Alhamisi, 16 Aprili 2026

WADAU WA SHERIA WANUFAIKA NA MAFUNZO MAALUM YA UTATUZI WA MIGOGORO

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu, Dodoma.

Mahakimu na Mawakili wa Mkoa wa Dodoma wameendelea kupatiwa elimu muhimu kuhusu utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi, hatua inayozidi kuimarisha mifumo ya haki na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za kisheria nchini.

Mafunzo hayo yaliyofanyika jana tarehe 15 Aprili, 2026 katika ukumbi wa Mahakama Kuu Dodoma kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) yamewakutanisha Wadau mbalimbali wa sekta ya sheria.

Lengo la mafunzo hay oni kujengeana uelewa wa kina kuhusu matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro (ADR), njia inayozidi kupata nafasi kubwa katika kuhakikisha haki inapatikana kwa haraka na kwa gharama nafuu.

Akitoa neno la ukaribisho, Naibu Msajili wa Mahakaa Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, aliwahimiza washiriki kutumia ipasavyo jukwaa hilo muhimu kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha weledi wao katika kushughulikia migogoro ya Wananchi.

Mafunzo hayo yaliendeshwa chini ya uratibu mahiri wa Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, ambaye ameendelea kuonesha uongozi thabiti, weledi wa hali ya juu pamoja na dhamira ya dhati ya kuendeleza usuluhishi nchini.

Kupitia jitihada zake, Wadau wa Sheria wameendelea kunufaika na elimu yenye tija, huku akihamasisha kwa vitendo matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama suluhisho endelevu.

Mada mbalimbali ziliwasilishwa wakati wa mafunzo hayo na wataalamu wa sheria, akiwemo Mhe. Thurstone Kombe, Mhe. Sarah Mwalilino, Mhe. Judith Barigenge pamoja na wengine kutoka Wizara ya Katiba na Sheria na Taasisi nyingine kama CHRAGG.

Mada hizo zilieleza kwa kina umuhimu wa usuluhishi katika kupunguza migogoro, kuokoa muda na gharama, pamoja na kuimarisha mahusiano katika jamii.

Akisimamia majadiliano, Mhe.  Dkt. Khalfan alisisitiza kuwa usuluhishi si tu njia mbadala, bali ni nyenzo muhimu ya kujenga jamii yenye amani na mshikamano, huku akitoa wito kwa Wadau wa Sheria kuendelea kuipa kipaumbele.

Washiriki walipata nafasi ya kuuliza maswali na kuchangia hoja mbalimbali, hali iliyoonesha mwitikio mkubwa na uhitaji wa elimu hiyo katika jamii ya Wanasheria.

Akitoa neno la shukrani, Mhe. Zabibu Mpangule aliwashukuru waandaaji pamoja na washiriki wote kwa ushiriki wao, akibainisha kuwa mafunzo hayo yameongeza thamani kubwa katika utendaji wao wa kila siku.

Mafunzo hayo yalihitimishwa kwa hotuba ya kufunga kutoka kwa Mkurugenzi Msaidizi wa Wizara ya Katiba na Sheria, aliyesisitiza umuhimu wa kuendeleza elimu ya usuluhishi ili kuhakikisha Wananchi wanapata haki kwa wakati, kwa ufanisi na kwa amani.

Kwa ujumla, tukio hili limeacha alama kubwa katika Mkoa wa Dodoma, likiwa ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za kuifanya Tanzania kuwa kinara wa matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati). Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mkurugenzi Msaidizi Kurugenzi ya Usuluhishi(ADR) Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Felix Chakila.


 

Mahakimu pamoja na Mawakili mbalimbali waliohudhuria elimu hiyo ya usuluhishi katika ukumbi uliopo Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma wakifuatilia kwa makini mafunzo hayo.

 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri, akitoa neno la ukaribisho kwa wajumbe hao waliohudhuria elimu ya usuluhishi kwa Mahakimu na Mawakili.

 Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan, akifuatilia kwa makini mada inayotolewa wakati wa utoaji wa elimu kwa Mahakimu na Mawakili.


 

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Mahakimu wa Dodoma walioshiriki mafunzo ya Mahakimu pamoja na Mawakili kuhusu usuluhishi. Kushoto kwake ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri na kulia kwake ni Mkurugenzi Msaidizi Kurugenzi ya Usuluhishi(ADR) Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Felix Chakila.


Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt. Fatma Khalfan (wa pili kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na watoa ujumbe maalumu kuhusu elimu ya usuluhish,i ambao pia ni Watumishi wa Mahakama Dodoma wakati wa mafunzo hayo.


Meza Kuu ikiongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye pia ni Mratibu wa Usuluhishi wa Wiki ya Usuluhishi, Mhe. Dkt.Fatma Khalfan (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe walioshiriki mafunzo ya Mahakimu pamoja na Mawakili kuhusu usuluhishi.


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni