Na. HABIBA MBARUKU- Mahakama, Dodoma
Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye
pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala
Kuu, amewataka wanachama wa chama hicho
kujenga utamaduni wa kukutana mara kwa mara ili kulinda uhai wa chama hicho.
Mhe.
Dkt. Siyani ameyasema hayo wakati alipofungua mafunzo na michezo kwa Wanachama
wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu, leo tarehe
9 Aprili, 2026 katika ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania
jijini Dodoma.
Mhe.
Dkt. Siyani amesema kuwa, upo umuhimu wa wanachama wa TMJA Tawi la Masjala Kuu
kukutana mara kwa mara, kama ambavyo vyama katika Taasisi nyingine hufanya, hivyo
ni muhimu kuhakikisha kwamba vikao vya Chama vinaandaliwa na wajumbe wanakutana
kama ambavyo Katiba ya Chama inaelekeza huku akiwahimiza wanachama na wajumbe
kuhudhuria vikao vya chama bila visingizio.
“Umuhimu
wa kukutana mara kwa mara, uhai wa vyama hivi kama ilivyo kwa taasisi nyingine
unategemea wajumbe wake kukutana, inategemea uwepo wa vikao, chama au taasisi
yoyote ambayo haikutani uhai wake unakuwa mashakani, kwa hiyo tawi hili kama
matawi mengine yote yanao wajibu wa kikatiba kwa mujibu wa Katiba yetu ya chama
kukutana, ni muhimu kuhakikisha kwamba vikao hivi vinaandaliwa na watu
wanakutana, ujengwe huo utamaduni na tusirudi tena kwenye historia ya kukaa
muda mrefu bila kukutana ili kulinda uhai wa chama” amesema Mhe. Dkt. Siyani.
Aidha,
Mhe. Dkt. Siyani ameongeza kuwa, kama ambavyo kila mmoja hulinda afya yake, ni
muhimu kila mwanachama kuanza kuitazama afya ya akili na kuipa kipaumbele kwa
sababu tatizo la afya ya akili linaweza kuathiri utendaji wa shughuli za kila
mmoja na hasa zile za kiofisi, hivyo ni vyema kuanza kutazama mambo yanayoweza
kupunguza msongo wa mawazo ili kutunza afya ya akili.
Akizungumza
kuhusu umuhimu wa mafunzo yatakayotolewa, Mhe. Dkt. Siyani ameeleza kuwa,
mafunzo hayo yatawasaidia kutambua ni shughuli gani wanaweza kufanya ili
kujiongezea kipato bila kuathiri uwajibikaji wao kama Maofisa Mahakama, kupitia
mada mbalimbali zitakazotolewa ikiwemo masuala ya uwekezaji salama na wenye
tija na kuwataka wajumbe kuchangia kwa uhuru na kuachana na utamaduni wa
kutotoa mawazo au hoja na kuongeza kuwa jamii itapiga hatua katika maendeleo
kama kila mtu atatoa mawazo na kuzungumza katika majadiliano.
Kupitia
mada ya utafiti wa sheria kwa njia ya mtandao itakayofundishwa wakati wa
mafunzo, Mhe. Dkt. Siyani ameeleza kuwa, Maofisa Mahakama hawataweza kutimiza
wajibu wao bila kufanya utafiti na kwamba utafiti utawasaidia kujenga hoja na
kuonesha sababu za kufanya maamuzi fulani, hivyo suala la utafiti lina umuhimu
mkubwa katika kujenga uelewa wa kutosha jambo linatalosaidia wakati wa kutoa
maamuzi yaliyo sahihi na kutenda kwa haki.
Aidha,
Mhe. Dkt. Siyani amewahimiza wajumbe waliohudhuria mafunzo hayo kushiriki
katika michezo itakayofanyika jioni baada ya mafunzo kukamilika ili kuendelea
kulinda afya ya akili na kuimarisha afya ya mwili.
Jaji
Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye
pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala
Kuu, akizungumza wakati alipofungua mafunzo na michezo kwa Wanachama wa TMJA
Tawi la Masjala Kuu, leo tarehe 9 Aprili, 2026 katika ukumbi wa mikutano, Makao
Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Naibu
Msajili Mahakama Kuu na Mkurugenzi wa Menejimenti ya Mashauri ya Mahakama ya Tanzania
Mhe. Desdery Kamugisha ambaye pia ni Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Masjala Kuu
akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu
ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa TMJA Tawi
la Masjala Kuu ili afungua mafunzo na michezo kwa wanachama wa Tawi hilo.
Meza Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na uongozi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu.
Meza
Kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Mustapher
Mohamed Siyani ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania
(TMJA) Tawi la Masjala Kuu (katikati), kulia ni Mkurugenzi wa Menejimenti ya
Mashauri ya Mahakama ya Tanzania na Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Masjala Kuu Mhe.
Desdery Kamugisha na kushoto ni Amidi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Amani
Aboud.
Meza
Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Chama cha Mahakimu na Majaji
Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu.
Meza
Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe Wanawake wa Chama cha Mahakimu na
Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu.
Meza
Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Chama cha Mahakimu na Majaji
Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Kuu.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)








Hakuna maoni:
Chapisha Maoni