Na. HILARI GDIYE NA WINIFRIDA KISAMO – Mahakama, Lindi
Wadau
wa Sekta ya Haki mkoani Lindi wamehimizwa kuongeza na kuimarisha ushirikiano katika
uendeshaji wa mashauri ili kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati mapema
ipasavyo na kwa ufanisi.
Akizungumza
katika kikao cha wadau kilichofanyika hivi karibuni, Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Sylester Kainda alisisitiza
umuhimu wa ushirikiano wa karibu miongoni mwa wadau wote wa Sekta ya haki ili
kutotoa nafasi ya kuchelewesha mashauri yanapofunguliwa mahakamani.
Mhe.
Kainda amesema kuwa, mafanikio ya Mahakama yanategemea mchango wa pamoja wa
kila mdau. Alibainisha kuwa kikao hicho kililenga kuweka mkakati madhubuti wa
namna bora ya kuendesha shughuli za Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Lindi kwa
ufanisi, uwazi na kasi na kuhakikisha huduma za haki zinatolewa kwa wakati mapema
ipasavyo na kwa viwango vinavyotarajiwa.
Aidha,
Jaji Mfawidhi alieleza kuwa, Mahakama haiwezi kusimama peke yake bila
ushirikiano wa wadau wake, akiwataka wadau wote kutambua nafasi zao katika
kuhakikisha mchakato wa haki unakuwa thabiti na wenye matokeo chanya kwa jamii.
Vilevile,
Mhe. Kainda alisisitiza umuhimu wa kumaliza mashauri kwa wakati ili kuwawezesha
wananchi kuendelea na shughuli zao za kiuchumi bila ucheleweshaji usio wa lazima,
kwa mujibu wa takwimu Mkoa wa Lindi una mashauri machache, hali inayotoa fursa
kwa Mahakama kuhakikisha kesi zote zinakamilika kabla ya mwezi Disemba, 2026.
“Kwa
idadi ndogo ya mashauri yaliyopo ni matarajio yetu kwamba, Mahakama zetu zifike
hatua ya kumaliza kesi zote kwa wakati na hata kuwa, katika nafasi ya kusubiri
mashauri mapya,” alisema Jaji Kainda.
Jaji
Mfawidhi huyo, alifafanua kuwa, mfumo wa kimahakama hupima ufanisi kwa
kuzingatia muda unaotumika kusikiliza na kumaliza mashauri, hivyo Mahakama
zinapaswa kuepuka uwepo wa kesi za muda mrefu zinazoleta mlundikano wa mashauri.
Akizungumzia
suala la mashahidi, Mhe. Kainda alisema kuwa, matumizi ya teknolojia
yamerahisisha usikilizwaji wa mashahidi kwa njia ya mtandao (remote hearing),
hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya umbali na gharama.
Hata
hivyo, alionya kuwa baadhi ya mashauri huathirika kutokana na mapungufu katika
uendeshaji wake, akiwataka Mahakimu na wadau kuongeza umakini katika maandalizi
na usikilizwaji wa mashauri ili kulinda haki za wahusika wote katika shauri
husika. Pia alikemea vitendo vya rushwa na ucheleweshaji wa majalada ya kesi,
akisisitiza kuwa maadili na uadilifu vinapaswa kupewa kipaumbele katika utoaji
wa haki.
Katika
jitihada za kurahisisha huduma kwa wananchi, Jaji Kainda alieleza kuwa,
utambulisho wa wadhamini unaweza kuthibitishwa kwa kutumia Kitambulisho cha
Taifa (NIDA) pekee, bila ulazima wa kuwasilisha barua za utambulisho kutoka kwa
viongozi wa vijiji au Serikali za mitaa.
Kwa
upande wa maboresho ya mifumo kiteknolojia, Mhe. Kainda alisema kuwa, Mahakama
Kuu Lindi na Mahakama zake za chini zimeshanza kutumia mfumo wa kielektroni
(paperless), hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kupunguza matumizi ya
karatasi.
Jaji
Mfawidhi huyo, ameyahimiza mabaraza ya ardhi kuhakikisha yanatoa nakala za
hukumu kwa wakati ili kuwawezesha wananchi kupata haki zao bila ucheleweshaji
usio wa lazima.
Wadau
walikubaliana juu ya umuhimu wa ushirikiano, uwajibikaji na matumizi ya
teknolojia katika kuimarisha utoaji wa haki, hatua inayotarajiwa kuongeza
ufanisi wa Mahakama katika utoaji wa haki kwa wananchi.
Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi akiwasilisha Mada wakati wa Kikao na Wadau. Wengine ni Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema (kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela (kulia)
Naibu Msajili Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Lindi Mhe. Elia Joseph Mrema akizungumza jambo wakati wa kikao hicho.
Mdau wa Mahakama Kutoka Ofisi ya Huduma ya Uangalizi wa Jamii Bi. Wilhelmina Qambalo akitoa hoja wakati wa kikao hicho.
Wadau wakifuatilia kwa Makini Mada
zilizokuwa zinawasilishwa wakati wa kikao.





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni