Na HALIMA MNETE – Mahakama, Dodoma
Uboreshaji wa kidijitali unaoendelea
ndani ya Mahakama ya Tanzania unalenga siyo kuimarisha mifumo ya ndani ya
Mahakama pekee, bali pia kuendana moja kwa moja na mipango na dira ya maendeleo
ya Taifa kwa ujumla.
Hayo yalisemwa jana
tarehe 25 Februari, 2026 na Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
[TEHAMA], Bw. Kalege Enock, wakati akiwasilisha taarifa ya matumizi ya TEHAMA
katika usikilizaji wa mashauri kwenye Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi kinachofanyika
Makao Makuu ya Mahakama, jijini Dodoma.
Kikao hicho kinahudhuriwa
na Majaji Wafawidhi wa Kanda zote za Mahakama Kuu, kikiongozwa na Jaji Kiongozi
wa Mahakam Kuu ta Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, kama Mwenyekiti
wa kikao hicho huku Mgeni Rasmi akiwa ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania,
George Masaju.
Katika taarifa yake, Bw.
Kalege alieleza kuwa safari ya Mahakama kuelekea Mahakama Dijitali (Smart
Court) imejengwa juu ya misingi ya kimkakati inayojumuisha Mpango Mkakati wa
Mahakama, Sera ya Taifa ya TEHAMA, Mkakati wa Serikali Mtandao, pamoja na Mfumo
wa Kimkakati wa Uchumi wa Kidijitali na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akisisitiza mwelekeo huo
wa kitaifa, alisema: “uboreshaji wote unaofanyika mahakamani katika eneo la
kidijitali tunazingatia siyo tu mipango ya Mahakama, bali pia mipango ya nchi,
tukianzia na Mfumo wa Taifa wa Uchumi wa Kidijitali na Dira ya Maendeleo ya
Taifa 2050. Hii yote tunaitumia kama dira ya kutuongoza katika kufikia maono
mapana ya nchi yetu.”
Alifafanua kuwa mageuzi
hayo yanalenga kuboresha usimamizi wa mashauri, kupunguza mrundikano wa mashauri,
kuongeza uwazi na uwajibikaji, pamoja na kuwezesha maamuzi yanayotegemea
takwimu sahihi.
Aidha, alieleza kuwa
Mahakama imeendelea kuimarisha matumizi ya mifumo ya kielektroniki ikiwemo
mfumo wa usimamizi wa mashauri (e-Case Management System), huduma za Mahakama
Mtandao, pamoja na matumizi ya Akili Unde (Artificial Intelligence – AI) katika
kunakili na kutafsiri mwenendo wa mashauri kwa Kiswahili na Kiingereza,
uchambuzi wa takwimu za mashauri na utafiti wa kisheria.
Kuhusu maadili na usalama
wa taarifa, Bw. Kalege alisisitiza kuwa Mahakama inazingatia kikamilifu matakwa
ya Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi ya mwaka 2022, pamoja na kuimarisha
mifumo ya usalama wa mtandao ili kulinda kumbukumbu na ushahidi wa kimahakama.
Kwa upande wake,
Mwenyekiti wa kikao hicho, Mhe. Dkt. Siyani alieleza umuhimu wa Viongozi wa
Mahakama katika ngazi za kanda kuhakikisha mifumo hiyo inatumika ipasavyo ili
kuleta matokeo chanya katika utoaji wa haki.
Naye Jaji Mkuu
alisisitiza dhamira ya Mahakama kuendelea kuwa Taasisi inayoendana na
mabadiliko ya teknolojia duniani, akieleza kuwa katika zama hizi, utoaji wa
haki unahitaji kuungwa mkono na mifumo imara ya kidijitali ili kuongeza ufanisi
na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mhimili wa Mahakama.





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni