Jumapili, 26 Aprili 2026

JAJI MKUU MASAJU AHUDHURIA IBADA YA SHUKRANI KUMBUKIZI YA KUZALIWA BI. LOYCE NYALALI

Na MARY GWERA, Mahakama-Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 26 Aprili, 2026 amehudhuria Ibada maalum ya shukrani ya kusherehekea kumbukizi ya miaka 80 ya kuzaliwa kwa Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali.

Ibada hiyo maalum ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai imefanyika katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro Oysterbay jijini Dar es Salaam ikiongozwa na Paroko wa Kanisa hilo, Padri Bartholomew Mrosso na Padri mwenzake.

Katika mahubiri yake wakati wa ibada hiyo, Padri Mrosso ametoa rai kwa Waumini kumshukuru Mungu kwa uzima kwa kuwa uzima ni zawadi kubwa ambayo kwayo yatupasa kumshukuru Mungu. Amesisitiza kwa kusema, “tumshukuru Mungu kwa uzima kwanza halafu vingine ndio vifuate.”

Kadhalika Padri huyo, amewakumbusha Viongozi kusimamia haki, na kutenda mema kwa walio chini yao na wanaowaongoza.

“Katika Injili ya Jumapili ya leo ya Mchungaji Mwema msingi wake ni Uongozi, namna fulani ya Uongozi ambao Kristo anaudhihirisha kupitia matendo yake mema,” ameeleza.

Ameongeza kuwa, Kiongozi anapaswa kusimama kwa ajili ya wale anaowaongoza hivyo, Uongozi usichukuliwe kama ajira bali kujitoa na kuwajali watu waliopo chini.

Ibada hiyo imehudhuriwa pia na baadhi ya Viongozi wakiwemo Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Joseph Sinde Warioba, Majaji Wastaafu wa Mahakama Rufani na Mahakama Kuu, Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Wakili Tom Nyanduga, Wenza wa Majaji Wakuu Wastaafu akiwemo Mama Marina Juma, Mama Sada Chande pamoja na ndugu, jamaa na marafiki na wageni wengine waalikwa.

Baada ya ibada hiyo, imefanyika sherehe maalum ya kumpongeza Bi. Loye Nyalali iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Kadinali Rugambwa uliopo pembeni ya Kanisa la Mt. Petro jijini Dar es Salaam.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (wa pili kushoto mwenye tai nyekundu) akiwa katika misa ya shukrani ya kusherehekea kumbukizi ya miaka 80 ya kuzaliwa kwa Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, marehemu Francis Nyalali. Ibada hiyo imefanyika leo tarehe 26 Aprili, 2026 katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro jijini Dar es Salaam. Kulia kwa Jaji Mkuu ni Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Joseph Sinde Warioba na aliyeketi mbele ni Mama Loyce Nyalali anayeadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimsalimia na kumpongeza Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali.
 
Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali akiingia ndani ya Kanisa Katoliki la Mtakatifa Petro lililopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya ibada maalum ya kumshukuru Mungu kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.

Bi. Loyce Nyalali, Mjane wa Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania, Marehemu Francis Nyalali akiwa katika uso wa furaha ikiwa ni siku yake maalum ya kuadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Stephen Bwana (kushoto) pamoja na mwenza wake (katikati) na wengine wakiwa katika ibada ya shukrani maalum kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Bi. Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.

Paroko wa Kanisa Katoliki la Mtakatifu Petro, Padri Bartholomew Mrosso akiongoza ibada maalum ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Mama Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake leo tarehe 26 Aprili, 2026.


Picha mbalimbali za matukio ya Ibada maalum ya kumshukuru Mungu kwa kumjaalia Bi. Loyce Nyalali kutimiza miaka 80 ya kuzaliwa kwake.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni