Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile amewataka watumishi
wapya wa Mahakama hiyo kuzingatia maadili na umoja katika kutimiza majukumu yao
huku wakitanguliza mbele uwajibikaji wa kiwango cha juu katika utumishi wao.
Mhe. Rwizile ametoa wito huo leo
tarehe 03 Machi, 2026 ofisini kwake katika mazungumzo aliyofanya na watumishi
hao wapya tis awa kada mbalimbali mara baada ya kupokelewa.
“Ninyi ambao mmepata kazi leo mmeona
ilivyo kazi kupata kazi, hivyo itunzeni kazi kwa maadili ya hali ya juu, mkiwa
kielelezo kazini na mtaani ambapo jamii inatarajia kuona mtumishi wa Mahakama
mwenye maadili mazuri na mfano kwa watu wengine,” amesema Mhe. Rwizile.
Jaji Mfawidhi huyo amesisitiza kuwa, mtumishi
yoyote wa Mahakama anayo dhamana katika mnyororo wa utoaji haki, ambalo ni
jukumu zito linalohitaji nidhamu, uaminifu na weledi wa hali ya juu, na kuwa
watumishi wanapaswa kufanya kazi kwa kuzingatia misingi ya sheria, kuepuka
tabia zisizofaa kwa mtumishi wa umma.
Aidha, amewataka pia watumishi hao
kujenga umoja na mshikamano na kuwahimiza kujifunza kwa watumishi watakaowakuta
katika vituo watakavyopangiwa kazi, huku akisisitiza kuwa nguvu ya Mahakama ipo
katika ushirikiano, uwajibikaji na kufanya kazi kwa kuzingatia kanuni na
taratibu zilizowekwa.
Kwa upande wake Mtendaji wa Mahakama
Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay amewahakikishia watumishi hao mazingira
wezeshi ya kazi ikiwemo vifaa na miundombinu itakayowawezesha katika utendaji
kazi wao pahala pa kazi.
Mazungumzo hayo yalihudhuriwa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Yohana Mbelwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay na Afisa Utumishi Mwandamizi wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Bw. Festo Sanga.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni