Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita
Mahakama
Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, imeendelea kujipambanua katika matumizi
ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), baada ya kupokea ugeni kutoka
Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara ya Dar es Salaam pamoja na Mahakama Kuu Masjala
Ndogo Singida.
Lengo
la ziara hizo lilikuwa ni kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya
TEHAMA katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama.
Ugeni
wa kwanza uliwasili tarehe 16 Aprili, 2026 ukitokea Mahakama Kuu Divisheni ya
Biashara, ukiwa na wajumbe wanane ukiongozwa na Naibu Msajili, Mhe. Suzan
Kihawa, pamoja na Mtendaji wa Mahakama, Anatory Kagaruki.
Ugeni
wa pili ulitoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo Singida, ukiwa na Watumishi tisa,
wakiongozwa na Naibu Msajili, Mhe. Evodia Kyaruzi, pamoja na Mtendaji wa
Mahakama, Filbert Matotay.
Katika
ziara hiyo, kulifanyika mafunzo yaliyofunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, ambaye aliwakaribisha wageni na
kuwashukuru kwa kuchagua Geita kama Kituo cha kujifunza.
Alieleza
kuwa ziara hiyo ni fursa muhimu ya kubadilishana mawazo na uzoefu kwa lengo la
kuboresha utoaji wa huduma za Mahakama kwa kutumia TEHAMA.
Jaji
Mhina alibainisha kuwa mafanikio ya Mahakama Kuu Geita yametokana na misingi
madhubuti iliyowekwa tangu kuanzishwa kwake, ikiwemo maelekezo ya Viongozi
wakuu wa Mahakama, yaliyosisitiza umuhimu wa kuifanya Mahakama kuwa ya kisasa
kidijitali.
Aliongeza
kuwa matumizi ya TEHAMA yameongeza uwazi, yamepunguza gharama za uendeshaji,
yamerahisisha upatikanaji wa taarifa na kuboresha mifumo ya ukaguzi wa shughuli
za Mahakama.
Aidha,
Jaji Mfawidhi alieleza kuwa mafanikio hayo yanatokana na mambo mbalimbali,
ikiwa ni pamoja na ukaguzi wa mara kwa mara wa mifumo, usimamizi thabiti wa Watumishi,
ufuatiliaji wa karibu wa utendaji kazi, utoaji wa motisha, pamoja na kuimarisha
ushirikiano miongoni mwa Watumishi bila kujali kada zao.
Mafunzo
hayo yalihusisha jumla ya mada tano zilizowasilishwa na Watumishi mbalimbali wa
Mahakama, kwa lengo la kupeana uzoefu na kuboresha utendaji wa kazi.
Mada
hizo zilitolewa na Naibu Msajili, Mhe. Fredrick Lukuna, Mtendaji wa Mahakama
Bi. Masalu Kisasila, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe.
Mujuni Muchunguzi, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe.
Ally Mgomba, pamoja na Mtunza Kumbukumbu wa Mahakama Kuu Geita, Bi. Winfirda Ng’humbu.
Akizungumza
wakati wa mafunzo hayo, Mhe. Lukuna, alisisitiza kuwa mafanikio ya Taasisi
yoyote yanategemea mshikamano wa pamoja miongoni mwa Watumishi wake.
Alieleza
kuwa ni muhimu kuwa na malengo ya pamoja, kushirikiana kikamilifu katika
utekelezaji wa majukumu, kukubali makosa na kujifunza kutokana nayo, pamoja na
kuhakikisha upatikanaji wa vitendea kazi vya kutosha.
Aidha,
alihimiza utambuzi wa mapema wa changamoto zinazoweza kujitokeza ili
zisikwamishe utekelezaji wa malengo yaliyowekwa.
Kwa
upande wa mada ya utawala na matumizi ya TEHAMA, Mtendaji wa Mahakama Geita
alieleza kuwa wamefanikiwa kuendesha shughuli nyingi za kiutawala bila matumizi
ya karatasi.
Alifafanua
kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano wa Watumishi wote pamoja na
utayari wao wa kuendana na dira ya uongozi wa Mahakama Kuu Geita ya kuimarisha
matumizi ya TEHAMA.
Akizungumza
kwa niaba ya wageni, Mhe. Kihawa alitoa shukrani kwa mapokezi mazuri pamoja na
mafunzo waliyoyapata, akieleza kuwa uzoefu huo utasaidia kuboresha utendaji
katika Mahakama zao.
Naye
Mhe. Kyaruzi alieleza kuridhishwa na mafunzo hayo na kuahidi kutumia maarifa
hayo kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika Masjala zao.
Wageni
walipata fursa ya kujionea kwa karibu namna Mahakama Kuu ya Geita
ilivyofanikiwa kufikia hatua ya matumizi kamili ya TEHAMA katika utoaji wa
huduma zake.
Kupitia
uzoefu huo, wageni hao waliondoka wakiwa na matarajio na dhamira ya kutekeleza
maboresho makubwa zaidi katika maeneo yao ya kazi, wakilenga kuiga na
kuendeleza mifumo waliyoishuhudia.
Lengo
kuu ni kuhakikisha kuwa wanakuwa sehemu ya mabadiliko chanya yatakayochochea
utoaji wa huduma za haki kwa Wananchi kwa ufanisi zaidi, uwazi ulioboreshwa na
kwa wakati muafaka.
Kwa
mtazamo wa jumla, ziara hizi zimekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha
matumizi ya TEHAMA ndani ya Mahakama za Tanzania.









Hakuna maoni:
Chapisha Maoni