● Awakumbusha maneno ya Hayati Benjamin William Mkapa kuhusu bidii, maarifa na kufanya kazi kwa matokeo
Na. Halima Mnete – Mahakama, Dodoma
Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher
Mohamed Siyani, amewataka Mahakimu kote nchini kuzingatia misingi ya uadilifu,
ueledi na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao, akisisitiza kuwa bila
kuzingatia nguzo hizo, haki haiwezi kutendeka kwa ufanisi.
Akizungumza mapema leo tarehe 4 Machi, 2026 katika hafla ya
kuapishwa kwa Mahakimu Wakazi wawili (2) iliyofanyika Makao Makuu ya Mahakama
jijini Dodoma, ambapo kiapo hicho kilisimamiwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe.
George Masaju, Mhe. Dkt. Siyani awakumbusha maneno ya Hayati Benjamin William
Mkapa kuhusu bidii, maarifa na kufanya kazi kwa matokeo.
Akizungumza mara baada ya kuapishwa kwa mahakimu hao, Mhe.
Dkt. Siyani alisema kazi ya uhakimu si ya mazoea bali ni dhamana kubwa kwa
umma, inayohitaji mtu mwenye maadili thabiti na uwezo wa kitaaluma.
“Sasa mambo haya yanabeba msingi kwa kazi mnayoenda
kuifanya. Mtumishi yeyote wa Mahakama au wa Umma, hususani Hakimu au Jaji,
anapaswa kuyachukua na kuyazingatia mambo haya matatu kama sehemu ya maisha
yake. Kazi ya uhakimu bila uadilifu hautofika popote, bila ueledi na kuwajibika
hamtafika popote,” alisema Mhe. Dkt. Siyani.
Aliongeza kuwa, Mahakimu hao wameomba wenyewe nafasi hiyo na
kwa mapenzi ya Mungu wamefanikiwa kuipata, hivyo wanapaswa kuitumikia kwa moyo
wa kujituma na kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao.
Katika kuimarisha msisitizo wake, Jaji Kiongozi alinukuu
maneno ya Rais wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati
Benjamin William Mkapa, aliyewahi kusema kuwa njia ya maendeleo imejaa jasho na
vumbi, na kusisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii, maarifa, ubunifu na
kujituma.
Aidha, Jaji Kiongozi alikumbusha kauli ya hayati Mkapa
kwamba kilicho muhimu si muda anaotumia mfanyakazi kazini, bali ni kiasi cha
kazi anachoweza kuifanya katika muda aliopewa. Alisema kauli hiyo ina umuhimu
mkubwa hata kwa Mahakama ya Tanzania, hasa katika kuhakikisha mashauri
yanamalizika kwa wakati na kwa ubora unaotarajiwa.
“Katika kuwajibika, si tu kufanya kazi kwa bidii, lazima
mfanye kazi kwa ufanisi. Matokeo yanapatikana kwa kufanya kazi kwa weledi na
kwa akili. Unaweza kufanya kazi usiku na mchana lakini usimalize kesi kama
haufanyi kazi kwa mpangilio na kwa ufanisi,” alisisitiza.
Mhe.Dkt. Siyani aliwakaribisha rasmi Mahakimu hao katika
utumishi wa Mahakama ya Tanzania na kuwahakikishia kuwa, licha ya kutopata
fursa ya kukutana nao wakati wa mafunzo yao, watakutana katika utekelezaji wa
majukumu yao ya kila siku wakiwa sehemu ya taasisi inayosimamia haki na ustawi
wa jamii.
Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akitoa nasaha kwa Mahakimu Wakazi Wapya walioapishwa leo tarehe 04 Machi, 2026 jijini Dodoma.
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. George Masaju (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mahakimu Wapya walioapishwa leo tarehe 04 Machi, 2026. Wengine ni Jaji Kiongozi wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa kwanza kushoto) na Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania ambaye pia ni Mkuu wa Cho cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA).




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni