Jumatatu, 2 Machi 2026

MAJAJI, MAHAKIMU IJC TEMEKE WAJADILI MAKOSA YANAYOJITOKEZA KWENYE UENDESHAJI MASHAURI YA NDOA

Na JENIFER MALISA-Mahakama, IJC Temeke

Majaji na Mahakimu katika Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, hivi karibuni walikutana kufanya mafunzo mafupi kuhusu makosa yanayojitokeza katika uendeshaji wa mashauri ya ndoa (common pitfalls in matrimonial proceedings).

Katika mafunzo hayo yaliyofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Mahakama hiyo, Majaji na Mahakimu pia walishirikishana uzoefu wa elimu kuhusu masuala hayo.

Kaimu Jaji Mfawidhi, Mhe. Sharmillah Sarwatt, alifungua mafunzo hayo ya ndani na kusisitiza; “Umuhimu wa mafunzo hauepukiki na tunapopata wasaa kama huu tunapata muda wa kuongeza ujuzi wetu.”

Pamoja na kujadili masuala ya ndoa na makosa yanayojitokeza katika uendeshaji na uamuzi wa mashauri ya ndoa, mjadala pia ulijikita zaidi katika masuala ya dhana ya ndoa na mgawo wa mali, masuala ya matunzo na malezi ya watoto.

Washiriki wa mafunzo hayo pia walijadili hangamoto au makosa mbalimbali yanayoweza kujitokeza au yaliyowahi kujitokeza wakati wa uendeshaji au uamuzi wa mashauri ya ndoa na kusababisha au kubatilisha mwenendo mzima na hukumu au kuwaathiri wadaawa kwa namna moja ama nyingine.

Washiriki pia walijadili na kuazimia namna bora ya kuepuka makosa hayo ili kuboresha utendaji wa kazi katika utoaji haki.

Watoa mada wakati wa mafunzo hayo walikuwa Hakimu Mkazi Mkuu, Mhe. Magdalena Malaba na Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Mhangwa Yunge.

Baada ya uwasilishaji wa mada hizo, Majaji wa Mahakama Kuu IJC Temeke, Mhe. Asina Omari na Mhe. Sarah Mwaipopo, walitoa uzoefu wao.

Katika mafunzo hayo, washiriki walishauri kuwa ilikuwa ni mjadala wa namna ya kuamua mtoto akae kwa nani katika ya baba na mama, ni vema maslahi ya mtoto yakaangaliwa kwa mapana yake, ikiwemo matakwa ya sheria ya mtoto pamoja na taarifa kutoka kwa Ofisa Ustawi wa Jamii.

Hata hivyo, washiriki walishauri ni vema masharti ya kumuona mtoto yawe wazi na yanayotekelezeka ili haki kwa pande zote zizingatiwe pale mtoto anapokaa chini ya usimamizi wa mzazi mmoja wapo.

Jaji Mwaipopo alifunga mafunzo hayo na kusisitiza kuwa ni vema Majaji na Mahakimu wakaendelea kubadilishana uzoefu ili kuwa na ufanisi na uamuzi bora.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Sharmillah Sarwatt (katikati aliyesimama) akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo. Wengine kutoka kulia ni Majaji wa Mahakama Kuu IJC Temeke, Mhe. Asina Omary na Mhe. Sara Mwipopo (kushoto).

Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Mhangwa Yunge akiwasilisha mada. Picha chini ni washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia yaliyokuwa yanajiri.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni