Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma
Waziri wa Katiba na
Sheria, Mhe. Dkt. Juma Zuberi Homera, amesema leo tarehe 24 Aprili, 2026 kuwa, usikilizaji
na umalizaji wa haraka wa mashauri yaliyopo mahakamani una mchango mkubwa kwa
Taifa kiuchumi na kijamii
Akiwasilisha bungeni
Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha
2026/2027, Mhe. Dkt. Homela ameeleza pia kuwa suala la kuharakisha usikilizaji
wa mashauri mahakamani ni moja ya vipaumbele muhimu vya Mahakama ya Tanzania
katika kuhakikisha kuwa Wananchi wote wanapata haki kwa wakati.
Ameliambia Bunge kuwa katika
kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026, kulikuwa na jumla ya mashauri 205,038
mahakamani na kati ya hayo, 45,187 yalianza mwaka 2024/ 2025, yaani yalikuwepo
kabla ya tarehe 30 Juni, 2025, na mashauri 159,851 yalifunguliwa katika mwaka
wa fedha 2025/2026.
“Kati ya mashauri 205,038
yaliyokuwepo, mashauri 166,553 yalisikilizwa na kuhitimishwa na mashauri 38,485
yanaendelea katika hatua mbalimbali. Aidha, mashauri yenye umri mrefu
mahakamani ni 3,675,” Waziri Homela amesema.
Amebainisha kuwa katika
kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026, kasi ya uondoshaji wa mashauri mahakamani
(case clearance rate) ni asilimia 104, huku uwezo wa umalizaji wa mashauri
(disposal rate) ni asilimia 81.
Akizungumzia mchango wa usikilizaji
na umalizaji wa haraka wa mashauri mahakamani kwa Taifa kiuchumi na kijamii,
Waziri Homela ameeleza kuwa katika zoezi maalum la kusikiliza mashauri ya
kiuchumi na kibiashara lililofanywa na Mahakama Oktoba na Novemba, 2025
lilifanikisha umalizaji wa mashauri 2,973.
“Kuhitimishwa kwa
mashauri hayo kuliwezesha kuachilia jumla ya shilingi za Kitanzania trilioni
13.1 zilizokuwa zimeshikiliwa na mashauri hayo kuingia kwenye mzunguko wa uchumi,”
amesema.
Akizungumzia ukaguzi na
usimamizi wa shughuli za kimahakama katika ngazi ya Mahakama ya Hakimu Mkazi,
Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo kwa Masjala Ndogo 20 za kimahakama,
Mhe. Dkt. Homela amesema kuwa zoezi hilo limefanyika kwa asilimia 100.
“Matokeo ya ukaguzi huo
yamewezesha kuongeza kasi ya umalizaji mashauri mahakamani kwa kuwa huambatana
na ukaguzi wa jalada moja baada ya jingine,” Waziri Homela ameliambia Bunge
wakati anawasilisha hotuba yake.
Ameeleza vilevile kuwa Magereza
129 kati ya 130 yaliyopo yalikaguliwa, sawa na asilimia 98.8 ikilinganishwa na
ukaguzi wa kipindi kama hiki katika mwaka 2024/2025 uliofanyika kwa asilimia
80.2.
Waziri pia ameeleza kuwa
katika mwaka 2025/2026, Mahakama ya Tanzania imeendelea kushirikiana na Wadau
wake katika mnyororo wa haki jinai ili kuhakikisha mashauri yanamalizika kwa
wakati.
Amebainisha kuwa tarehe
12 na 13 Machi, 2026 Mahakama iliitisha kikao kazi cha pamoja kilichohusisha Wadau
kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Mamlaka ya Maabara ya Mkemia
Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka.
Waziri Homela ametaja
Wadau wengine waliohudhuria kikao kazi hicho kama Chama cha Wanasheria
Tanganyika, Idara ya Ustawi wa Jamii, Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza pamoja
na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya.
“Kupitia kikao hicho,
wajumbe walijadili taarifa ya hali ya mashauri ya mlundikano hadi kufikia
Desemba, 2025, hali ya mahabusi magerezani na mikakati ya kupunguza mlundikano
pamoja na kuongeza matumizi ya TEHAMA kwenye usikilizaji wa rufaa na maombi,”
amesema.
Kwa mujibu wa Mhe. Dkt.
Homela, kikao hiki kimesaidia kupata ufumbuzi wa pamoja wa changamoto
mbalimbali, ikiwemo kuongeza kasi ya umalizaji wa 36 mashauri mahakamani, na
kila mdau kutekeleza wajibu wake kwa wakati.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni