Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju amezitaka Taasisi za Haki
Jinai kudumisha ushirikiano katika kutekeleza mikakati ya Haki Jinai ili
kuendelea kufanikisha upatikanaji wa Haki kwa haraka katika jamii sambamba na
kudumisha utawala wa sheria na ushirikiano wa kikatiba ili kuleta amani, ustawi
na maendeleo katika Taifa.
Mhe.
Masaju ameyasema hayo leo tarehe 02 Machi, 2026 alipokuwa akifungua na
kufunga mkutano wa kwanza kwa Mwaka 2026 wa Wadau wa Haki Jinai, uliofanyika katika ukumbi
wa Mkutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji
Mkuu ameeleza kuwa, ushirikiano uliopo umejengwa katika wajibu wa kila Taasisi
na kwamba wajibu wa Kikatiba na Kisheria wa kila Mdau wa Haki Jinai ndio
unaozalisha ushirikiano huo, huku akirejea Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa uzinduzi wa Bunge la
13 mnamo tarehe 14 Novemba, 2025 ambapo Rais Samia alisema
kwamba, "msingi wa mafanikio yote ya nchi unategemea utawala wa sheria ikiwa ni
pamoja na kushirikiana na Mahakama ya Tanzania ili haki ipatikane kwa wote mapema
ipasavyo."
“Ushirikiano
huu tulionao pia umejengwa katika wajibu wetu, wote hapa wajibu wetu ni wa
kikatiba na kisheria, utekelezaji wa Sheria au Katiba unazalisha ushirikiano,
lakini pia tunashukuru kwamba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk.
Samia Suluhu Hassan ambaye kwa mujibu wa Katiba pia ndiye Mkuu wa Nchi, Kiongozi
wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu amekuwa akisistiza juu ya ushirikiano huu wa
Mahakama na Wadau wake,” amesisitiza Mhe. Masaju.
Kadhalika,
Jaji Mkuu ameendelea kuutambua mchango wa Jukwaa la Haki Jinai katika
kukabiliana na vitendo vya uhalifu kama ambavyo Mhe. Dkt. Samia alivyosisitiza katika hotuba yake ya kufungua Bunge kuhusu umuhimu wa
jukwaa la Haki Jinai ambapo alisema kwamba, Serikali itaendelea kufanya mageuzi na
maboresho katika Taasisi zote zinazoshughulikia masuala ya Haki Jinai ili
ziweze kukabiliana na vitendo vya uhalifu jambo linaloonesha umuhimu wa Taasisi
hizi katika utekelezaji wa Utawala wa Sheria ambao umewekwa kwenye Ibara ya 26
ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Aidha,
Mhe. Masaju amesisitiza kuwa, Mahakama iko tayari kuendelea kushughulikia
changamoto ambazo zimeonekana kukwamisha utekelezaji wa mikakati iliyowekwa,
kwa kuzingatia mikakati iliyowekwa ili kushughulikia changamoto hizo na kila Taaasisi
inahusika kuzirekebisha changamoto hizo mapema ipasavyo.
“Tutaendelea
kuwa tayari kushughulikia zile changamoto ambazo tulikuwa tunaziona
zinatukwamisha lakini kwa kuzingatia ile mikakati ambayo tumeiweka ya
kushughulikia hizo changamoto kwa hiyo hizo changamoto zinazojitokeza kila
Taasisi inayohusika twende tukazirekebishe mapema ipasavyo na matokeo au tija yaanze kuonekana mapema,”ameeleza Jaji Mkuu.
Ameongeza
kuwa, kila mtu katika jamii anao wajibu wa kuifuata na kuitii Katiba na Sheria za
nchi, kwa kufuata utaratibu uliowekwa, kadhalika kuchukua hatua za kisheria
kuhakikisha hifadhi ya Katiba na Sheria za nchi, huku akiwataka Mawakili wa Kujitegemea wanapowakilisha watu fulani, wasichukuliwe kama wahusika wa tuhuma,
bali wapewe ushirikiano ili na wao waweze kutimiza majukumu yao ya kikatiba.
Akirejea
hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa mwaka 2026 tarehe 02 Februari mwaka huu alisisitiza kuhusu wadau kushirikiana na Mahakama
katika suala la utoaji haki, huku akizitaja faida zake kuwa ni, kuongeza kasi
ya utoaji haki, kulinda uhuru na ukuu wa Mahakama na heshima yake, kupunguza
migogoro ya kiutendaji ambayo waathirika ni wananchi, kuimarisha imani ya umma
kwa mfumo wa utoaji haki, kukuza Utawala wa Sheria, kuzuia migogoro ya
kimaslahi.
Faida
nyingine alizozitaja ni pamoja na kurahisisha utekelezaji wa maamuzi ya
Mahakama ambapo lengo kuu ni ustawi wa wananchi kama ambavyo inaelezwa vizuri
katika Ibara ya 8(1)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo
inasema lengo kuu la Serikali ni ustawi wa wananchi, huku ripoti ya Msajili
Mkuu ya utendaji wa shughuli za kazi za Mahakama kwa mwaka 2025 ikithibitisha
faida zilizoletwa na mahusiano na ushirikiano mzuri baina ya Mahakama na Wadau katika kuyafikia mafanikio.
Aidha,
Mhe. Masaju ameongeza kuwa, ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu si jambo
la hisani wala maelewano ya kirafiki bali ni takwa la kikatiba, kisheria na
kisera hivyo wadau wote watenge muda wao kuhudhuria katika vikao, isipokuwa kwa
sababu za msingi za kutohudhuria na ikitokea hivyo watume wawakilishi kwa
sababu katika vikao ndipo changamoto za utekelezaji na mafanikio ya kila
Taasisi yanapoonekana.
Akizungumza
kuhusu maana ya haki, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, Haki ni uamuzi unaofanywa na
Mahakama kwa kuzingatia na kutekeleza masharti ya Katiba na Sheria kwa mujibu
wa ushahidi ulioletwa mahakamani huku akisisitiza Taasisi zinazohusika
kujitahidi ushahidi uwe unaojitosheleza.
“Kwa
maana hiyo, basi tujitahidi kwa Taasisi zinazohusika zinapokusanya ushahidi, ushahidi uwe ule unaotosheleza kufanya kesi iende mahakamani na Mahakama
inapofanya maamuzi kama mtu hakuridhika akate rufaa vinginevyo Mahakama ndio
ina jukumu la kutamka hiyo haki,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Akisisitiza kuhusu ushirikiano, Mhe. Masaju amesema kwamba, majukumu ya utoaji haki
hayaihusu Mahakama peke yake, hivyo kila Taasisi inapaswa kutekeleza wajibu
wake akirejea hotuba ya Rais Samia katika Siku ya Sheria mwaka 2026 ambapo
alisema na kuagiza kutoa haki kwa kuzingatia masharti yaliyoainishwa katika
Ibara ya 107A(2)(a)(e) na 107B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
kuheshimu na kuulinda uhuru wa Mahakama bila kuutumia vibaya, kutotumia uhuru
huo kama kichaka cha kuficha uzembe na vitendo visivyo vya haki.
Pia kutenda kwa uadilifu na kwa uwazi, kuendeleza suala la usimamizi wa dhamana ili
kuhakikisha kuwa, watuhumiwa wenye stahili ya kupata dhamana wanapata dhamana
kwa mujibu wa sheria, pia wadau wote wa Mahakama katika suala la dhamana kuunga
mkono jitihada za Mahakama katika suala la dhamana.
Kadhalika
kuendeleza kuimarisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kwenda sambamba na mabadiliko ya
teknolojia, pia wadau wa haki kuendelea kushirikiana na Serikali na Mahakama
katika utoaji wa msaada wa kisheria kwa wasioweza kumudu gharama, kuimarisha
ushirikiano kwa utoaji huduma za kisheria mapema ipasavyo na kwa ufanisi, pia kuendelea
kushirikiana na Mahakama katika kuimarisha Utawala wa Sheria pamoja na Taasisi za Haki Jinai kutekeleza mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Haki Jinai.
Kadhalika, Jaji
Mkuu amewashauri wadau wengine kurejea mapendekezo mbalimbali ya Mhe. Dkt. Samia kuhusu utoaji haki na kujiridhisha endapo wameshayatekeleza na kuchukua hatua kwa
sababu jukumu hilo ni jukumu mtambuka, jukumu jumuishi, la pamoja ambalo haliwezi
kuwa jukumu la Mahakama peke yake.
Ameongeza
kuwa, kila jamii yoyote lazima iwe na Viongozi kwa ajili ya kusimamia Utawala wa Sheria na mambo mengine, "kwa hiyo ni vyema kuwa tayari na hasa sisi watumishi wa umma
kuwa tunafuatilia kunasemwa nini kwenye sekta yetu lakini na Viongozi Wakuu wa Serikali ngazi ya Taifa wanasema nini."
Amesema
kuwa, masuala ya jinai yanapodhibitiwa kwa ufanisi ipasavyo yanawezesha wananchi
kushiriki shughuli zao za kiuchumi, kisiasa na kijamii ipasavyo na hivyo
kuimarisha uwepo wa ustawi na maendeleo
ya Taifa, jambo linalodhihirisha mchango wa Mahakama katika ustawi na maendeleo
ya Taifa kama ilivyo kaulimbiu ya Mahakama kwa mwaka huu.
Katika
hatua nyingine, Mhe. Masaju ameeleza kuwa, msingi mkuu wa Dira ya Maendeleo 2050
ni Utawala, Amani, Usalama na Utulivu ambapo ndipo umuhimu wa Sekta ya Sheria
unaonekana, Mahakama na Wadau wake wa Haki Jinai, kwa sababu kama huo ndio
msingi mkuu unaowezesha mengine yote kutekelezwa.
Aidha, amefafanua kuwa, katika hotuba ya Rais, Mhe. Dkt. Samia ya Siku ya Sheria mwaka 2026 alieleza kuwa, Mahakama ina mchango mkubwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050 na kuelekeza mambo kadhaa yafanyike ikiwa ni pamoja na kuendelea kulinda haki na misingi ya Katiba, ambapo alihimiza Mahakama isitoke katika misingi yake na jukumu lake, kuhakikisha migogoro ya kiuchumi, kibiashara na kijamii inatatuliwa kwa haraka na kwa haki, kujenga imani ya wananchi na wawekezaji katika mfumo wa kisheria wa nchi, kukuza uwajibikaji na nidhamu katika utumishi wa umma na wa sekta binafsi.
Vilevile, kudumisha amani na mshikamano wa kitaifa ambao ni msingi wa maendeleo endelevu,
kuwezesha mazingira bora ya uwekezaji na ukuaji wa uchumi kwa kuhakikisha Utawala wa Sheria unazingatiwa,
kulinda haki za makundi maalumu wakiwemo Wanawake, Watoto na watu wenye
mahitaji maalumu, kuzuia migogoro inayoweza kuwa chanzo cha mgawanyiko wa
kijamii au kisiasa.
Pia,
kuharakisha utekelezaji wa sera na mipango ya maendeleo kwa kutoa tafsiri ya
kisheria iliyo wazi na thabiti, kujenga na kuimarisha utamaduni wa kuheshimu
sheria, haki na taasisi za umma, kuchangia katika mapambano dhidi ya rushwa na
matumzizi mabaya ya madaraka kwa kutoa haki bila upendeleo pamoja na kuwezesha
wananchi kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya Taifa kwa kuwahakikishia
ulinzi wa haki zao za kisheria.
Mhe.
Masaju amebainisha kuwa, Mahakama inaendelea kusogeza huduma zake karibu zaidi na wananchi, pamoja na kufanya ugatuzi wa Mahakama ya
Rufani, ambapo mwezi Aprili Mahakama zinazoanzishwa katika Kanda za Arusha, Dar es
Salaam, Mbeya, Mwanza na Tabora pamoja na Makao Makuu Dodoma zitaanza kufanya
kazi.
"Sambamba
na hilo, Kanda za Mahakama Kuu nazo zinafunguliwa mapema mwezi huu ambazo ni
Mahakama Kuu Singida, Mahakama Kuu Songwe, Mahakama Kuu Katavi, Mahakama Kuu
Njombe na Mahakama Kuu Lindi, hii ikiwa ni hatua kubwa inayopigwa na Mahakama
katika kutambua umuhimu wa utawala wa sheria katika ustawi na maendeleo ya
taifa letu," ameeleza Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju amehitimisha kwa kushauri na kuhimiza
kuwa, mikutano itapimwa kwa utekelezaji wa majukumu ipasavyo na si kwa idadi na
wingi wa mikakati.
“Niwashauri na kuwahimiza kuwa mikutano yetu hii itapimwa si kwa idadi ya wingi wa mikakati bali kwa ufanisi wa utekelezaji wa majukumu yetu ipasavyo hususan katika jukumu la utoaji haki mapema ipasavyo, kila aliye na wajibu wa kutekeleza atekeleze,” amesisitiza Jaji Mkuu.
Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wadau wa Utekelezaji wa Mkakati wa Haki Jinai kuhusu ushirikiano na mahusiano katika
utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki Mahakamani uliofanyika leo tarehe 02
Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Jaji Mkuu- Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania
jijini Dodoma.
Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika Mkutano wa Wadau wa Utekelezaji wa Mkakati wa Haki Jinai. Aliyeketi kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amiri Mruma.
Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akizungumza jambo na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani wakati wa mawasilisho ya Utekelezaji wa Mkakati wa Haki Jinai kwa Wadau na Taasisi zinazohusika, katika mkutano wa kwanza kwa mwaka 2026 uliofanyika leo tarehe 02 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mkutano wa Jaji Mkuu, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba akifuatilia mawasilisho ya utekelezaji wa mikakati ya Haki Jinai wakati wa mkutano huo uliofanyika leo tarehe 02 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mkutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akifuatilia kwa makini mawasilisho kutoka kwa Wadau wa Mnyororo wa Haki Jinai katika mkutano uliofanyika leo tarehe 02 Machi, 2026 kwenye ukumbi wa Mkutano wa Jaji Mkuu- Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Sehemu
ya Wadau wa mnyororo wa utekelezaji wa Mkakati wa Haki Jinai walioshiriki
katika mkutano huo.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akifuatilia mawasilisho katika mkutano huo.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Arusha)







Hakuna maoni:
Chapisha Maoni