Ijumaa, 17 Aprili 2026

MANYARA YAENDESHA MAFUNZO YA USULUHISHI KWA WADAU

Na. CHRISTOPHER MSAGATI - Mahakama, Manyara

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora amejumuika na wadau wa Mahakama katika kuendesha mafunzo ya Wiki ya Usuluhishi yakiwa na lengo la kuwajengea wadau wa haki madai uwezo wa kusuluhisha migogoro kwa njia za upatanishi, elimu hiyo ilitolewa katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Mhe. Kamuzora alieleza kuwa, usuluhishi ni silaha ambayo inamaliza na kutatua migogoro na matatizo katika jamii kuliko hata kufika mahakamani na kusikiliza mashauri.

“Tukiachana na mashauri ya jinai yanayohusu makosa au uhalifu mkubwa, mashauri mengi ya madai yanaweza kwisha kwa kutumia Suluhu ambazo tunaweza kufanya wenyewe. Usuluhishi unasaidia sana katika kuokoa muda na gharama ambazo tunaweza kuzitumia wakati tumefungua mashauri mahakamani,” alieleza Mhe. Kamuzora.

Akitoa neno la utangulizi, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo, aliwaasa watu wote kutumia muda wao kusikiliza elimu ambayo itatolewa kwa sababu ni ya msingi sana na ina tija katika kutatua migogoro mbalimbali katika jamii.

“Wananchi wengi mnafika mahakamani kwa ajili ya kutatua migogoro ambayo kimsingi mngeweza kuimaliza wenyewe kwa sababu mmekosa elimu hii ya usuluhishi. Hivyo, ninawasihi sana msikilize kwa makini yale ambayo yatakuwa yanafundishwa na wataalamu wetu,” alisema Mhe. Mpepo.

Naye, Wakili wa Kujitegemea Bw. Kuyengwa Ndonjekwa alisema kuwa, elimu hiyo ni muhimu sana kuendelea kutolewa mara kwa mara kwa sababu ina madhumuni ya kupunguza mzigo mkubwa kwa Mahakama wa kusikiliza mashauri na kuwafanya wananchi wapatane wenyewe kuliko kuendelea kuleta mashauri mahakamani hususan kwa masuala ambayo yanaweza kuzungumzika na suluhu ikapatikana.

Kwa upande wake mdau wa Mahakama Bw. Gwandu Nada ambaye ni mwananchi kutoka katika Wilaya ya Babati aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kufanya elimu hiyo ya upatanishi kuwa endelevu kwani itaisaidia jamii kuokoa muda wa kwenda mahakamani kutatua migogoro isiyokuwa na tija.

“Mafunzo haya ni mazuri kwa kuwa yamenifundisha kupatana na washtaki wangu mapema kabla ya kufikishana katika vyombo vya sheria na ninaahidi kwenda kupatana na wale ambao nimekosana nao kwa njia ya usuluhishi,” alisema Bw. Nada.

Waliohudhuria kupata elimu hiyo ni wadau wa Mahakama pamoja na wadaawa waliofika kwa ajili ya kupata mafunzo ya usuluhishi, Watumishi wa Mahakama Kuu Manyara, Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi, Mwakilishi kutoka Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia, Ofisi ya Ustawi wa Jamii pamoja na baadhi ya wananchi.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora akitoa neno wakati wa utoaji elimu ya Usuluhishi iliyofanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu. Kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo na kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara Mhe. Mariam Lusewa.

Sehemu ya wananchi wakifuatilia mafunzo ya upatanishi 

Afisa Huduma kwa Jamii Mkoa wa Manyara Bw. Tumaini Moshi akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi waliofika Mahakama Kuu Manyara kupata elimu hiyo.

Mwananchi wa Wilaya ya Babati akitoa maoni yake wakati wa mafunzo elimu ya Wiki ya usuluhishi yaliyofanyika katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Victor Kimario akitoa elimu ya usuluhishi kwa wananchi waliofika Mahakama Kuu Manyara kupata elimu hiyo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Bernard Mpepo kushoto akizungumza na mmoja wa Wananchi waliofika kupata elimu ya upatanisho kwenye maadhimisho ya Wiki ya Usuluhishi. 

Sehemu ya wananchi waliohudhuria mafunzo ya wiki ya usuluhishi wakiwa katika picha ya Pamoja na Meza Kuu wakati wa utoaji elimu ya Wiki ya usuluhishi iliyofanyika katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

(Habari Hii imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni