Alhamisi, 26 Februari 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAFANYA MAAJABU MWAKA 2025

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imetekeleza kwa mafanikio makubwa jukumu lake la utoaji haki nchini kwa mwaka 2025. Kiwango cha uondoshaji wa mashauri kimeongezeka kutoka asilimia 83 hadi 88 na kiwango cha umalizaji kikiongezeka kutoka asilimia 101 hadi 105.

Hayo yamebainishwa jana tarehe 25 Februari, 2026 na Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Desdery Kamugisha, wakati anawasilisha taarifa ya Utendaji wa Mahakama kwa Mwaka 2025 kwenye Kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kinachofanyika jijini Dodoma.

Mhe. Kamugisha aliwaeleza Majaji hao kuwa mashauri yaliyofunguliwa kwa mwaka 2025 yalikuwa 243,848, sawa na ongezeko la asilimia 0.6 ya mashauri ya mwaka 2024. Mashauri hayo yanajumuisha 105,480 ya madai na 138,368 ya jinai.

Alibainisha kuwa, mashauri yaliyofunguliwa katika Mahakama ya Rufani yalikuwa 3,214, Mahakama Kuu yalikuwa 21,518, Mahakama za Hakimu Mkazi 6,033, Mahakama za Wilaya 35,144, Mahakama za Watoto 1,225, na Mahakama za Mwanzo 176,687, hivyo kufanya jumla ya 243,848.

‘Mashauri yaliyoamuliwa na Mahakama ya Rufani kwa mwaka 2025 yalikuwa 4,405, Mahakama Kuu zilikuwa 22,164, Mahakama za Hakimu Mkazi 5,967, Mahakama za Wilaya zilikuwa 40,367, Mahakama za Watoto 1,372 na Mahakama za Mwanzo 180,518, hivyo kufanya jumla ya 254,793,’ alisema.

Kwa upande wa mashauri yanayoendelea, Mhe. Kamugisha alieleza kuwa Mahakama ya Rufani ni 5,039, Mahakama Kuu 10,381, Mahakama za Hakimu Mkazi 2,303, Mahakama za Wilaya 8,214, Mahakama za Watoto 202 na Mahakama za Mwanzo 7,240, hivyo kufanya jumla ya 33,379.

Aidha, alibainisha kuwa kiwango cha jumla cha umalizaji wa mashauri kwa 2025 kilikuwa asilimia 105, huku Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, ikiongoza kwa asilimia 141, wakifuatiwa na Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara kwa asilimia 111.

Kwa upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi, Mhe. Kamugisha alieleza kuwa Iringa iliongoza kwa asilimia176, wakifuatiwa na Mtwara kwa asilimia 168, huku upande wa Mahakama za Wilaya, Newala ilikuwa ya kwanza baada ya kuzoa asilimia 156, wakifuatiwa na Geita iliyopata asilimia 142.

'Kiwango cha jumla cha uondoaji wa mashauri kwa mwaka huo kilikuwa asilimia 88.4, huku Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke kikiongoza kwa asilimia 94, wakifuatiwa na Geita iliyopata asilimia 90,' alisema.

Aliongeza kuwa upande wa Mahakama za Hakimu Mkazi, walioongoza ni Simiyu kwa asilimia 97, wakifuatiwa na Mahakama ya Watoto Temeke kwa asilimia 92, huku upande wa Mahakama za Wilaya, Kilolo iliongoza kwa asilimia 99, wakifuatiwa kwa karibu na Newala wenye asilimia 98.

Alibainisha pia mafanikio yaliyopatikana kwa mwaka 2025 kuwa malengo yote ya Mpango Mkakati wa Mahakama na mradi wa kupeleka huduma karibu na mwananchi yalifikiwa kikamilifu.

Mhe. Kamugisha aliongeza kuwa, kumekuwa na ongezeko la kiwango cha umalizaji mashauri kwa asilimia nne kutoka asilimia 101 kwa mwaka 2024 hadi asilimia 105 kwa mwaka 2025.

Kadhalika, alisema, kumekuwa na ongezeko la kiwango cha uondoshaji wa mashauri kwa asilimia tano kutoka asilimia 83 kwa mwaka 2024 hadi asilimia 88 kwa mwaka 2025.

Mhe. Kamugisha alibainisha pia kuwa muda wa wastani wa kuamua mashauri ulipungua kwa siku 12 kutoka wastani wa siku 78 kwa mwaka 2024 hadi siku 66 kwa mwaka 2025 na wastani wa mzigo wa kazi ulipungua kwa asilimia 2.6 kutoka 228 kwa mwaka 2024 hadi 222 kwa mwaka 2025.

‘Matokeo haya chanya yanaonesha utayari wa Mahakama ya Tanzania kukidhi mahitaji yanayokuwa ya haki kwa kuongeza nguvu kazi na kutekeleza mikakati madhubuti ya usimamizi wa mashauri, ikijumuisha mapitio ya kimkakati ya kanuni za taratibu na matumizi makubwa ya teknolojia,’ alisema.

Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Desdery Kamugisha [juu na chini], akiwasilisha taarifa ya Utendaji wa Mahakama kwa Mwaka 2025 kwenye Kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu kinachofanyika jijini Dodoma.


Viongozi na Wakurugenzi wa Mahakama ya Tanzania [juu na chini] wakifuatilia mambo mbalimbali yanayojiri kwenye kikao hicho.


Sehemu nyingine ya Viongozi wa Mahakama [juu na chini] ikiwa kwenye kikao hicho. 



Meza Kuu inayoogozwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju ikiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania [juu na chini]. 




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni