Jumamosi, 11 Aprili 2026

BARAZA LA WAFANYAKAZI MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA KAZI LAFANYIKA MOROGORO

Na LIGHTNESS KABAJU-Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Morogoro

Katika kuimarisha utendaji wa Taasisi na ustawi wa Watumishi wa Mahakama, jana tarehe 10 Aprili, 2026 wajumbe wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi wamefanya kikao cha Baraza la Wafanyakazi mjini Morogoro.

Kikao hicho kimehudhuriwa na baadhi ya Watumishi pamoja na wajumbe wengine, akiwemo Bw. Alquine Masubo kutoka TUGHE Makao Makuu, Bw. Steven Wadi, ambaye ni mjumbe wa TUGHE Baraza Kuu serikalini, Bw. Anthelmus Tarimo, ambaye ni Mwakilishi wa Katibu TUGHE Mkoa na Bi. Christina Matage, ambaye ni Afisa Kazi Mwandamizi Idara ya Kazi kwa Mkoa wa Morogoro.

Baraza hilo limekutana katika kikao chake cha kawaida kwa kila mwaka chini ya uongozi wa Jaji mfawidhi wa Mahakama kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina, kwa lengo la kupitia utekelezaji wa majukumu na kujadili bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027.

Malengo mengine ni kufanya uchaguzi wa Katibu na Katibu Msaidizi wa Baraza la Wafanyakazi, kupokea na kujadili hoja za Watumishi kwa ajili ya kuziwasilisha katika Baraza Kuu la Wafanyakazi la Mahakama ya Tanzania.

Akifungua kikao hicho, Mhe. Mlyambina ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza alisisitiza umuhimu wa wajumbe kushiriki kikamilifu katika mijadala na kutoa michango yenye tija itakayosaidia kuimarisha ufanisi wa Taasisi. Vilevile, alieleza kuwa Baraza la Wafanyakazi ni chombo muhimu kinachowezesha ushirikishwaji wa Watumishi katika maamuzi yanayohusu maendeleo ya Mahakama kwa ujumla.

Katika kikao hicho, Bi. Christina Matage, kwa mujibu wa sheria aliongoza uchaguzi wa kumpata Katibu wa Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ambapo Bi. Stella Omozo, alichaguliwa kuwa Katibu, huku Bw. Godfrey Albetus, akiwa Katibu Msaidizi.

Aidha, Bw. Robert Mchocha alichaguliwa kuwa Mwakilishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi katika Baraza Kuu la Wafanyakazi.

Katika kuwashirikisha wajumbe, Bi. Joyce Mulugu, ambaye ni Mtendaji wa mMhakama Kuu Divisheni ya Kazi aliwapitisha wajumbe katika taarifa ya utendaji kazi, huku Bw. Fredrick Tenga, ambaye ni Afisa Hesabu Mkuu, aliwapitisha wajumbe katika kujadili bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027, wakilenga kuhakikisha kuwa rasilimali zilizopo zinatumika kwa ufanisi na kwa kuzingatia vipaumbele vilivyowekwa.

Aidha, hoja mbalimbali zilizowasilishwa zilijikita katika kuboresha mazingira ya kazi, kuongeza motisha kwa Wafanyakazi, pamoja na kuimarisha huduma zinazotolewa na Mahakama.

Sambamba na hilo, Wajumbe wa Baraza walipata fursa ya kujadili hoja za Wafanyakazi wa mMhakama Kuu Divisheni ya Kazi zinazowakabili katika utekelezaji wa majukumu yao na kupendekeza ziwasilishwe katika Baraza Kuu la Wafanyakazi.

Sambamba na hilo, wajumbe kutoka TUGHE walitoa pongezi zao kwa Jaji Mfawidhi katika kusimamia utoaji elimu kwa watumishi, pamoja na kupokea tuzo ya ubunifu, huku wakipongeza taarifa zilizowasilishwa kwa wajumbe kwani zililenga vipaumbele muhimu katika utekelezaji wa majukumu.


Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) pamoja na wajumbe.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina (katikati) pamoja na wajumbe kutoka TUGHE.

Mwakilishi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi katika Baraza Kuu la Wafanyakazi, Bw. Robert Mchocha.

Mwenyekiti akiwa na Katibu na Katibu Msaidizi waliochagulia (mbele) pamoja na Viongozi wa Baraza la Wafanyakazi waliomaliza muda wao.



Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe, Dkt. Yose Mlyambina (katikati) akiongoza kikao cha Baraza la Wafanyakazi.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni