Jumanne, 3 Machi 2026

MAHAKAMA YA TANZANIA YAANZA MWAKA 2026 KWA KUIMARISHA USHIRIKIANO NA WADAU

  • Msajili Mkuu asema ushirikiano, mahusiano imara ni msingi wa utoaji haki

Na Halima Mnete-Mahakama, Dodoma

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, jana tarehe 2 Machi, 2026 amezungumza na Waandishi wa Habari kuhusu mkutano wa kwanza wa mwaka 2026 kati ya Mahakama na Wadau wa haki jinai, uliolenga kuimarisha ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani.

Akizungumza katika mkutano huo katika ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Nkya alisema kuwa kikao hicho ni mwendelezo wa makubaliano yaliyofikiwa tarehe 24 Septemba, 2025. Katika kikao hicho, Mahakama na Wadau walikubaliana kuweka mikakati tisa ya pamoja, ikiwemo kufanya vikao mara nne kwa mwaka ili kuimarisha uratibu na mawasiliano katika mnyororo wa haki jinai.

Alisema kuwa mkutano huo wa kwanza kwa mwaka 2026 umejikita katika tathmini ya utekelezaji wa mikakati iliyowekwa pamoja na kuweka mwelekeo wa pamoja kwa mwaka, kwa lengo la kuhakikisha mashauri yanashughulikiwa kwa ufanisi na kwa wakati.

“Utoaji haki ni jukumu la pamoja, Mahakama haiwezi kufanya kazi peke yake bila ushirikiano madhubuti wa Wadau wote katika sekta ya haki jinai. Mahusiano yetu ya kikazi ndiyo msingi wa kuongeza ufanisi na kuimarisha imani ya wananchi kwa Mhimili wa Mahakama,” alisema.

Akiwasilisha mafanikio yaliyopatikana kupitia ushirikiano huo, Msajili Mkuu alieleza kuwa katika kipindi cha Septemba hadi Desemba 2025, mashauri 30,076 yalifunguliwa huku mashauri 38,639 yakimalizika, sawa na asilimia 128 ya mashauri yaliyofunguliwa katika kipindi hicho.

Kwa mwaka mzima wa 2025, mashauri ya jinai 138,368 yalifunguliwa katika ngazi zote za Mahakama na mashauri 145,467 yalimalizika, sawa na asilimia 105 ya mashauri yaliyofunguliwa. Kutokana na hali hiyo, Mahakama ilifunga mwaka ikiwa na mashauri 14,172 pekee yanayoendelea, ambapo asilimia 75 ya mashauri hayo yana umri usiozidi miezi sita.

Aidha, Mhe. Nkya alieleza kuwa ushirikiano huo umeimarisha matumizi ya mifumo ya kidigitali, hususan mfumo wa JOT-eCMs ambao umeunganishwa na mifumo ya Wadau mbalimbali ili kurahisisha usimamizi na ufuatiliaji wa mashauri. Kupitia mfumo wa Mahakama Mtandao, mashauri 24,662 yalisikilizwa katika kipindi cha Januari hadi Desemba 2025.

Vilevile, aligusia kutungwa kwa Kanuni katika Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya, ambazo zimempa haki mshtakiwa kupewa ushahidi wa upande wa mashtaka mapema, hatua ambayo imeongeza uwazi na kuharakisha usikilizaji wa mashauri.

Akihitimisha, Msajili Mkuu alisisitiza kuwa Mahakama itaendelea kuimarisha mahusiano ya kikazi na Wadau wake kwa mwaka 2026, kwa lengo la kuhakikisha haki inatolewa kwa wakati, kwa uwazi na kwa kuzingatia misingi ya sheria, huku akiipongeza vyombo vya habari kwa mchango wao katika kuhabarisha umma kuhusu masuala ya haki na sheria.


Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo kwenye picha).

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni