Jumanne, 3 Machi 2026

WADAU WAWEKA MKAKATI MPYA KUIMARISHA UTOAJI HAKI 2026

  • Jaji Mkuu asema uwajibikaji, mageuzi ya kiutendaji ili kulinda imani ya wananchi

Na HALIMA MNETE &  JAMES BUSANYA-Mahakama,  Dodoma

Mkutano wa kwanza wa mwaka 2026 kati ya Mahakama ya Tanzania na Wadau wa sekta ya haki jinai umefanyika jana tarehe 2 Machi, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania jijini Dodoma.

Lengo la mkutano huo ni kupitisha tathmini ya utekelezaji wa mikakati iliyokubaliwa hapo awali na kuweka mwelekeo wa pamoja katika kuimarisha ushirikiano na mahusiano katika utekelezaji wa majukumu ya utoaji haki mahakamani.

Mkutano huo uliongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani, huku Mgeni Rasmi akiwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Akifungua mkutano huo, Jaji Mkuu alisisitiza kuwa uimara wa mnyororo wa haki jinai unategemea kwa kiasi kikubwa uwajibikaji wa kila Taasisi katika kutekeleza wajibu wake kwa wakati, kwa kuzingatia Katiba na sheria za nchi.

Alieleza kuwa haki inapocheleweshwa huathiri si wahusika wa shauri pekee, bali pia hupunguza imani ya wananchi kwa mfumo mzima wa utoaji haki.

Katika kikao hicho, Wadau mbalimbali waliwasilisha taarifa za utekelezaji wa majukumu yao pamoja na changamoto wanazokutana nazo katika utekelezaji wa mkakati wa haki jinai.

Bi. Singwa Mokiwa, aliyemwakilisha Kamishna Mkuu wa Uhamiaji, alieleza kuwa Taasisi ya Uhamiaji imeendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria na maadili ya utumishi wa umma.

Alisema Taasisi hiyo inahakikisha watuhumiwa wanafikishwa mahakamani kwa wakati, vielelezo vinawasilishwa ipasavyo na amri za Mahakama zinatekelezwa bila kuchelewa.

Hata hivyo, alibainisha changamoto zikiwemo ucheleweshaji wa usajili wa majalada katika baadhi ya maeneo, upungufu wa wakalimani na ucheleweshaji wa upatikanaji wa mashahidi, hali inayoweza kusababisha watuhumiwa kukaa mahabusu kwa muda mrefu zaidi.

Kwa upande wake, Bi. Alice Mtulo kutoka Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali aliwasilisha tathmini ya mashauri ya kikatiba na haki za binadamu yenye viashiria vya jinai yanayosimamiwa na ofisi hiyo. Alieleza kuwa katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2025, ofisi ilisajili mashauri 1,693 ya madai, ambapo 216 yalikuwa mashauri ya kikatiba na haki za binadamu, yakiwemo mashauri ya uchaguzi.

Bi Alice pia alibainisha kuwa changamoto kubwa ni ucheleweshaji wa upatikanaji wa taarifa kutoka Taasisi mbalimbali za Serikali wakati wa kuandaa majibu ya utetezi, pamoja na ufinyu wa muda wa siku 14 uliowekwa kwa mujibu wa kanuni za mashauri ya kikatiba na haki za binadamu.

Aidha, alieleza changamoto ya matumizi ya hati za dharura katika baadhi ya mashauri bila kuwepo utaratibu madhubuti wa kuthibitisha udharura wake, jambo linaloweza kuathiri maandalizi ya kina ya utetezi wa Serikali.

Ofisi hiyo imeweka mikakati ya kuimarisha mafunzo kwa Mawakili wa Serikali, kuboresha mawasiliano kupitia mfumo wa usimamizi wa mashauri (CMIS) na kuanzisha mifumo ya kupata taarifa za mashauri kwa njia ya simu za kiganjani.

Vilevile, Mkurugenzi Divisheni ya Uaimamizi wa Kesi na Uratibu wa Upelelezi, Bw. Siraji Iboru, alisema kikao hicho kilipitia na kuthibitisha utekelezaji wa mikakati minane iliyokubaliwa katika kikao kilichopita.

Alieleza kuwa ofisi hiyo hufanya vikao vya kila Wiki kwa ajili ya tathmini ya utendaji na utoaji wa maelekezo kwa watumishi wake. Alibainisha kuwa mlundikano wa kesi umepungua na kiwango cha ushindi wa kesi kimeongezeka na kufikia asilimia 84.

Hata hivyo, alieleza kuwa bado kuna changamoto ikiwemo baadhi ya Wilaya kukosa Magereza na uhaba wa Waendesha Mashtaka katika maeneo kadhaa.

Naye Kamishna wa Jeshi la Magereza, Afande Nicodemus Tenga, alieleza   kuwa Jeshi limeendelea kuimarisha uwajibikaji kwa kuingiza maudhui ya uwajibikaji katika mitaala ya mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi kwa Askari na Maofisa wake.

Aidha, vituo 181 vya Magereza tayari vimeunganishwa na Mahakama kwa njia ya mtandao, hatua inayorahisisha ufuatiliaji wa mashauri na upatikanaji wa taarifa kwa wakati.

Jeshi hilo pia linaendelea kusimika mfumo wa taarifa za Wafungwa unaounganishwa na Taasisi mbalimbali, ikiwemo NIDA, NECTA, Mahakama na Jeshi la Polisi. Pamoja na jitihada hizo, changamoto ya ukosefu wa Magereza katika baadhi ya Wilaya imeelezwa kuongeza gharama za usafirishaji wa Wafungwa.

Kwa upande wake, Bw. Joseph Kisusi, ambaye ni Kamishna Msaidizi Kanda ya Kati Dodoma na Mwakilishi wa Kamishna Jenerali, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, alisema ofisi hiyo imeendelea kuwajengea uwezo watumishi wake na kuimarisha maadili katika utekelezaji wa majukumu.

Alieleza kuwa kamati maalum zimeanzishwa kwa ajili ya kufuatilia na kusimamia maadili ya watumishi, huku wakisisitizwa kuheshimu hadhi na mamlaka ya Mahakama wanapotekeleza majukumu yao.

Katika mkutano huo pia, Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bonaventure Mwabukusi, alisema chama hicho kimeendelea kusimamia kwa ukali maadili ya taaluma ya uwakili, hususan kwa Mawakili wanaochukua fedha za wateja bila kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa makubaliano.

Alieleza kuwa TLS imekuwa ikiwalazimisha Mawakili watakaobainika kukiuka maadili kurejesha fedha kwa wateja wao pamoja na kuchukuliwa hatua stahiki za kinidhamu kwa mujibu wa Katiba na kanuni za chama. Alisisitiza kuwa chama hicho hakitavumilia vitendo vinavyodhalilisha taaluma ya uwakili na kuathiri imani ya wananchi kwa mfumo wa haki.

Aidha, alisema TLS inaendelea kutoa elimu ya maadili kwa Mawakili ili kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa kuzingatia Katiba, sheria na kanuni za taaluma, pamoja na kuheshimu ukuu na hadhi ya Mahakama.

Alibainisha kuwa chama hicho kimeimarisha ushirikiano na Wadau wa mnyororo wa haki jinai, kinaendelea kutoa mafunzo ya maadili kwa Mawakili wapya na kusisitiza umuhimu wa msaada wa kisheria kwa wasiojiweza ili kuendeleza dhana ya usawa mbele ya sheria.

Wakili Mwabukusi pia alisema TLS inakaribia kukamilisha matumizi ya mifumo ya kidijitali itakayowezesha mawasiliano na ushirikiano wa karibu zaidi na Wadau wa sekta ya haki jinai.

Hata hivyo, alitaja changamoto zinazoikabili taaluma hiyo kuwa ni pamoja na vitisho dhidi ya Mawakili, masuala ya ulinzi na uhuru wa taaluma ya uwakili. Alisisitiza kuwa Wakili anapomtetea mteja mahakamani haimaanishi anahusika na kosa analodaiwa mteja wake, bali anatekeleza wajibu wake wa kisheria wa kuhakikisha haki inapatikana kwa mujibu wa sheria.

Kwa ujumla, mkutano huo umeonesha dhamira ya pamoja ya kuimarisha uwajibikaji, maadili na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika Taasisi zote za mnyororo wa haki jinai.

Wadau walikubaliana kuwa ushirikiano wa karibu, mawasiliano ya wazi na utekelezaji wa majukumu kwa weledi ndivyo vitakavyoendelea kuimarisha utoaji haki na kulinda imani ya wananchi kwa mfumo wa Mahakama nchini

Mkutano huo umehitimishwa kwa msisitizo kwamba utoaji haki ni dhamana ya pamoja ya Taasisi zote katika mnyororo wa haki jinai, na kwamba uwajibikaji, maadili na ushirikiano wa karibu ndivyo vitakavyoendelea kuimarisha imani ya wananchi kwa mfumo wa Mahakama nchini.

Bi. Singwa Mokiwa, aliyemwakilisha Kamishna Mkuu wa Uhamiaji.

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Bw. Crispin Chalamila.

Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Alice Mtulo.

Kamishna wa Jeshi la Magereza, Afande Nicodemus Tenga.

Kamishna Msaidizi Kanda ya Kati Dodoma na Mwakilishi wa Kamishna Jenerali, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Bw. Joseph Kisusi. 

Mkurugenzi Divisheni ya Usimamizi wa Kesi na Uratibu wa Upelelezi, Bw. Siraji Iboru.


Wadau wakichukua kumbukumbu kwenye mkutano huo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.



 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni