheria, amani na
maendeleo ya jamii kwa ujumla.
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Samweli Maneno akizungumza wakati wa Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wa Kujitegemea wapya 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi akitoa hotuba yake wakati wa Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wa Kujitegemea wapya 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.
Baadhi ya makundi ya Mawakili wa Kujitegemea wapya wakifuatilia hotuba zilizokuwa zikitolewa wakati wa Sherehe ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wa Kujitegemea wapya 774 leo tarehe 05 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mabeyo jijini Dodoma.
(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)









Hakuna maoni:
Chapisha Maoni