Ijumaa, 13 Machi 2026

NAIBU MSAJILI WA MAHAKAMA KUU KANDA YA LINDI AFANYA KIKAO NA WATUMISHI

Na. Hilary Lorry  & Winifrida Kisamo– Mahakama, Lindi

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi pamoja na Mahakama ya Wilaya ya Lindi, tarehe 11 Machi 2026 wamefanya kikao kazi na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Lindi, Mhe. Elia Joseph Mrema ambaye amesema Mahakama Kuu Kanda hiyo inayotarajiwa kuanza kutoa huduma za Mahakama Kuu kwa wananchi hivi karibuni kuanzia sasa.

Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuanza kwa shughuli za Mahakama Kuu Kanda ya Lindi.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mtendaji wa Mahakama Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela aliwapongeza watumishi wa Mahakama hizo kwa uwajibikaji wao na uchapakazi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Alieleza kuwa watumishi hao wamekuwa wakitekeleza majukumu yao kwa bidii na kila mmoja anatambua wajibu wake katika kuhakikisha huduma za kimahakama zinatolewa kwa ufanisi.

Aidha, Mtendaji huyo aliwasisitiza watumishi kuendelea kudumisha usafi wa mazingira katika majengo ya Mahakama pamoja na kuyatunza ipasavyo, akibainisha kuwa mazingira safi na yakitunzwa vizuri huchangia kuongeza ufanisi katika utendaji kazi na kutoa taswira nzuri kwa wananchi wanaofika kupata huduma.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter Singano alisisitiza umuhimu wa utunzaji wa vifaa vya Ofisi pamoja na matumizi sahihi ya rasilimali za Ofisi.

Alieleza kuwa, utunzaji mzuri wa vifaa hivyo utasaidia kuvifanya vitumike kwa muda mrefu, hivyo kuvifanya viweze kutumika kwa mahitaji ya sasa na ya baadaye. Pia alibainisha kuwa matumizi sahihi ya rasilimali za Ofisi yatasaidia kupunguza gharama zisizo za lazima katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema aliwashukuru watumishi kwa ushirikiano waliyompatia tangu alipowasili katika Kituo hicho. Vilevile aliahidi kutoa ushirikiano wa karibu katika utekelezaji wa majukumu ya Mahakama.

Mhe. Mrema aliongeza kuwa, kwa mara ya kwanza katika Mkoa wa Lindi tunaenda kuwa na Mahakama Kuu hivyo basi yatupasa kufanya maandalizi muhimu pamoja na kujianda kwa ujio wa Jaji Mfawidhi, “Sisi  tupo kwenye kufanya maandalizi muhimu pamoja na kujiandaa  kwa ujio wa Jaji Mfawidhi ” alisisitiza Mhe. Mrema.

Aidha, aliwapongeza watumishi wa Mahakama Kanda ya Lindi kwa kazi nzuri wanayoifanya, akieleza kuwa tangu alipowasili mkoani humo na kutembelea baadhi ya ofisi, ikiwemo ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Ofisi ya Kamada wa Polisi Mkoa, Takukuru, Ofisi ya Uhamiaji, Ofisi ya Mawakili wa kujitegemea(TLS) na wadau wengine  hakupokea malalamiko yoyote kuhusu utendaji wa watumishi.

Mhe. Mrema alisema hali hiyo inaonesha kiwango kizuri cha uwajibikaji na nidhamu ya kazi miongoni mwa watumishi wa Mahakama katika Kanda hiyo hivyo aliwataka watumishi kuendeleza juhudi hizo na ikiwezekana kufanya vizuri zaidi.

Naibu Msajili pia alisisitiza umuhimu wa kudumisha upendo, kuaminiana na kuheshimiana miongoni mwa watumishi pamoja na viongozi, huku akisisitiza kuwa kufanya kazi kwa ushirikiano na kuheshimu mipaka ya majukumu ya kila mmoja ni msingi muhimu wa mafanikio katika utendaji wa taasisi, “Tufanye kazi kwa ushirikiano huku tukiheshimu mipaka na tuhakikishe Lindi inakuwa ya mfano” Alisisitiza Mhe. Mrema.

Vilevile, aliwataka watumishi kuwa wabunifu na kuchapa kazi kwa bidii na  kwa kuzingatia misingi ya uadilifu, uwajibikaji na weledi katika kutekeleza majukumu yao, hivyo kuimarisha ufanisi wa kazi na utoaji huduma bora kwa wananchi mapema ipasavyo.

Kikao hicho ni sehemu ya maandalizi muhimu kuelekea kuanza rasmi kwa shughuli za Mahakama Kuu Kanda ya Lindi, inayotarajiwa kuanzishwa hivi karibuni, hatua inayotarajiwa kuimarisha upatikanaji wa huduma za utoaji haki kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi na maeneo ya jirani.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema akizungumza na watumishi wa Mahakama Lindi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter Singano (aliyesimama) akitoa neno la utambulisho.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela (aliyesimama) akitoa neno la ukaribisho.

Afisa Hesabu Mkuu Mahakama ya Wilaya ya Lindi Bw. Lucas M. Kadossa akitoa neno la shukurani kwa niaba ya watumishi.

Waandishi Waendesha Ofisi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi wakitekeleza jukumu lao la uchukuaji wa Muhtsari katika kikao hicho.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni