Ijumaa, 10 Aprili 2026

WADAU WA SHERIA WAIBUA NGUVU YA USULUHISHI

  • Wahimiza njia za amani kutatua migogoro

Na HALIMA MNETE-Mahakama, Dar es Salaam

Wadau wa sekta ya sheria nchini wameeleza kwa kina namna usuluhishi unavyoendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuhakikisha Wananchi wanapata haki kwa haraka, nafuu na kwa njia ya amani, huku wakisisitiza umuhimu wa kuongeza uelewa kwa jamii kuhusu mfumo huo.

Maelezo hayo yametolewa tarehe 9 Aprili 2026, katika uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi 2026 uliofanyika katika ukumbi wa Golden Jubilee Tower, jijini Dar es Salaam, ambapo mgeni rasmi alikuwa Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.George Masaju.

Katika hafla hiyo, kulikuwepo na mjadala kabambe ulioongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Dkt. Eliamani Laltaika, ulioshirikisha Wadau mbalimbali waliotoa mitazamo yao kuhusu nafasi ya usuluhishi katika mfumo wa utoaji haki nchini.

Akichangia mada hiyo, Mtaalamu wa Usuluhishi na Mwanzilishi wa Taasisi ya ESS Creative and Legal Foundation, Bw. Eric Mukiza, alisisitiza kuwa mawasiliano ndiyo msingi mkuu wa mafanikio ya usuluhishi.

Alibainisha kuwa ujumuishi (inclusion) ni jambo la msingi, hasa kwa watu wenye ulemavu, ili kuhakikisha kila mmoja anapata fursa sawa ya kusikilizwa na kushiriki kikamilifu katika mchakato wa utatuzi wa migogoro.

Kwa upande wake, kiongozi wa dini, Sheikh Zaila Hassan, alieleza kuwa usuluhishi una mizizi ya kiimani, akisisitiza kuwa ni wajibu wa Wasuluhishi kuzingatia haki, uadilifu na hofu ya Mungu katika kutekeleza majukumu yao.

Naye Chifu Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mtemi Henry Mazengo wa Pili, aligusia umuhimu wa mila na desturi katika kuendeleza utatuzi wa migogoro kwa njia ya maelewano, akibainisha kuwa jamii nyingi za kiafrika zimekuwa zikitumia mbinu hizo tangu zamani kudumisha amani na mshikamano.

Akizungumza kwa upande wa sekta ya fedha, Bw. Ramadhani Myonga kutoka Benki Kuu ya Tanzania alieleza kuwa hapo awali kulikuwepo changamoto za mifumo ya kushughulikia migogoro ya kifedha kutokana na kukosekana kwa miongozo mahsusi (internal guidelines), hali iliyosababisha malalamiko kutoka kwa wananchi.

Hata hivyo, alisema maboresho yaliyofanyika yamewezesha kuanzishwa kwa mfumo wa “Sema na BoT” unaorahisisha Wananchi kuwasilisha na kutatua malalamiko yao bila gharama.

Kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Bw. Peter Ernest Mogoro alieleza kuwa moja ya majukumu ya Wizara hiyo ni kusaidia Wananchi kutatua changamoto zao kupitia njia mbadala za utatuzi wa migogoro, ikiwemo usuluhishi. Aliongeza kuwa programu kama “Mama Samia Legal Aid” zimekuwa msaada mkubwa kwa Wananchi katika kupata haki.

Naye Bw. Lucas Malunde kutoka Ofisi ya Rais – TAMISEMI, alisisitiza kuwa Taasisi hiyo inalenga kuhakikisha uwepo wa utangamano ndani ya jamii kwa kuhimiza matumizi ya usuluhishi katika ngazi za chini za utawala.

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi, alibainisha kuwa chama hicho kinaendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu umuhimu wa usuluhishi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kupunguza migogoro inayofikishwa mahakamani.

Kwa ujumla, Wadau hao walikubaliana kuwa usuluhishi umeleta manufaa makubwa kwa wananchi kwa kuokoa muda na gharama, huku ukitoa nafasi ya kufikia suluhu za kudumu kwa njia ya maelewano badala ya migogoro ya muda mrefu mahakamani.

Uzinduzi wa Wiki ya Usuluhishi 2026 umefanyika chini ya kauli mbiu isemayo: “Kutumia njia mbadala za utatuzi wa migogoro kama mbinu inayopendelewa nchini Tanzania,” ikiwa ni jitihada za kuhamasisha matumizi ya mfumo huo kwa manufaa ya jamii nzima.

 


Wadau mbalimbali walioshiriki kwenye mjadala wakiwa kwenye picha ya pamoja. Picha chini ni wageni mbalimbali aliohudhuria uzinduzi wa Wiki ya Uuluhishi nchini.




Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni