Jumatatu, 30 Machi 2026

KATAVI YAJIONDOA RASMI KUTOKA MAHAKAMA KUU KANDA YA SUMBAWANGA

Na. Ally Ramadhani – Mahakama, Katavi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda tarehe 27 Machi, 2026 alikabidhi rasmi eneo jipya la kiutawala la masjala ndogo ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Katavi kwa Jaji Mfawidhi wa Kanda hiyo Mhe. Godfrey Ntemi Isaya, katika hafla iliyofanyika katika Jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi.

Aidha, Mhe. Manyanda alifanikiwa kutembelea jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Katavi na kufanya ukaguzi wa vifaa vya ofisi kisha kufanya makabidhiano kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya.

Baada ukaguzi huo Mhe. Manyanda alifanya kikao cha kuagana na watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo Katavi na kuwashukuru kwa ushiriakiano alioupata kutoka kwao na kuahidi kuwa ataendelea kutoa ushirikiano wakati wote atakapo hitajika. Vilevile, aliwakumbusha umuhimu wa kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Kabla ya mwaka 2005, wakazi wa Sumbawanga na Katavi walikua wanapata Huduma za Mahakama Kuu kutoka Kanda ya Mbeya ila mwaka 2005 nasi tukapata Huduma za Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga na leo hii mwaka 2026 nina furaha kubwa sana kuwa kwenye historia ya tukio hili la kukabidhi eneo jipya la kiutawala la Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo Katavi,” alisema Mhe. Manyanda.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya, aliwasisitiza watumishi kuhusu suala la nidhamu, kuthaminiana, upendo, ulinzi wa miundombinu, vitendea kazi wa vya Ofisi na utendaji wa kazi mzuri kwa watumishi wote ili kuwezesha kutoa huduma bora ya haki kwa wananchi.

Vilevile, Mhe. Isaya ameupongeza Uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kuendelea kuboresha mazingira ya utoaji haki kwa kusogeza huduma za utoaji haki kwa wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri.

Kufuatia makabidhiano hayo, Mhe. Manyanda aliambatana na Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Pamela S. Mazengo pamoja na Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga Bi. Irene Mlangwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda (Katikati) akimkabidhi Hati ya makabidhiano Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya (kushoto) kuashiria shughuli rasmi za Mahakama Kuu, Kanda ya Katavi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya (wa kwanza kushoto) akionesha hati ya makabidhiano.

Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Thadeo M. Mwenempazi (wa Kwanza Kushoto) akikabidhi zawadi kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Sumbawanga Mhe Fredrick Kapela Manyanda (wa Kwanza Kulia), iliyo andaliwa na Uongoz wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Katavi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga Mhe. Fredrick Kapela Manyanda akionesha tuzo (Troph) aliyozawadia na Uongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ndogo ya Katavi kupitia Mhe Thadeo M.  Mwenempazi Jaji wa Mahakama kuu ya Tanzania kanda ya Sumbawanga.

Naibu Msajili Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Pamela S. Mazengo akilishwa keki na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Katavi Mhe. Godfrey Ntemi Isaya.


Uongozi wa Mahakama Kuu Masjala ndogo Kanda ya Katavi ilipotembelea  jengo jipya la Kituo Jumuishi cha Utoaji haki Kanda Katavi 






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni