Ijumaa, 27 Februari 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAFANIKISHA MAGEUZI MAKUBWA

  • Malengo yote ya Mradi wa Maboresho wa Mahakama yamefikiwa kwa asilimia 100

Na JAMES BUSANYA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imepiga hatua kubwa katika kuimarisha utendaji na upatikanaji wa huduma za haki kwa wananchi, ikifikia kiwango cha juu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya Mahakama katika mageuzi ya kisheria.

Hayo yamesemwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho (JDU), Mhe. Dkt. Angelo Rumisha, tarehe 25 Februari, 2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, wakati anawasilisha taarifa ya maboresho kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Mhe. Dkt. Rumisha alieleza kuwa malengo yote 12 ya maendeleo ya mradi (PDO) yamefikiwa au kuzidi matarajio, huku kiwango cha kuridhika kwa wananchi kikiongezeka kwa asilimia kubwa, ukilinganisha na awali, jambo ambalo ni ishara kubwa ya mafanikio katika kuboresha ufanisi, uwazi na upatikanaji wa haki katika ngazi zote za Mahakama nchini.

Katika kuimarisha miundombinu na upatikanaji wa huduma, Jaji Rumisha alieleza kuwa Mradi wa Maboresho ya Mahakama umejikita katika kuunda miundombinu ya kisasa kwa kujenga Mahakama za Mwanzo 94 na Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki (IJCs) 18.

Hatua hizi zimeleta mapinduzi makubwa kwa wananchi, kwani sasa huduma za kisheria zinapatikana karibu na maeneo yao, kupunguza vikwazo vya kijiografia na gharama kubwa za usafiri ambazo zilikuwa changamoto kubwa kabla ya mwaka 2015,” alisema.

Mhe. Dkt. Rumisha alibainisha kuwa kupungua kwa muda wa mashauri na kuongeza ufanisi, mageuzi ya kimkakati, kidijitali na uboreshaji wa usimamizi wa kesi umepunguza muda wa kusubiri kupata haki kwa kiasi kikubwa.

Alitoa mfano wa kesi za biashara, ambapo katika Mahakama Kuu kuna punguzo la asilimia 64, kesi za familia Mahakama za Mwanzo zimepungua kutoka siku 120 hadi 35, punguzo la asilimia 71, na kesi Mahakama ya Wilaya zimepungua kutoka siku 40 hadi 15, punguzo la asilimia 63.

Punguzo hili limefanikiwa kutokana na matumizi ya TEHAMA, Mahakama tembezi (Mobile Courts), upanuzi wa Mahakama na kuanzishwa kwa IJCs katika Mikoa mbalimbali. Hii imesaidia wananchi kupata haki kwa haraka,” alisema.

Mhe. Dkt. Rumisha alieleza kuwa katika mageuzi ya kidijitali na uboreshaji wa utendaji, Mradi umejikita pia katika mabadiliko ya kidijitali ya mfumo wa Mahakama. Alieleza kuwa mfumo wa mapitio na tathimini ya utendaji Maofisa wa Mahakama (JOPRAS) hutoa uchambuzi wa muda halisi wa utendaji.

Aidha, alisema kuwa uchapishaji wa uamuzi mtandaoni umeongezeka kutoka asilimia 3 hadi 88, jambo linaloongeza uwazi, uwajibikaji na uelewa wa wananchi kuhusu mfumo wa kisheria.

Alieleza kuwa kiwango cha kuridhika kwa huduma za Mahakama kwa wananchi kimeongezeka kutoka asilimia 61 hadi asilimia 88 kutokana na kupungua kwa muda wa mashauri, hasa ya biashara na familia.

Kuhusu mlundikano wa mashauri, Mhe. Dkt. Rumisha alieleza kuwa kesi zilizokuwa zinasubiri zimepungua kutoka asilimia 10 mwaka 2021 hadi asilimia 5 mwaka 2025, hivyo kesi zote zenye umri zaidi ya miezi 24 ni asilimia 5 pekee. Alisema kuwa punguzo hilo limefanikiwa kupitia usimamizi makini wa mtiririko wa kesi, upanuzi wa Mahakama tembezi, na kuanzishwa kwa IJCs katika maeneo mbalimbali.

Alibainisha athari za kiuchumi na kijamii kupitia Mahakama tembezi na IJCs, ambapo gharama kwa wananchi zimepunguzwa kwa kiasi kikubwa, jambo ambalo inawawezesha wananchi kupata haki bila kero za kifedha, huku akiba ya Taifa ikifikia mabilioni ya shilingi.

Mhe. Dkt. Rumisha alieleza kuwa Mahakama imeendelea kudumisha imani ya wananchi kupitia uwajibikaji thabiti na mifumo ya maoni inayoruhusu michango ya umma na kwamba njia mbalimbali za maoni, ikiwemo sanduku la mapendekezo na maoni ya mtandaoni, zimeimarisha uhusiano na wananchi na kuleta uwazi katika utendaji wa Mahakama.

Alihitimisha kwa kusema kwamba mageuzi hayo ya kimkakati, kidijitali na kiutawala yameonesha wazi kwamba mfumo wa Mahakama unaweza kubadilika na kuendeshwa kwa ufanisi, uwazi, uwajibikaji na upatikanaji wa haki karibu na wananchi. 

Mafanikio hayo ni ishara tosha kwamba Tanzania ina mfumo wa Mahakama wa kisasa, unaojali wananchi, unaotumia teknolojia na mbinu za kisasa za usimamizi wa mashauri na unaendelea kuboresha maisha ya raia kwa kuharakisha upatikanaji wa haki, kupunguza gharama na kuongeza kuridhika kwa umma.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho (JDU), Mhe. Dkt. Angelo Rumisha (juu na chini), akiwasilisha taarifa ya maboresho kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.


Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania (juu na picha mbili) wakichangia mada kwenye kikao hicho.



Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni