Na ASHA JUMA- Mahakama Morogoro.
Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro,
imeendesha mafunzo maalumu kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo pamoja na Makarani kuhusu matumizi ya mfumo wa kuhifadhi mienendo, vielelezo na hukumu ikiwa ni
sehemu ya kuimarisha matumizi ya teknolojia katika utoaji haki.
Mafunzo hayo yalifanyika jana tarehe 22 Aprili, 2026, katika Ukumbi wa Mikutano
uliopo katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Morogoro, sambamba na njia
ya mtandao (online) ili kuwezesha ushiriki mpana.
Mafunzo hayo yaliendeshwa na kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) Morogoro, kikiongozwa na Mkuu wa Kitengo hicho pamoja na Mwanzilishi
wa mfumo huo, Bw. Justine Kemhe. Aidha, mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Amiri
Msumi.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo
hayo, Mhe. Msumi alikishukuru kitengo cha TEHAMA kwa ubunifu wao katika
kuanzisha mfumo huo unaoitwa unaoitwa Primary Court Depository, akieleza
kuwa ni hatua muhimu katika kuboresha utendaji kazi wa Mahakama.
Pia aliwahimiza washiriki kutoa ushirikiano wa kutosha pale changamoto
zitakapojitokeza ili kuhakikisha mfumo unaboreshwa zaidi.
“Hongereni sana kwa kutafsiri mawazo ya watu
na kuyaweka katika utekelezaji. Nawasihi Mahakimu na watumiaji wote wa mfumo
huu kuwasilisha changamoto na maoni yao ili kuboresha mfumo huu,” alisema Mhe.
Msumi.
Mfumo wa Primary Court Depository ni
sehemu ya jitihada za kuendeleza matumizi ya TEHAMA katika Mahakama ya Tanzania.
Mfumo huu unasaidia kurahisisha upatikanaji wa mienendo ya mashauri kutoka Mahakama za Mwanzo
pamoja na kuhifadhi kumbukumbu hizo kidijitali, hivyo kupunguza usumbufu wa
kutafuta nyaraka kwa njia za kawaida.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA
alibainisha umuhimu wa kuongeza vifaa vya TEHAMA kama kompyuta na skana ili
kuhakikisha mfumo huo unafanya kazi kwa ufanisi zaidi. Aliongeza kuwa mfumo huo
tayari umeanza kutumika katika baadhi ya Masjala nyingine, zikiwemo Simiyu na Geita.
Naye Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro, Mhe. Janeth Kinyage,
alisisitiza umuhimu wa washiriki kuzingatia maelekezo waliyopewa wakati wa
mafunzo hayo, akieleza kuwa mfumo huo utarahisisha kazi na kuondoa changamoto
ya upatikanaji wa mienendo ya mashauri.
Mafunzo haya yanatarajiwa kuleta mabadiliko chanya katika utendaji kazi wa Mahakama za Mwanzo kwa kuongeza ufanisi, uwazi na uhifadhi bora wa kumbukumbu za mashauri kwa njia ya kisasa (kidijitali).
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni