Asema Hayati Dkt. Magufuli alikuwa mnyenyekevu, mwenye huruma na mchapakazi
Apongeza Kanisa kwa kuhimiza usalama wa jamii, maadili ya jamii, amani katika jamii, umoja wa kitaifa na maslahi ya Taifa
Na MARY GWERA, Mahakama-Chato
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Viongozi wengine wa Serikali, Wanafamilia
na Watanzania kwa ujumla leo tarehe 17 Machi, 2026 kwa pamoja wameungana na Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Emmanuel John Nchimbi, kuadhimisha
miaka mitano ya Kumbukizi ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa
Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katika Kumbukizi hiyo, Makamu
wa Rais, Mhe. Dkt. Nchimbi amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan huku Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akiwa Mgeni Maalum.
Ibada Maalum ya Kumbukizi
ya miaka mitano ya Kifo cha Hayati Dkt. Magufuli imefanyika katika Viwanja vya JS
Chato vilivyopo katika Kijiji cha Kilimani mkoani Geita.
Aidha, shughuli za Maadhimisho
hayo zilianza majira ya saa 3:30 Asubuhi kwa Adhimisho la Ibada Takatifu iliyoongozwa
na Maaskofu mbalimbali wakiongozwa na Askofu Severine Niwemugizi wa Jimbo
Katoliki la Rulenge-Ngara.
Mara baada ya ibada
kukamilika, Viongozi mbalimbali walipata wasaa wa kutoa neno miongoni mwao
akiwemo Jaji Mkuu, Mhe. Masaju ambaye ameishukuru familia ya Hayati Magufuli
kwa mwaliko wa kushiriki katika Kumbukizi hiyo.
“Nashukuru Mama Janeth
kwa ukarimu wako na kutualika, hii ni fursa ambayo inatukutanisha, lakini yatosha
tu kusema kwamba nikushukuru Mhashamu Baba
Askofu kwa ibada kubwa hii na muhimu uliyoifanya, ninawashukuru Kanisa kwa
kuendelea kuhimiza usalama wa jamii, maadili ya jamii, amani katika jamii,
umoja wa kitaifa na maslahi ya Taifa,” amesema Jaji Mkuu.
Jaji Mkuu ameeleza kuwa,
alimfahamu Hayati Magufuli wakati akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alipokuja
kusoma Shahada ya Pili wakati yeye (Mhe. Masaju) akiwa anasoma Shahada ya kwanza.
Aidha, Mhe. Masaju
amesema kuwa, baadaye mwaka 2015, Hayati Magufuli alimteua kuwa Mwanasheria
Mkuu wa Serikali mara baada ya kuwa ametumika kama Naibu Mwanasheria Mkuu wa
Serikali na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa uteuzi wa Rais Mstaafu wa Awamu ya
Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.
Jaji Mkuu ameongeza kuwa,
alifanya kazi na Hayati Dkt. Magufuli kwa miaka miwili katika nafasi ya
Mwanasheria Mkuu wa Serikali na baadaye alimteua kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya
Tanzania na hatimaye Rais wa Awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akamteua kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania Juni, 2025.
“Ninawashukuru sana Viongozi
hawa, Rais Kikwete, Rais Magufuli, Rais Samia, Rais Mwinyi ‘Senior’ na Rais
Mkapa wana mchango mkubwa sana katika utumishi wangu,” ameeleza Mhe. Masaju.
Kadhalika, Jaji Mkuu amebainisha kuwa, Hayati Magufuli alikuwa na huruma, mnyenyekevu na mchapakazi.
“Hayati Magufuli alikuwa mchapakazi na uchapakazi ule ndio maana tunayashuhudia haya aliyoyafanya na ambaye mrithi wake ambaye mimi naamini ilikuwa timu nzuri ameyakamilisha na mengine ameendelea kuyaibua na kuyafanya. Huu ni utaratibu mzuri kwa Taifa letu,” amesisitiza Mhe. Masaju.
Jaji Mkuu alitumia nafasi hiyo pia kuitakia heri familia ya Hayati Magufuli kuendelea kwa kuwaombea kwa Mwenyezi Mungu kuwabariki katika maisha yao, katika utumishi wao na katika shughuli zao.
“Tunajua hili ni pengo,
Mwanadamu yeyote anapofariki anaacha pengo kubwa ambalo halizibiki lakini pia
linaloumiza kwa sababu pia kila mwanadamu ana utambulisho wake, faraja yangu
mimi kwenu ni kwamba Mungu yupo pamoja na ninyi,” amesema Mhe. Masaju huku akimsihi
Mama Janeth Magufuli kuendelea kuwa imara katika kuisimamia familia huku
akimtanguliza Mungu.
Viongozi mbalimbali
waliopata nafasi ya kuzungumza wakiongozwa na Makamu wa Rais wa Tanzania, Mhe.
Dkt. Nchimbi wamemuelezea Hayati Magufuli kwa mema aliyoyafanya enzi za uhai
wake na kutoa rai kwa Watanzania kuyaenzi yote mema aliyoyafanya.
Wakati wa kumbukizi hiyo,
Makamu wa Rais ameendesha Harambee maalum ya kuchangia ujenzi wa Kanisa la Parokia
ya Mlimani-Chato ambayo ilikuwa ndoto ya Hayati Magufuli ambapo imepatikana Ahadi
za jumla ya Shilingi 474,000,000/=.
Shughuli ya Kumbukizi imehudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa Serikali wakiwemo Mawaziri, Viongozi Waastafu, Wanafamilia na Wananchi kwa ujumla.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa neno wakati wa Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo tarehe 17 Machi, 2026 katika Viwanja vya JS Chato vilivyopo katika Kijiji cha Kilimani mkoani Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje wakiwa katika Kumbukizi ya miaka mitano ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.



















Hakuna maoni:
Chapisha Maoni