Na LYDIA CHURI, Tume ya Utumishi wa Mahakama
Jaji Mkuu wa Tanzania na Mwenyekiti wa Tume
ya Utumishi wa Mahakama, Mhe. George Masaju leo tarehe 13 Machi, 2026
amewaapisha wajumbe wanne wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.
Katika hafla iliyofanyika leo kwenye Ofisi za Tume ya
Utumishi wa Mahakama jijini Dodoma, Jaji Mkuu amemuapisha Jaji wa Mahakama ya
Rufani ya Tanzania, Mhe. Gerson Mdemu kuwa Mjumbe wa Tume kufuatia uteuzi uliofanywa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Aidha, Jaji Mkuu pia amemuapisha Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari kuwa Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kufuatia
kuteuliwa kwa mara ya pili na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa
Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na
Madiwani uliofanyika Oktoba 29, 2025.
Jaji Mkuu pia amewaapisha kwa mara ya pili Mawakili
Bahame Tom Nyanduga na Dosca Kemilembe Mutabuzi kuwa Wajumbe wa Tume ya
Utumishi wa Mahakama baada ya kumaliza kipindi chao cha miaka mitatu cha kuwa
Wajumbe wa Tume na kuteuliwa tena na Rais kushika nafasi hiyo kwa mujibu wa Ibara
ya 112 (1) (e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania.
Tume ya Utumishi wa Mahakama inaundwa na wajumbe
wafuatao; Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ambaye ni Mwenyekiti, Mwanasheria
Mkuu wa Serikali, Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Wajumbe wawili wanaoteuliwa na Rais.
Tume ya Utumishi wa Mahakama ni chombo kilichoundwa kwa
mujibu wa Ibara ya 112 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya
mwaka 1977 ikisomwa pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Mahakama Sura ya 237.
Chombo hiki kimeundwa kwa lengo la kusimamia utendaji kazi wa Mahakama ya
Tanzania ikiwa ni pamoja na kusimamia Ajira na Nidhamu za Watumishi wa Mahakama.





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni