Na ABDALLAH SALUM, Mahakama-Njombe
Jaji mfawidhi wa mahakama kuu ya Tanzania Kanda
ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru amekabidhi ofisi ya Mahakama Kuu Kanda mpya ya
Njombe kwa Jaji Victoria Mlonganile Nongwa ambaye ameteuliwa kuwa Jaji Mfawidhi.
Makabidhiano ya Masjala ndogo ya Mahakama Kuu
Njombe ambayo itaanza kutoa huduma zake
rasmi kuanzia tarehe 30 Machi, 2026 yalifanyika Ijumaa tarehe 27 Machi, 2026
mbele ya watumishi wote w Mahakama ya Hakimu
Mkazi Njombe na Wilaya nne (4) ambazo ni Ludewa, Wanging’ombe, Makete pamoja na
Makambako.
Aidha
akiwa katika kikao cha makabidhiano, Mhe. Ndunguru alimpongeza Mhe. Jaji Nongwa kwa kuteuliwa
kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe huku akishukuru kwa
kupunguziwa majukumu ya mashauri ya rufaa ambazo zilikuwa zikitokea Njombe
kwenda Mahakama Kuu Iringa.
Pamoja
na hayo alizungumza na watumishi wote wa Mahakama za Mkoa wa Njombe kupitia
mfumo wa mkutano mtandao (Video Conference) kwa ambao hawakuweza kufika katika
kikao hicho cha makabidhiano hayo.
Kadhalika,
Jaji Ndunguru alitoa pongezi kwa watumishi wote hususani kwa ushirikiano mkubwa
waliompa kwa kipindi chote alichokuwa
akihudumu kwa Mahakama zote za Mkoa wa Njombe na Wilaya zake na kuwaomba
ushirikiano waliompa yeye kwa kipindi chote wampe pia na Jaji Nongwa ambaye
ameteuliwa kuwa Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Njombe.
Kwa
upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria
Mlonganile Nongwa alimpongeza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa
pamoja na kuwashukuru watumishi wote wa Mahakama za Mkoa wa Njombe kwa kumpa
ushirikiano Jaji Ndunguru ambaye amehudumu kwa kipindi chote ambacho amekuwa
akisimamia Mahakama za Mkoa wa Njombe ambaye kwa sasa atahudumu Mahakama Kuu Kanda
ya Iringa pekee.
Aidha, Mhe. Nongwa aliwasisitiza na kuwaomba
watumishi wote wa Mahakama mkoani Njombe kumpa ushirikiano pamoja na kusisitiza
watumishi watumie mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na
kuachana na matumizi ya peni na karatasi katika utendaji kazi pamoja na
kuwahudumia wananchi vizuri hasa makundi maalum mfano walemavu na akina mama
wajawazito.
Tukio
la makabidhiano ya Kituo cha Mahakama Kuu Njombe lilihudhuriwa na Naibu Msajili
wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mhe. Bernazitha Maziku, Naibu Msajili wa Mahakama
Kuu Kanda ya Njombe, Mhe. Joseph Luambano, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa,
Bi. Melea Mkongwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Bw. Richard Mbambe,
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama pamoja na
Afisa Bajeti wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe na Wilaya zake, Bw. Juma Nyenzi.
Aidha,
Viongozi hao walitoa neno la shukrani kwa pamoja wakati wa makabidhiano hayo mbele
ya Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru na Jaji Mfawidhi
Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa.
Awali Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe pamoja na Wilaya zake zote zilikuwa chini ya Mahakama Kuu Kanda ya Iringa. Mahakama inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za uboreshaji huduma ikiwemo ujenzi wa majengo ya Mahakama ili kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Dunstan Ndunguru (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Mahakimu pamoja na watumishi wa kada mbalimbali baada ya kumalizika kikao cha makabidhiano ya Kituo cha Mahakama Kuu Kanda ya Njombe. Wa tatu kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Victoria Nongwa, wa tatu kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa, Mhe. Bernazitha Maziku, wa pili kulia ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa, wa kwanza kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe, Mhe. Liadi Chamshama, wa pili kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Njombe, Mhe. Mhe. Joseph Luambano, wa kwanza kushoto ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Njombe, Bw. Richard Mbambe.







Hakuna maoni:
Chapisha Maoni