Alhamisi, 19 Februari 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAJADILI BAJETI YA MWAKA 2026/2027

  • Mtendaji Mkuu asema bajeti iakisi dira, kuimarisha msingi wa utoaji haki
  • Asisitiza nidhamu ya matumizi, ulinzi wa Mahakama za Mwanzo

Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, amesema maandalizi ya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27 yanapaswa kwenda sambamba na mipango ya kimkakati ya Mahakama na kulenga kuimarisha utoaji wa haki kwa ufanisi zaidi.

Prof. Ole Gabriel alisema hayo wakati anafungua kikao cha mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 na uchambuzi wa maoteo ya bajeti ya 2026/27 kilichofanyika tarehe 16 Februari 2026 katika Ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Alikumbusha kuwa Julai Mosi 2025, wakati utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 ulipoanza, alitoa waraka ulioelekeza masuala ya msingi ya kuzingatia, ikiwemo kudhibiti ulimbikizaji wa madeni, kuzingatia Sheria ya Bajeti Na. 11 ya Mwaka 2015 na kutohamisha fedha kutoka vifungu vya Mahakama za Mwanzo na Wilaya kwenda Mahakama za juu. Alisema maelekezo hayo yalilenga kuimarisha nidhamu ya matumizi na kuhakikisha rasilimali zinatumika kwa mujibu wa sheria.

“Kuna wakati unaweza kutamani kufanya malipo fulani, lakini kama ni nje ya utaratibu na nje ya sheria huwezi kufanya, kwa sababu itatuletea hoja za ukaguzi. Majukumu yetu tunapaswa kuyafanya kwa mujibu wa sheria na si vinginevyo,” alisema, akitoa shukrani kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Fedha na Uhasibu kwa mchango wao mkubwa katika kuhakikisha Mahakama inaendelea kuwa kinara wa Taasisi za umma zenye hati safi ya hesabu.

Alisema mafanikio hayo ni matokeo ya mipango madhubuti na usimamizi thabiti wa fedha, akisisitiza kuwa rasilimali fedha huwa hazitoshi, hivyo upangaji sahihi ni muhimu ili kufikia matarajio na Dira ya Mahakama. Alieleza kuwa mapitio ya nusu mwaka yanatoa fursa ya kujitathmini kama utekelezaji unaendana na mipango na kama Taasisi iko katika mwelekeo sahihi.

Akigusia suala la Mahakama za Mwanzo, Prof. Ole Gabriel alisema kuwa zaidi ya asilimia 70 ya mashauri huanzia katika ngazi hiyo, hivyo ni lazima zilindwe na kuimarishwa. Alibainisha kuwa katika bajeti ya sasa, Mahakama za Mwanzo zimeongezewa fedha kwa asilimia 100 kwa makusudi maalum, na akaelekeza fedha hizo ziende moja kwa moja katika ngazi hiyo.

“Haikuwa kwa bahati mbaya. Tulimaanisha kulinda Mahakama za Mwanzo kwa sababu ndizo msingi wa utoaji haki kwa wananchi wengi,” alisema.

Aliongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2026/27, Mahakama inapanga kuongeza uwekezaji katika ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama za Mwanzo ili kuboresha mazingira ya utoaji haki na kuongeza imani ya wananchi.

Kuhusu rasilimali watu, alisema Mahakama imeendelea kuiomba Serikali kuongeza watumishi kwa kuwa bila rasilimali watu ya kutosha, utoaji haki unaweza kukwama. Alieleza kuwa tayari kibali cha ajira 642 kimepatikana na mchakato wake umekamilika kupitia Tume ya Utumishi wa Mahakama, akiwashukuru watendaji wote waliohusika katika zoezi hilo.

Aidha, aliwahimiza washiriki kutoa ushiriki wa dhati katika maandalizi ya Mpango Mkakati wa Tatu wa Mahakama, akibainisha kuwa mafanikio ya mpango huo yatategemea tathmini ya mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mipango iliyopita na ushiriki wa pamoja katika kuweka mikakati mipya inayopimika.

Alieleza pia umuhimu wa kuunganisha udhibiti wa vihatarishi katika maandalizi na utekelezaji wa bajeti ili kuhakikisha mipango inayowekwa inatekelezeka bila kuathiri malengo makuu ya Taasisi.

Prof. Ole Gabriel aliwataka wasimamizi wa bajeti katika kanda na divisheni kuandaa bajeti zinazoakisi uhalisia wa mahitaji na kuongeza thamani katika utoaji wa haki.

“Jiulizeni kila wakati: Shughuli hii ninayoipangia fedha inatusaidiaje kufikia malengo yetu makuu. Tuwekeze kwenye maeneo yenye matokeo makubwa na yanayoakisi uhalisia,” alisisitiza.

Alisema maandalizi ya bajeti ni mchakato wa kimkakati unaobeba mustakabali wa Mahakama na kwamba uwajibikaji, ushirikiano na nidhamu ya matumizi ni nguzo muhimu za kuendelea kuimarisha Taasisi hiyo na kulinda imani ya wananchi.

Kwa upande wake, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, alisema bajeti ni nyenzo ya kimkakati inayopaswa kuakisi dira na dhamira ya Taasisi katika utoaji wa haki.

Alisisitiza kuwa maandalizi ya bajeti ya 2026/27 yanapaswa kuendana na maandalizi ya Mpango Mkakati wa Tatu wa Mahakama ili kuhakikisha mipango inayowekwa inatekelezeka na inapimika.

“Haki inapaswa kutolewa kwa wakati na kwa usawa. Hilo linahitaji mipango madhubuti na usimamizi makini wa rasilimali,” alisema.

Mhe. Nkya pia alisisitiza umuhimu wa kuendelea kupunguza mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama, pamoja na kuimarisha matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHAMA] katika usimamizi wa mashauri ili kuongeza uwazi na ufanisi.

Kikao hicho kimeweka msingi wa mchakato wa upangaji wa rasilimali kwa mwaka wa fedha 2026/27, kikionesha dhamira ya uongozi wa Mahakama ya Tanzania ya kuendelea kuimarisha utendaji, uwajibikaji na utoaji wa haki kwa manufaa ya wananchi na maendeleo ya Taifa.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akizungumza wakati anafungua kikao cha mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya 2025/26 na uchambuzi wa maoteo ya bajeti ya 2026/27 kilichofanyika Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho.

Sehemu ya Watendaji na Naibu Wasajili kutoka Kanda na Divisheni [juu na picha mbili chini] wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa kikao hicho.



Meza Kuu ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa kikao hicho [juu na chini].



 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni