Na DOTTO MKAJA-Mahakama, Geita
Matumizi ya Teknolojia ya
Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yameiwezesha Mahakama Kuu Kanda ya Geita kuondoa
mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama kwa mwaka 2025.
Hayo yamebainishwa jana Februari 2, 2026 na Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala ya Geita, Mhe. Kevin Mhina,
wakati akitoa hotuba yake katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini
yaliyofanyika katika Uwanja wa Kituo Jumuishi Geita (Jengo Jipya).
Mhe. Mhina alisema
Mahakama ni chombo muhimu katika kuchochea ukuaji wa uchumi na kulinda amani ya
wananchi, akibainisha kuwa bila uwepo wa Mahakama, vyombo vya ulinzi na
usalama, Magereza na Serikali, hata siku moja haviwezi
kupita bila kutokea uvunjifu mkubwa wa amani.
Akizungumza kuhusu
utendaji wa Mahakama Kanda ya Geita, alisema kuwa kwa mwaka 2025 Mahakama zote
zilifanikiwa kumaliza mashauri kwa wakati, huku wastani wa umalizaji wa
mashauri katika Mahakama za Wilaya tano ukiwa siku 35.
Aliongeza kuwa Mahakama
ya Hakimu Mkazi Geita ilikuwa na wastani wa siku 60, Mahakama Kuu siku 46 na
Mahakama za Mwanzo siku 15. Alisema kuwa wastani wa muda wa usikilizaji mashauri kwa mwaka 2025 umepanda
kulinganisha na mwaka 2024.
Akifafanua mafanikio
hayo, alisema yameleta ongezeko la ufanisi katika usikilizwaji wa mashauri,
kupungua kwa muda wa mashauri kusikilizwa na kuamuliwa, pamoja na kuondolewa
kabisa kwa mlundikano wa mashauri
katika ngazi zote za Mahakama Kanda ya Geita.
Aidha, alisema Mahakama
ilisikiliza na kumaliza mashauri yote ya kimkakati yaliyokuwa yameshikilia
uchumi, hali iliyosababisha
fedha zilizokuwa zimezuiwa kurejeshwa katika mzunguko wa uchumi na kuhamasisha
uwekezaji.
Mhe. Mhina alisema
mafanikio hayo yametokana na matumizi ya TEHAMA, akieleza kuwa teknolojia hiyo
imeongeza uwazi kwa wadau wa haki na kuimarisha ushirikiano kati ya Taasisi mbalimbali kupitia mifumo
inayosomana, ikiwemo NIDA, RITA, Magereza na taasisi nyingine.
Aliwasihi
wadau wa sheria kuendelea kufanya kazi kwa kuzingatia uadilifu, weledi na
ushirikiano.
Kwa upande wake, Mgeni
Mwalikwa katika maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martin Shigela,
aliipongeza Mahakama Kuu Kanda ya Geita kwa kumaliza mashauri kwa wakati na kwa
haki, akisema hali hiyo imepunguza kwa kiasi kikubwa malalamiko kutoka kwa
wananchi.
“Sipokei malalamiko kutoka mahakamani, jambo linaloonesha kuwa haki inatendeka kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji,” alisema Mhe. Shigela.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina,
akitoa
hutuba Siku ya Sheria
katika uwanja wa Mahakama Kuu Geita (Jengo Jipya).
Mchungaji kutoka Kanisa la KKKT akitoa maombi ya kufungua Maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Uwanja wa Kituo Jumuishi Geita (IJC - Geita).
Meza kuu katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria iliyofanyika katika kituo Jumuishi Geita (IJC – Geita).
Mahakimu wakikiwa katika picha ya pamoja Siku ya Sheria nchini katika uwanja wa Kituo Jumuishi Geita(IJC - Geita).
Maofisa kutoka ofisi ya Mwendasha Mashitaka wakiwa katika picha ya pamoja.
Mawakili wa Kujitegemea wakiwa katika picha ya pamoja na meza kuu kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Kevin Mhina, akikagua gwalide Siku ya Sheria katika uwanja wa kituo Jumuishi Geita.








Hakuna maoni:
Chapisha Maoni