Jumatatu, 2 Machi 2026

MADEREVA WA MAHAKAMA WANAMCHANGO MUHIMU KWENYE UTOAJI HAKI

Na. LORDGARD KILALA-Mahakama, IJC Temeke

Maderev awa Mahakama kutoka Divisheni za Mahakama Kuu ya Tanzania, hivi karibuni walipatiwa mafunzo maalum kwa lengo la kuboresha utendaji kazi na utoaji huduma zenye tija na ufanisi zaidi.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Bw. Samson Mashalla, alisema kuwa, Mahakama ya Tanzania katika kutekeleza jukumu lake la msingi la utoaji haki kwa wote na kwa wakati, haiwezi kuiacha nyuma kada muhimu ya Madereva.

“Ndio maana mafunzo haya yameandaliwa kwa nia ya kuwajengea uwezo katika kutekeleza majukumu yenu ipasavyo, kwa kuzingatia baadhi yanu mmeajiriwa hivi karibuni,” alisema Bw. Mashalla aliyefunga mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa - IJC Temeke kwa niaba ya Mtendaji wa Mahakama Kuu Divisheni.

Bw. Mashalla aliwasihi washiriki wa mafunzo hayo kuzingatia yote yatakayofundishwa na mwezeshaji na kuhakikisha wanaenda kuyafanyia kazi kwa lengo la kuleta tija kwa Taasisi na Serikali kwa ujumla.

Mwezeshaji kutoka Chuo cha Taifa cha Usafirishaji, Bw. Ally Kilimila aliwapitisha washiriki katika mada nne; Maadili katika utumishi wa Umma, Utunzaji wa Magari ya Serikali, Udereva wa kujihami na Ukagauzi wa Magari.

Akasisitiza kwamba nidhamu kwa Dereva ni taswira katika utendaji wake ambayo inahusisha utii wa dhati wa sheria na kanuni za Utumishi wa Umma kwa kuwa nadhifu, tabia njema, utunzaji wa siri na muda, nidhamu ya dhati badala ya nidhamu ya woga.

Pia aligusia kuhusu udereva wa kujihami kwa kujinyima haki yake kwa muda mfupi ili kuepusha ajali ambayo ingeweza kutokea, udereva wenye mbinu zinazoweza kuzuia ajali ambazo zingeweza kuzuilika, hata zinazosababishwa na watumia barabara wengine. 







Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni