Ijumaa, 10 Aprili 2026

SERIKALI YASISITIZA UMUHIMU WA MATUMIZI YA NJIA MBADALA ZA UTATUZI WA MIGOGORO

  • Naibu Waziri asema usuluhishi nguzo muhimu katika mfumo wa utoaji haki nchini

Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dar es Salaam

Serikali imesisitiza umuhimu wa matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro, hususan usuluhishi, kama njia bora ya kuharakisha upatikanaji wa haki na kudumisha amani katika jamii.

Msisitizo huo umetolewa tarehe 9 Aprili, 2026 na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainabu Katimba, wakati akitoa salamu zake katika hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi 2026 uliofanyika katika ukumbi wa Golden Jubilee Tower, jijini Dar es Salaam.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, ambaye alikuwa mgeni rasmi pamoja na Viongozi mbalimbali wa Mahakama, Serikali, sekta binafsi na Wadau wa Sheria.

Uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi ulikuwa na kauli mbiu isemayo: “Kutumia njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama mbinu inayopendelewa nchini Tanzania.”

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Katimba amesema usuluhishi umeendelea kuwa nguzo muhimu katika mfumo wa utoaji haki nchini kutokana na uwezo wake wa kupunguza gharama, kuokoa muda na kulinda mahusiano ya kijamii na kiuchumi.

Aidha, ameeleza kuwa jitihada za kuimarisha usuluhishi zinaendana na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo inalenga kujenga mfumo wa haki wenye ufanisi na unaoweza kutoa huduma kwa wakati kwa Wananchi wote.

“Matumizi ya usuluhishi ni sehemu ya dhamira ya Serikali kuhakikisha Mahakama inakuwa chombo chenye ufanisi katika utoaji wa haki kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” amesema Mhe. Katimba.

Amefafanua kuwa tofauti na mwenendo wa kawaida wa mashauri mahakamani, usuluhishi hutoa fursa kwa pande zinazohusika kufikia makubaliano kwa hiari, kwa haraka na kwa gharama nafuu, hali inayochangia kuimarisha mshikamano na utengamano katika jamii.

Kwa mujibu wa Mhe. Katimba, Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria itaendelea kuunga mkono na kuimarisha matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro kwa kushirikiana na Mahakama ya Tanzania pamoja na Wadau mbalimbali.

Katika hatua nyingine, amesema Wiki ya Usuluhishi inayotarajiwa kufanyika kuanzia Aprili 13 hadi 17, 2026, itatoa fursa kwa Wananchi kupata elimu na huduma za usuluhishi bure katika Mahakama mbalimbali nchini.

Amesema hatua hiyo inalenga kuwahamasisha Wananchi kutumia zaidi njia za maelewano katika kutatua migogoro yao, badala ya kutegemea mashauri marefu na yenye gharama kubwa mahakamani.

Aidha, amewahimiza Wadau wa sekta ya sheria, wakiwemo Mawakili, Wasuluhishi na Watumishi wa Mahakama, kuendelea kuhamasisha matumizi ya usuluhishi pamoja na kutoa elimu kwa umma ili kuongeza uelewa na imani ya Wananchi katika mfumo huo.

Kwa upande wa Serikali, Mhe. Katimba amesema juhudi zinaendelea kufanyika katika kuboresha sekta ya sheria ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya Mahakama, kuongeza rasilimali watu na kuendeleza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuhakikisha haki inapatikana kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

Amesisitiza pia umuhimu wa maadili, weledi na uadilifu kwa Wasuluhishi ili kuhakikisha mchakato wa usuluhishi unafanyika kwa haki, uwazi na kwa kuzingatia misingi ya sheria.

Akihitimisha hotuba yake, Mhe. Katimba ametoa wito kwa Wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Wiki ya Usuluhishi na kutumia fursa hiyo kumaliza migogoro yao kwa njia ya amani na maelewano.

Uzinduzi huo umeacha mwamko mpya miongoni mwa wadau wa sekta ya sheria na jamii kwa ujumla, ukiashiria hatua muhimu katika juhudi za Serikali za kuimarisha upatikanaji wa haki kwa njia mbadala na endelevu nchini.

Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainabu Katimba, akitoa salama katika hafla ya uzinduzi wa Wiki ya Usuluhisho 2026 uliofanyika tarehe 9 Aprili 2026 katika ukumbi wa Golden Jubilee Tower jijini Dar es Salaam.

Viongozi mbalimbali wa Mahakama, Serikali, Sekta binafsi na wadau wa sheria walioudhuria katika hafla ya Wiki ya Usuluhishi 2026 iliyofanyika katika ukumbi wa Golden Jubilee Tower, jijini Dar es salaam.

 




Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.



 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni