Alhamisi, 26 Februari 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAIMARISHA MIUNDOMBINU KUPITIA MIRADI YA MAJENGO

Na HALIMA MNETE – Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imeendelea kutekeleza kwa kasi miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama katika Mikoa na Wilaya mbalimbali nchini, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha upatikanaji wa haki kwa wananchi na kuboresha mazingira ya utoaji huduma za kimahakama.

Hayo yalibainishwa jana tarehe 25 Februari, 2026 na Mkurugenzi wa Uendelezaji na Matengenezo ya Majengo wa Mahakama, Mhandisi Moses Lwiwa, wajati anawasilisha Taarifa ya Miradi ya Majengo ya Mahakama katika Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kilichofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Akiwasilisha taarifa hiyo mbele ya Mgeni Rasmi, Jaji Mkuu wa Mahakama Tanzania, Mhe. George Masaju, na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt Mustapher Mohmed Siyani, ambaye ni Mwenyekiti wa kikao hicho, Mhandisi Lwiwa alieleza kuwa Mahakama inaendelea na utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa Vituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJCs) katika Mikoa mbalimbali pamoja na majengo ya Mahakama za Mwanzo na Wilaya (SBCs), kwa lengo la kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi na kupunguza changamoto za miundombinu.

Kwa upande wa miradi ya IJCs, alibainisha kuwa miradi katika Mikoa ya Geita, Njombe, Simiyu, Songea, Pemba, Singida, Songwe na Lindi ipo katika hatua za mwisho za utekelezaji, ambapo baadhi ya majengo tayari yamekamilika na yanafanya kazi, huku mengine yakiwa katika kipindi cha uangalizi baada ya kukamilika (Defect Liability Period).

Alieleza kuwa Mahakama imeweka mkakati wa kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi hiyo kwa kushirikiana na Washauri Elekezi ili kuhakikisha mapungufu yote yanayojitokeza yanarekebishwa kwa wakati.

“Mwelekeo wetu ni kuhakikisha kila jengo linalokabidhiwa kwa Mahakama linakidhi viwango vya ubora vinavyotakiwa na linaweza kutumika kikamilifu katika utoaji wa huduma za haki,” alisisitiza.

Kwa upande wa miradi ya SBCs, Mhandisi Lwiwa alieleza kuwa miradi mingi iliyopo katika vifurushi mbalimbali (Packages na Lots) imekamilika kwa kiwango kikubwa na ipo kwenye kipindi cha uangalizi. Miradi hiyo inahusisha Mahakama za Mwanzo na Wilaya katika maeneo mbalimbali ikiwemo Kigoma, Mtwara, Manyara, Katavi, Rukwa, Mbeya, Dar es Salaam na Mikoa mingine.

Alifafanua kuwa miradi hiyo inatekelezwa kwa awamu na kwa mikataba maalum inayosimamiwa kwa karibu na Mahakama, kwa kushirikiana na Washauri Elekezi, ili kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana na majengo yanakuwa na ubora unaokidhi mahitaji ya watumishi na wananchi.

Katika hatua za mbele, amesema Mahakama imepanga kuimarisha usimamizi wa kiufundi katika miradi yote inayoendelea, kuweka msisitizo wa uwajibikaji kwa Wakandarasi pamoja na kuhakikisha kuwa marekebisho ya kasoro zozote zinazobainika katika kipindi cha uangalizi yanafanyika kwa wakati.

Utekelezaji wa miradi hiyo ya majengo unaenda sambamba na jitihada za Mahakama katika kufanya mageuzi ya kiutawala na kidijitali, kwa lengo la kujenga Mahakama imara yenye miundombinu ya kisasa, inayowezesha utoaji wa haki kwa ufanisi, uwazi na kwa wakati.

Mkurugenzi wa Uendelezaji na Matengenezo ya Majengo wa Mahakama, Mhandisi Moses Lwiwa, akiwasilisha Taarifa ya Miradi ya Majengo ya Mahakama katika Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kilichofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Majaji wa Wafawidhi wa Mahakama Kuu [juu na picha mbili chini] wakichangia mada kwenye kikao hicho.



Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni