Na OBADIA KAWONGA-Mahakama, Mtwara
Utawala bora na unaozingatia
sheria ni msingi wa haki wa kufikia ustawi wa maendeleo ya Taifa, Jaji Mfawidhi
wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, amesema.
Akizungumza kwenye
Maadhimsho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika kikanda tarehe 2 Februari, 2026 katika
Viwanja vya Mahakama Kuu Mtwara, Mhe. Kakolaki alisema kuwa Mahakama kwa
kushirikiana na Serikali imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha utoaji haki
kwa wakati kwa Taasisi, mashirika na jamii kwa ujumla.
'Utawala bora na wa
sheria unazingatia misingi ya haki na ndio msingi mkuu wa kufikia ustawi wa
maendeleo ya Taifa.' aliongezea Mhe. Edwin Kakolaki.
Kwa upande wake, Mkuu wa
Mkoa wa Mtwara, Kanali Patrick Sawala, alihimiza utoaji haki kwa wananchi
mapema ipasavyo ili kudumisha amani na utulivu katika Mkoa na Taifa kwa ujumla.
'Nchi yenye amani na
utulivu inakaribisha wawekezaji kwa kuwa hawana mashaka ya kupoteza mali zao.
Wito wangu tuendelee kuitunza amani yetu,' alisema.
Aidha, Mhe. Sawala alitoa
rai kwa wadau wote wa haki jinai na madai kutekeleza majukumu yao kwa weledi na
uadilifu ili kuisaidia Mahakama kustawisha maendeleo ya Taifa kupitia utoaji
haki bila ucheleweshaji.
Naye Wakili wa Serikali
kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mkoa wa Mtwara, Bi. Nunu Mangu,
alibainisha kuwa Mahakama inalinda amani katika jamii na kuzuia wananchi
kuangukia kwenye kutafuta haki kwa njia zisizo rasmi.
'Nchi imeshuhudia
mabadiliko makubwa kwenye mfumo wa utoaji haki ikiwemo ongezeko la Majaji na
Mahakimu, matumizi ya mifumo ya kisasa pamoja na uboreshaji wa mazingira ya
kazi,' Bi. Mangu alisema.
Maadhimisho hayo
yalihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa
Mtwara, wadau wa sekta ya Sheria: Wakili wa Serikali wa Kujitegemea, Mahakimu
kutoka Wilaya ya Mkoa wa Mtwara, Viongozi wa Dini, Wanafunzi wa Vyuo mbalimbali
pamoja na Wananchi kwa ujumla.
Kabla ya kuhitimisha Maadhimisho
hayo kulikuwepo na gwaride maalum lilioandaliwa na Jeshi la Polisi wa Mkoa wa
Mtwara ambalo lilikagua na Jaji Mfawidhi kuashiria mwanzo wa shughuli za kimahakama
kwa mwaka 2026.
Sambamba na maadhimisho
hayo, kulikuwepo na burudani mbalimbali zilizotolewa na wachezaji wa ngoma za
asili pamoja na Kwaya ya Mtakatifu Mikaeli Malaika Mkuu, ambao waliweza
kufurahisha na kuburudisha nyoyo za waliohudhuria kwa uchezaji mzuri na ujumbe
ulioakisi Kauli mbiu ya Maadhimisho hayo.
Baada ya Maadhimisho hayo,
kulifanyika bonanza katika Viwanja vya Nangwanda lililoongozwa na Jaji Mfawidhi
ambaye alishiriki kikamilifu katika mazoezi na michezo mbalimbali pamoja na
watumishi wa Mahakama.
Akizungumza wakati wa
bonanza hilo, Mhe. Kakolaki alisisitiza umuhimu wa michezo na mazoezi kwa
watumishi wa Mahakama, akisisitiza kuwa shughuli hizo zinaleta afya imara na
kuwawezesha watumishi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.
'Mtumishi mwenye afya
njema ni rasilimali muhimu kwa Taifa. Tunapofanya mazoezi tunajenga miili yetu
na akili zetu, na hivyo tunakuwa na uwezo mkubwa wa kutoa huduma bora kwa
wananchi,' alisema Mhe. Kakolaki.
Bonanza hiyo iliyojaa shangwe na furaha ilihusisha michezo mbalimbali ikiwemo mbio, kuvuta kamba, mpira wa miguu pamoja na wa kikapu. Watumishi Pamoja na wadau mbalimbali walishiriki kwa hamasa kubwa huku wakiimarisha udugu na ushirikiano miongoni mwao.
Wadau pamoja na wananchi katika maandamano kuelekea viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara,
Mhe. Seraphine Nsana, akitoa utambulisho wa Viongozi pamoja na kukaribisha wageni.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara,
Mhe. Edwin Kakolaki akihutubia katika maadhimisho ya Siku ya Sheria mkoani
Mtwara.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara,Kanali Patrick Sawala, akitoa salamu katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara.
Wachezaji wa ngoma za asili wakitoa burudani kwa wageni waalikwa wa hafla hiyo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda
ya Mtwara, Mhe. Saidi Ding’ohi (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya
Mtwara, Mhe. Martha Mpaze (kulia), Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Partick
Sawala (w apili kushoto) pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mhe, Abdallah
Mwaipaya (kushoto) katika picha ya pamoja na baadhi ya Mahakimu.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (wa tatu kushoto) katika uzinduzi wa
bonanza lililoandaliwa baada ya hafla ya maadhimisho ya Siku ya Sheria.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama Dodoma

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni