Ijumaa, 6 Machi 2026

HUDUMA ZA MAHAKAMA KUU KATAVI KUANZA WAKATI WOWOTE KUANZIA SASA

Na. Ally Ramadhani - Katavi

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mkoa wa Katavi Mhe. Silivia S. Lushasi tarehe 5 Machi, 2026 amefanya kikao na wadau wa Mahakama cha maandalizi ya uanzishaji wa masjala ndogo ya Mahakama Kuu, Kanda ya Katavi na kuwapongeza wadau kwa ushiriki wao kwa kuhakikisha masjala hiyo inaanza kuwatumikia wananchi.

Akizungumza katika kikao, Mhe. Lushasi amesema, taarifa itatolewa kwa wananchi muda wowote ya kuanza kupata huduma za Mahakama Kuu Mara tu itakapokuwa imetangazwa rasmi kwenye Tangazo la Serikali.

Naibu Msajili huyo amesema, Mahakama Kuu itakapoanza mkoani Katavi, mashauri yote yaliyo sajiliwa Mahakama Kuu Sumbawanga yataendelea huko huko ila yale mapya yatasikiliziwa masjala mpya ya Katavi na kuongeza kuwa, dira ya Mahakama ya Tanzania ni kutoa haki kwa wakati na mapema kadri iwezekanavyo.

Aidha, Mhe. Lushasi aliongeza kuwa, wadau waliopo kwenye mnyororo wa haki Jinai inabidi kuendana na kasi ya Mahakama kidijitali kwa kuboresha na kuimarisha miundombinu.

Mhe. Lushasi ameongeza kuwa, nguzo ya pili ya Mpango Mkakakati wa miaka mitano wa Mahakama ya Tanzania inasisitiza utoaji haki kwa wakati. Mahakama ya Tanzania inatekeleza mpango huo kwa kuboresha mazingira ya utoaji haki na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi kwa kujenga miundombinu bora na wezeshi itakayochangia ufanisi mzuri wa utekelezaji wa nguzo hiyo.

Kwa upande wake, Mwakilishi kutokea TANESCO Mhandisi Victor Ng’wigulu alisema, kwa sasa Taasisi zote za umma ikiwemo Mahakama tumeziweka kwenye kipaumbele cha kwanza katika kuhakikisha zinapata nishati ya umeme.

“Tuliwashauri Mahakama ya Tanzania Mkoa wa Katavi wapate kangavuke (Standby Generator) na nitumie nafasi hii kuwashukuru kwa kupata kangavuke zuri na la kisasa tumeliona lipo, hivyo ikitokea changamoto za umeme wa TANESCO naamini shughuli za kimahakama zitaendelea ila tumejipanga vizuri kama TANESCO Mkoa kuendelea kutoa huduma bora kwa Taasisi zote.

Wadau wa Mahakama waliohuduria kwenye kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Katavi ni pamoja na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Takukuru, Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali Sumbawanga, Ofisi ya Magereza Katavi, Chama cha wanasheria Tanganyika (TLS) Katavi, Baraza la Ardhi na Nyumba, Hifadhi ya Taifa Katavi, Afisa Ustawi wa Jamaii Katavi, Mahakimu Wafawidhi, Tanesco, Tume ya Usuluhishi na Upatanishi (CMA) Katavi, Ofisi ya Mganga Mkuu Katavi, Mwanasheria wa Halmashauri za Mpanda, Mlele na Tanganyika.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania,  Mhe. Silivia S. Lushasi (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama ya Tanzania mkoa wa Katavi mara baada ya kikao cha wadau wa Mahakama.

Wakili wa Serikali Mwandamizi kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Katavi Bi. Flavia F. Shiyo akichangia hoja wakati wa Kikao cha Wadau wa Mahakama Katavi.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania,  Mhe. Silivia S. Lushasi (katikati waliokaa mbele) akiongea na Wadau wa Mahakama ya Tanzania mkoa wa Katavi kwenye kikao cha wadau wa Mahakama.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni