Na JAMES BUSANYA & HALIMA MNETE- Mahakama Dodoma.
Msajili
wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert, amesisitiza
umuhimu wa matumizi ya mifumo ya kidijitali katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.
Mhe. Herbert ametoa msisitizo huo leo tarehe 13 Machi,
2026, wakati anafunga mafunzo ya siku tano kati ya Maofisa wa Mahakama ya Tanzania na Mahkama
ya Zanzibar yaliyokuwa
yanafanyika Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Dodoma.
Msajili wa Mahakama ya Rufani ameeleza kuwa teknolojia inaweza kusaidia kuongeza ufanisi wa
kazi pamoja na kupunguza muda wa usikilizaji wa mashauri.
“Ni
muhimu kuendelea kuimarisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika Mahakama
zetu, ikiwemo usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mfumo wa kielektroniki, jambo
ambalo linaweza kusaidia kuondoa mlundikano wa mashauri na kuongeza ufanisi
katika utoaji wa haki,” amesema.
Akizungumzia mafunzo hayo, Mhe. Herbert amewasihi washiriki
kutumia maarifa waliyoyapata katika kuboresha utendaji kazi ndani ya Taasisi
zao na kuimarisha utoaji wa haki kwa wananchi.
Amesema kuwa
mafunzo ya kubadilishana uzoefu ni muhimu katika kujenga uwezo wa watumishi wa Mahakama,
hususan katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiutendaji pamoja na
kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia.
Naye Naibu
Mrajisi wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Faraji Shumari Juma, akizungumuza kwenye hafla hiyo alitoa shukrani kwa Mahakama ya Tanzania kwa kuandaa mafunzo
hayo muhimu, akisema kuwa yamewasaidia washiriki kupata maarifa na uzoefu mpya
wa kiutendaji.
Aidha,
aliomba ushirikiano kati ya Mahakama ya Tanzania na Mahkama ya Zanzibar
uendelee kuimarishwa ili kusaidia Taasisi hizo
kujifunza zaidi kutoka kwa kila upande.
Alieleza
kuwa ushirikiano huo ni muhimu hasa katika kuboresha matumizi ya mifumo ya
kiteknolojia kwenye uendeshaji na usikilizaji wa mashauri kwa
njia ya kidijitali ili kuongeza ufanisi na kuharakisha upatikanaji
wa haki kwa wananchi.
Wakati wa mafunzo
hayo ya siku tano yaliyoanza tangu
tarehe 9 Machi, 2026, washiriki wamepata
fursa ya kubadilishana uzoefu katika maeneo mbalimbali ya utendaji kazi, matumizi
ya mifumo ya kidijitali, maadili ya kazi pamoja na mbinu za kuboresha utoaji wa
huduma za Mahakama.
Washiriki wameeleza
kufurahishwa na elimu waliyoipata na kuahidi kutumia maarifa hayo katika
kuboresha utendaji wa kazi katika Mahakama zao.






Hakuna maoni:
Chapisha Maoni